Maandalizi ya Sensa ya Watu na Makazi mwaka 2022 yashika kasi nchini

Na Rotary Haule,Diramakini Blog

SIKU chache baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kumteua aliyekuwa Spika wa Bunge, Anne Makinda kuwa Kamishna wa Sensa Tanzania Bara na Rais wa Zanzibar, Dkt. Hussein Mwinyi kumteua Balozi Mohamed Hamza tayari wawili hao wamekutana kwa mara ya kwanza Mjini Kibaha kwa ajili ya kufanya ziara ya kukagua maandalizi ya vituo vilivyopangwa kwa ajili ya kufanyia Sensa ya mwaka 2022.

Ziara ya makamishna hao imefanyika kwa kumshirikisha Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Sarah Msafiri na wataalamu wa masuala ya Sensa ambapo walitembelea kituo cha Muheza kilichopo Kibaha Mjini, eneo ambalo litatumika katika sensa ya majaribio itakayofanyika Agosti, mwaka huu.

Katika ziara hiyo, Makinda amesema kuwa, lengo kubwa ya ziara yao ni kuangalia na kukagua maandalizi yaliyofanyika juu ya kutenga maeneo ambayo yatatumika katika kuhesabia watu katika Sensa ya mwaka 2022.

Makinda amesema kuwa, Sensa ya mwaka 2022 itakuwa ya kisasa na bora zaidi kwa kuwa imepangwa kufanyika mpaka ngazi ya kitongoji tofauti na ile ya 2010 iliyofanyika kwa kuishia ngazi ya wilaya.

Amesema kuwa,wameweka utaratibu mzuri wa kuhakikisha kila mtu anahesabiwa kwa wakati na kwamba kila kituo kitatumia kuhesabu kaya 50.

"Sensa ya mwaka 2022 itafanyika kwa kiwango cha juu kwa kuwa tumejipanga vizuri kuendesha zoezi hilo na tumeandaa vifaa vya kutosha vikiwemo Vishikwambi vitakavyotumika (Tablets) kwa hiyo wananchi wawe tayari kutoa ushirikiano mara baada ya zoezi hilo kuanza,"amesema Makinda.

Nae Kamishna wa Sensa kutoka Zanzibar, Balozi Mohamed Hamza amesema kuwa, kwa sasa wapo katika maandalizi ya awali ya kugawa maeneo ya Sensa na Kibaha ni miongoni mwa maeneo yatakayofanyikia Sensa ya majaribio.

Balozi Hamza,alitumia nafasi hiyo kueleza umuhimu wa Sensa na kusema kuwa Sensa inasaidia kupata idadi sahihi ya watu na hivyo kuifanya Serikali kutoa huduma za kijamii kulingana na idadi ya watu wake.

Amesema kuwa, Serikali inapokosa idadi sahihi ya watu inasababisha kushindwa kutoa huduma za kijamii kwa watu wake jambo ambalo linaweza kuwanyima haki wananchi.

"Umuhimu wa Sensa ni mkubwa kwa nchi zetu kwani tunapopata idadi sahihi ya watu ndipo inaposaidia Serikali kutoa huduma sahihi kulingana na watu wake kwahiyo tunaomba kila mwananchi hawe na utayari wa jambo hili,"amesema Balozi Hamza

Balozi huyo amewataka wataalamu waliopewa jukumu la kufanyakazi hiyo wahakikishe wanatumia lugha ya upole na unyenyekevu ili kila mwananchi ajisikie furaha kuhesabiwa kuliko kutoa matusi na dharau zitakazosababisha watu kuacha kuhesabiwa.

Kwa upande wake mrasimu ramani kutoka ofisi ya takwimu inayoshughulikia masuala ya Sensa Mkoa wa Pwani, Tumaini Komba kazi ya kugawa maeneo hayo ilianza Juni 18, mwaka huu.

Komba amesema, kazi hiyo ilianza katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha na baadae kumalizia Halmashauri ya Kibaha Mjini ambapo mpaka sasa maandalizi hayo yamefanyika vizuri .

Amesema kuwa,kwa Mtaa wa Muheza pekee wamefanikiwa kutenga maeneo madogo madogo 17 ambapo kila eneo litakuwa na kaya 50 za watu watakaohesabiwa.

Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Sarah Msafiri,amesema kuwa amefurahishwa na hatua ya kupewa kipaumbele kwa eneo lake kuwa sehemu ya kufanyika kwa Sensa ya majaribio Agosti, mwaka huu.

Hata hivyo, Msafiri aliwaomba wataalamu hao kuendelea kushirikiana kwa kila jambo hili kuhakikisha wanatatua kwa pamoja changamoto zinazojitokeza na kufanya zoezi la sensa litakapoanza liwe la mafanikio zaidi.

Kamishna wa Sensa Tanzania Bara Anna Makinda (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa mrasimu ramani wa Sensa ya mwaka 2022, Tumaini Komba( katikati ) namna walivyotenga maeneo ya vituo vya Sensa katika eneo la Muheza Kibaha Mjini,Makinda alifanya ziara juzi ya kukagua maandalizi na maeneo ya vituo vya Sensa na kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Sarah Msafiri. (Picha na Rotary Haule).

