BUNDI WA GAMBOSHI SEHEMU YA 44

NA WILLIAM BOMBOM

Ilipoishia... lilipita Juma moja tukiwa kwenye ya ujenzi wa GAMBOSHI MPYA, maandalizi ya ujenzi yalikuwa yakienda vyema.
Vifaa vyote vya ujenzi vilikuwa eneo husika, saruji nyingi tulizipata viwandani na zingine tulizipata kwa kuangusha magari yaliyokuwa yakisafirisha kupeleka Kigoma.

Mazindiko ya kutosha yalikuwa yamewekwa kwenye eneo la ujenzi, wale Wachina tayari tulikuwa tumeshawaweka sawa kwa kazi iliyokuwa mbele yao.

Endelea

Siku ya kwanza ya ujenzi wa misingi ya majengo ya GAMBOSHI MPYA,tulipaswa kutoa kafara ya mnyama pamoja na binadamu.

Kulingana na maelekezo ya mkuu wetu, ng'ombe kumi weusi tii walipaswa kuchinjwa na damu zao zinyunyuziwe kwenye msingi.

Kwa upande wa kafara ya binadamu, alitakiwa mwanasiasa maarufu ndani ya bunge. Alitakiwa kukamatwa na kuletwa eneo hilo kisha achinjwe kama kuku, damu yake inyunyuziwe kwenye eneo la ujenzi.

Ndugu msomaji kuna muda wachawi huwa tunaua watu huku nafsi zikitusuta, hebu fikiria kitendo cha kumuua mwanao kisa uchawi yahitaji uvumilivu.

Hebu fikiria baba na mama walivyoamua kunitoa kafara THE BOMBOM kwa wachawi wenzao, wakati huo tayari walikuwa wameshawachukua dada zangu!! Hapa inahitaji uvumilivu wa hali ya juu, sheria za kichawi ndiyo hutufanya kutimiza hayo.

Kuna muda mwingine huwa tunaua huku tukiwa na furaha. Hebu fikiria mfano unapangiwa kumuua mbunge yeyote?

Ni ngumu kumuua mbunge ambaye anatetea wananchi, mara nyingi wabunge wasio na faida ndani ya bunge na nchi kwa ujumla ndiyo huwa tunawaua. Fikiri mbunge anayetetea ongezeko la tozo kwa wananchi huyo anafaa?

Fikiria mbunge ambaye anatetea rushwa za kipuuzi zinazofanywa na viongozi wengine, je huyu anafaida ndani ya jamii? Fikiria kiongozi anayeshiriki katika kuwaua wapinzani au wanachama wenzake ndani ya chama chake kwa maslahi ya tumbo lake, je, vitendo hivyo vina tija kwa wananchi?

Kikao kilipendekeza jina la mbunge wa kutolewa kafara, haraka usiku huo tuliamua kumfuata kwa ajili ya shughuli iliyokuwa mbele yake. Kundi la watu ishirini liliandaliwa tayari kwa kumfuata mbunge huyo, katika kundi hilo THE BOMBOM niliamua kuambatana nao.

Kwa kuwa kilikuwa ni kipindi cha vikao vya bunge mwanasiasa huyo alikuwa bungeni nyakati hizo, hivyo tusingepata tabu ya kwenda jimboni kwake. Tulikutana kwenye uwanja wa kambini kwetu usiku wa saa tano, tukajadili usafiri wa haraka ambao tungeutumia kwenda Dodoma.

Ndugu msomaji, wachawi huwa na usafiri wa aina mbalimbali kutegemea na umbali na malengo ya safari yao.

Kuna usafiri wa upepo huu huwa unabeba watu kulingana na ukubwa wa kigoda kilichopo. Hapa niseme kidogo, unapoona kimbunga chenye nguvu sana basi tambua huo ni usafiri mojawapo wa kichawi.

Siyo kila kimbunga ni usafiri wa kichawi, mara nyingi kimbunga cha kichawi hubeba uchafu mwingi na huwa kinatengeneza duara pana kikiwa kinasafiri. Katikati ya kimbunga huwa kuna kigoda, kigoda hicho ndicho hupakwa dawa ya upepo ili kiweze kusafiri.

Usafiri wa pili ni kutumia wanyama, mara nyingi matumizi ya wanyama hutofautiana kutoka eneo moja kwenda jingine. Wapo ambao hutumia fisi, mbwa, mbweha, paka nk usafiri wa aina hii hutumika ndani ya eneo la kawaida siyo mbali sana.

Usafiri mwingine ni vifaa vinavyoruka, vifaa hivyo ni pamoja na nyungo, fagio, ngozi za wanyama, vijiko, mwiko nk.

Usafiri huu pia huwa na sheria zake, hutofautiana kasi kutoka eneo moja kwenda jingine. Pia hutofautiana kiwango cha watu wa kuwabeba. Usafiri mwingine ni ule wa kukata, yaani unaandika ardhini sehemu unayotoka na kwenda.

Kisha unasimama kwenye duara lililoandikwa jina la mahali unapotoka, baada ya hapo unamwaga dawa kisha unachimba kwa jembe maalumu udongo wa eneo unakokwenda.

