Ujenzi vyumba vya madarasa Singida washika kasi, RAS Mwaluko atoa wito

NA MWANDISHI DIRAMAKINI

WATENDAJI wa Serikali katika ngazi ya Kata, Tarafa na vijiji mkoani Singida wametakiwa kutumia muda wao mwingi katika kusimamia ujenzi wa vyumba vya madarasa unaoendelea katika maeneo mbalimbali mkoani hapa ili kufanikisha ujenzi huo kwa wakati na kwa viwango vilivyokusudiwa.
RAS Singida Dorthly Mwaluko akitoa maelekezo kwa viongozi mbalimbali wa vijiji na kata kuhusu usimamizi wa ujenzi wa miradi ya vyumba vya madarasa kupitia fedha za UVIKO-19.

Mkoa wa Singida umepokea fedha za UVIKO-19 kiasi cha Shilingi Bilioni 13.24 kwa upande wa elimu ili kujenga vyumba vya madarasa 632 ambapo vyumba 330 ni kwa ajili ya shule za sekondari na 330 shule za msingi pamoja na mabweni mawili kwa ajili wenye mahitaji maalum ikiwa ni matarajio ya Serikali kwamba fedha hizo zitasimamiwa na kukamilisha ujenzi huo.

Kauli hiyo imetolewa Novemba 29,2021 na Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dorothy Mwaluko wakati akikagua miradi mbalimbali ya ujenzi wa vyumba hivyo katika Wilaya ya Mkalama ambapo amebainisha kwamba hali ya ujenzi inaendela vizuri na vyumba vingi vikiwa vimefikia katika hatua ya lenta na vingine vikisubiri kupauliwa.

RAS amewataka viongozi mbalimbali wa Serikali wakiwemo watendaji wa vijiji, Kata na Tarafa kuhakikisha haipiti siku bila kujua kinachoendelea katika miradi hiyo ambayo inatakiwa kukamilika kabla ya Desemba 15, mwaka huu.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, Asia Juma Mesossi akimuelezea RAS maendeleo ya ujenzi wa madarasa wilayani Mkalama.

Ziara hiyo ya RAS imehusisha viongozi mbalimbali wa Wilaya ya Mkalama ambapo walitembelea miradi katika shule ya Ibaga Kata ya Ibaga ambapo kunajengwa vyumba vitano vya madarasa, Shule ya Sekondari Nduguti kunakojengwa vyumba viwili, Shule ya Sekondari Gunda Kata ya Ilunda kunakojengwa chumba kimoja, Shule ya Sekondari Grace Mesaki kunakojengwa chumba kimoja, Kikhonda Sekondari kwenye ujenzi wa vyumba vitatu (3) na Shule ya Sekondari Iguguno kunakojengwa vyumba vinne vya madarasa .

Akiwa katika miradi hiyo, Dorothy Mwaluko ametuma ujumbe kwa wakuu wa shule zote mkoani Singida zenye miradi inayotumia fedha za UVIKO-19 kuhakikisha wanajenga kwa kufuata michoro iliyokubalika na kuhakikisha kwamba wanafanya mawasiliano ya karibu na wahandisi wa halmashauri za wilaya zao endapo kuna umuhimu wa kufanya hivyo ili kulinda ubora na viwango vilivyotajwa na wataalamu hao.
Katibu Tawala Mkoa wa Singida,Dorthly Mwaluko akiwa kwenye ziara ya kutembelea miradi ya ujenzi wa vyumba vitano vya madarasa katika Shule ya Sekondari Ibaga iliyopo Kata ya Ibaga mkoani Singida.

Aidha, RAS akawataka viongozi kuhakikisha wanazishirikisha kamati za ujenzi wa madarasa na kamati za mapokezi ya vifaa vya ujenzi, kiasi cha fedha zilizokuja na namna ya matumizi ya fedha hizo kama sehemu ya kuweka uwazi na kutengeneza dhana ya ushirikishwaji.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, Sophia Kizigo amesema wilaya imepokea fedha kwa ajili ya ujezi wa vyumba vya madarasa 63 na ya shule shikizi 16 ambazo kwa jitihada wanazofanya vyote vitakamilika ndani ya wakati.

DC Sophia amebainisha kwamba, hali ya ujenzi kwa sasa inaendelea vizuri baada ya kumaliza changamoto ya upatikanaji wa vifaa vya ujenzi ambavyo amesema vilikuwa havipatikani kwa kuwa zoezi la ujenzi wa vyumba vya madarasa unafanyika nchi nzima, hivyo kusababisha changamoto za upatikanaji wa vifaa hivyo.
Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, Sophia Kizigo akiongea na viongozi mbalimbali wa mkoa na halmashauri kuhusu maendeleo ya ujenzi.

Amesema, kwa sasa wilaya imeshanunua vifaa vyote vinavyohitajika katika ujenzi huo ambapo amebainisha kwamba asilimia 85 ya majengo yamefikia hatua ya kufungwa lenta wakati asilimia 15 vinafungwa mkanda wa katikati ili kuondoa nyufa zinazoweza kutokea.

DC amefafanua kwamba, mbao zitakazotumika kwa wilaya nzima tayari zimeshafika kilichobaki ni kuzisambaza kwenye shule mbalimbali na mpaka kufikia Novemba 30, 2021 jioni mabati nayo yatakuwa yamefika.

Wakimalizia ziara hiyo katika shule Sekondari Iguguno, DC Sophia amezitaka kamati za mapokezi na za ujenzi kujipanga kupokea vifaa hivyo ambapo watatakiwa kuongeza usimamizi ili kupata thamani ya fedha zilizotumika.

Mwisho DC Kizigo akamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha hizo katika Wilaya ya Mkalama jambo ambalo amesema limeondoa kabisa changamoto ya uhaba wa madarasa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news