Maana ya Sensa ya Watu na Makazi

Sensa ya watu na makazi ni utaratibu wa kukusanya, kuchambua, kutathimini na kuchapisha na kusambaza takwimu za kidemographia, kiuchumi na kijamii kuhusiana na watu wote na makazi yao katika nchi kwa kipindi maalum. Kwa maana nyingine, sensa ni zoezi maalum lenye lengo la kupata idadi ya watu wote katika nchi, kwa umri na jinsia, mahali wanapoishi na hali yao ya elimu, hali ya ajira, hali ya vizazi na vifo na hali ya makazi. Takwimu hizi za msingi ndiyo zinazoweza kuanisha mahitaji halisi ya wananchi yakiwemo makundi maalum yenye uhitaji maalum kwa mfano, watu wenye ulemavu, wanawake, watoto, vijana na wazee hivyo kurahisisha uandaaji wa sera na mipango ya maendeleo kulingana na uhitaji na mazingira yaliyopo.

 

Umuhimu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022

Umuhimu wa kipekee wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 ni pamoja na:-

  1. Kuisadia Serikali kupata taarifa za msingi zitakazosaidia mchakato wa utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya mwaka 2025, mageuzi ya masuala ya afya na jamii, pamoja na ufuatiliaji wa ajenda za maendeleo za kimataifa;

  2. Taarifa za idadi ya watu husaidia katika mamlaka za wilaya katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo ambayo huakisi matakwa ya watu katika ngazi husika na kusaidia kwenye uwiano wa mgawanyo wa rasilimali;

  3. Taarifa za msingi za hali ya kidemografia, kijamii na kiuchumi za idadi ya watu na makazi za mipango katika ngazi zote;

  4. Kigawio katika kukokotoa viashiria vingine mfano Pato la mtu mmoja mmoja, Pato la Taifa, Ajira na ukosefu wa Ajira na kiwango cha uandikishaji wa wanafunzi;

  5. Taarifa itakayowezesha serikali kujua ongezeko la idadi ya watu, kwa mgawanyo na viashiria vingine, ambavyo ni muhimu kwa usimamizi wa mazingira; na

  6. Msingi wa utawala bora na ujumuishaji wa demokrasia. Takwimu sahihi za Sensa zinahitajika kwa ajili ya ugawaji wa majimbo ya uchaguzi kwa ufanisi, kurekebisha mipaka ya kiutawala katika serikali za mitaa.

 

Madodoso ya Sensa

Sensa ya mwaka 2022 kama zilivyo sensa zilizopita itatumia aina mbili kuu za madodoso. Dodoso refu litakalotumika kuhoji asilimia 30 ya maeneo yote ya kuhesabia watu na Dodoso fupi litakalotumika kuhoji kwenye asilimia 70 ya maeneo yote ya kuhesabia watu.

Madodoso Mengine ni:-

  • Dodoso la Taasisi ambalo ni mahsusi kwa ajili ya wasafiri, waliolala mahotelini/nyumba za wageni, na waliolazwa hospitalini; na

  • Dodoso la Wasio na Makazi maalum ambalo ni mahsusi kwa watu wote wanaolala maeneo yasiyo rasmi, kwenye baraza za majengo mbalimbali, kwenye madaraja na maeneo mengine.

 

Maandalizi ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022

Utekelezaji wa sensa ya watu na makazi hufanyika katika awamu kuu tatu kuu ambazo ni Kipindi Kabla ya Kuhesabu Watu, Wakati wa Kuhesabu Watu na Kipindi Baada ya Kuhesabu Watu.

Kipindi Kabla ya Kuhesabu Watu

Kipindi kabla ya kuhesabu watu kinajumuisha Uandaaji wa Kitabu cha Mkakati wa Usimamizi na Utekelezaji wa Sensa na nyaraka nyingine, Utengaji wa Maeneo ya Kuhesabia Watu na Uzalishaji wa Ramani, Uandaaji wa Nyenzo (Madodoso na Miongozo mbalimbali); Uhamasishaji, Sensa ya Majaribio ifikapo tarehe 29 Agosti 2021 ikiwa ni mwaka mmoja kamili kabla ya Sensa yenyewe; Kuunda kamati za sensa; kufanya mikutano na wadau wa takwimu; kufanya manunuzi, kufanya uchaguzi wa aina ya teknolojia itakayotumika, kuajiri wadadisi na wasimamizi, usambazaji wa vifaa; na kufanya maandalizi ya Tathmini ya Sensa.

 

Kipindi cha Kuhesabu Watu

Kipindi cha kuhesabu watu kinajumuisha kazi kuu na ya muhimu katika zoezi hili ya kuhesabu watu.

 

Kipindi Baada ya Kuhesabu Watu

Kipindi baada ya kuhesabu watu kinajumuisha Uchakataji wa Taarifa za Sensa, Uchambuzi, Utoaji wa Matokeo ya Awali, Usambazaji wa matokeo ya mwisho, uhamasishaji wa matumizi ya takwimu kwa watumishi wa Wizara, Idara na Taasisi za Serikali.

 

Maandalizi ya sensa ya watu na makazi 2022 yalianza 2018, ikiwa ni kutenga maeneo ya kuhesabia watu, kutayarisha nyaraka muhimu za sensa kama vile madodoso, miongozo, fomu za kudhibiti ubora na kufanya sensa ya majaribio.

 

Kwa sasa maandalizi ya sensa yamefikia katika hatua zifuatazo;

  1. Kuandaa Kitabu cha Mkakati wa Usimamizi na Utekelezaji wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022;

  2. Kutenga Maeneo katika wilaya 5 za mkoa wa Dodoma ambazo ni Bahi, Chamwino, Kondoa, na Chemba; na Wilaya moja ya Mkoa wa Singida (Singida Mjini);

  3. Kazi ya kutenga maeneo ya kuhesabia watu inaendelea katika mkoa wa Singida katika wilaya za Manyoni, Ikungi; na mkoani Dodoma katika wilaya za Mpwapwa na Kongwa.

  4. Kufanyika kwa ziara moja ya kimafunzo nchini Kenya kwa ufadhili wa UNFPA ambao wamefanya sensa ya kidigitali hivi karibuni na kujifunza matumizi ya teknolojia ya kisasa katika kufanya sensa kwa mafanikio. Matumizi ya teknolojia hii itasaidia kupunguza gharama za kufanya sensa na kupunguza muda wa kutoa matokeo ya sensa.

  5. Kuandaa rasimu ya Dodoso la Sensa na nyaraka nyingine muhimu kama vile miongozo ya kufundishia, miongozo ya makarani wa sensa, miongozo ya wasimamizi wa sensa na miongozo ya waratibu wa sensa mkoa na wilaya.

 

Maswali Yatakayoulizwa katika Sensa ya mwaka 2022

Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 ina moduli kumi na nne ambazo zitatumika kukusanya taarifa za watu na makazi yao nchi nzima.

 

Maswali yatakayoulizwa yatahusu:-

  1. Taarifa za kidemografia (umri, jinsi, uhusiano, hali ya ndoa, uraia, n.k.);

  2. Maswali yanayohusu ulemavu;

  3. Taarifa za Elimu;

  4. Maswali ya uhamaji, pamoja na taarifa za Watanzania wanaoishi nje ya nchi

  5. Maswali kuhusu umiliki wa nyaraka za kitaifa (vitambulisho vya NIDA, Mzanzibari mkazi, cheti cha kuzaliwa, hati ya kusafiria, na leseni ya udereva)

  6. Shughuli za kiuchumi

  7. Umiliki wa ardhi na taarifa za TEHAMA

  8. Taarifa za Uzazi na Vifo vilivyotokea ndani ya kaya

  9. Vifo vitokanavyo na uzazi

  10. Hali ya nyumba za kuishi na umiliki wa rasilimali mbalimbali

  11. Maswali ya kilimo na mifugo

  12. Mifuko ya hifadhi ya jamii.

 

Tofauti ya Sensa ya Mwaka 2022 na Sensa zilizopita:-

Katika sensa ya mwaka 2022 inatarajiwa kuwa na vitu vipya kama vile;

  • Kutenga maeneo ya kijiografia ya kuhesabia watu katika ngazi za kitongoji/mtaa na upatikanaji wa taarifa za kitakwimu katika ngazi za kitongoji/mtaa pamoja na kuwa na mipaka ya kudumu katika ngazi hizo;

  • Matumizi ya Vishikwambi (tablets) katika hatua zote za utekelezaji wa sensa kwa lengo la kupunguza gharama;

  • Nyongeza ya maswali yatakayowezesha upatikanaji wa taarifa zaidi za kitakwimu ikilinganishwa na Sensa ya Mwaka 2012:-

  1. Taarifa za kidemografia (umri wakati wa ndoa ya kwanza);

  2. Maswali yanayohusu ulemavu (Kichwa kikubwa, Mgongo wazi, Kifafa/Epilepsy, Mbalanga/storiasis na Usonji/autism);

  3. Maswali ya uhamaji kulingana na mapendekezo ya IOM (International Organization of Migration);

  4. Maswali kuhusu umiliki wa nyaraka za kitaifa (vitambulisho NIDA, vitambulisho vya wafanyabiashara wadogo wadogo, Mzanzibari mkazi, hati ya kusafiria, na leseni ya udereva);

  5. Maboresho ya maswali ya shughuli za kiuchumi ikiwa ni pamoja na idadi ya kaya ziliko kwenye sekta isiyo rasmi;

  6. Umiliki wa ardhi na taarifa za TEHAMA

  • Takwimu za nyumba (orodha, hali ya umiliki na aina ya nyumba)

  • Maswali ya kilimo na mifugo

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news