Kisha unarukia eneo hilo, ni kitendo cha kufumba na kufumbua unakuwa eneo ulilokuwa unakwenda. Usafiri huu unaweza kutumia sekunde moja kwenda Marekani au ulaya. Ni usafiri wa hali ya juu sana, ni wachawi wachache wanaomiliki kwani masharti yake ni magumu sana.

Tuliamua kwenda Dodoma kwa usafiri wa ngozi, huu ni usafiri wenye kubeba watu zaidi ya kumi kwa mpigo. Huwa na kasi kubwa kuliko usafiri wote wa aina hii. Tulichukua ngozi mbili tukapanda wote, kisha tukaanza safari ya kuelekea Dodoma. Tulienda kutua nje kidogo ya mji eneo la Makulu, pale kuna uwanja ambao hutumiwa na jamii kwenye michezo.

Ilikuwa ni saa sita usiku watu walikuwa wamelala na baadhi walikuwa barabarani wakiendelea na shughuli zao. Tukachukua umbo la mbwa kisha tukaanza safari ya kuelekea CBA. Eneo hilo ndipo walikuwa wakiishi waheshimiwa wabunge.

Tulikamata barabara iendayo mjini, tulipofika JK CONVENTION tuliachana na barabara ipitiayo DODOMA HOTEL na Shirika la POSTA. Tulinyoosha na barabara tukavuka BOT na HAZINA kwa mbele tukaingia kulia, tulivuka reli tukatokeza VETA kisha tukanyoosha.

Tulikwenda kutokeza chuo cha CBE, tulikamata barabara itokayo Dodoma kati kuelekea Meriwa na Kisasa. Tuliifuata barabara hiyo hadi bungeni, kwa kuwa safari yetu ilikuwa ni mbunge tuliachana na jengo hilo tukaingia kulia tukiachana na barabara hiyo.

Tulikamata barabara inayotenganisha DODOMA SEKONDARI na majumba ya watu kuelekea stendi ya Sabasaba. Kwa mbele yetu tuliingia kulia tukatokeza kwenye barabara kuu itokayo Kizota kuelekea stendi ya nanenane.

Tulichepuka kidogo tukatokeza kwenye mtaa uliojengwa nyumba za wabunge. Kulikuwa na nyumba nyingi sana zilizojengwa kwa ajili ya waheshimiwa hao.

Kila nyumba ilijengwa kisasa ikiwa na ua wake, ilijitosheleza kwa kila kitu ndani yake. Tulichukua dawa tukamwaga chini kujua ni nyumba ipi alipokuwa akikaa mbunge huyo, baada ya sekunde chache tulitambua hivyo tuliamua kuelekea kwenye nyumba hiyo.

Tulipofika mlangoni mwa ua wa nyumba hiyo, tulifanikiwa kuona walinzi waliokuwa wamevalia nguo za kijeshi. Yaani serikali ilikuwa ikitumia gharama kubwa kuwahudumia hata na wabunge wa hovyo kama huyu.

Askari hao walikuwa wameshika SMG mkononi mwao tayari kwa lolote mbele yao. Taa zilikuwa zikimlika eneo hilo mfano wa paradiso ndogo, mazingira yalikuwa rafiki kwa namna ya mandhari yake. Hakuna kapuku aliyeruhusiwa kukatisha eneo hilo, ni waheshimiwa pekee ndiyo walipaswa kuonekana.

Tulijibadili toka kwenye umbo la mbwa kwenda umbo la popo. Tuliweza kuingia kwenye nyumba hiyo iliyokuwa na bustani ndani yake, kwa kuwa tulikuwa kwenye umbo la popo wale askari hawakutugundua. Tulikwenda kwenye pembe ya nyumba hiyo tukazitumia kupenya ndani. Mle ndani tulikuta mbunge huyo akiwa na mchepuko, maana mke wake tulikuwa tukimtambua.

Tukachukua viboko vyetu maalumu, tukaanza kuwashikisha adabu yeye na mchepuko wake. Ndugu msomaji wakati huo tayari tulikuwa tumeshaondoa sauti ili kukata mawasiliano baina ya walinzi na mbunge.

Tulijitokeza kwenye maumbo ya kutisha ili mbunge huyo azidishe uoga zaidi, tuliendelea kumchapa viboko mwili mzima bila huruma. Kilikuwa ni kipigo cha mbwa koko tulichompatia mbunge huyo, kuna muda tulimkaba shingo yake kwa hasira kulipa kisasi kwa ushenzi aliokuwa kalifanyia Taifa letu.

Alitaika na kupiga kelele lakini haikumsaidia, alitakiwa kuchukuliwa kwa ajili ya kafara ya ujenzi wa GAMBOSHI MPYA. Wakati huo hatukuwa tumemfanyia dawa yeyote ya kupunguza maumivu, kwa hiyo kichapo tulichokuwa tukimpatia kilipenya ndani yake. Yalikuwa ni maumivu makubwa na ya kuumiza sana, hatukumhurumia tulimshikisha adabu kwelikweli wakati huo tukifurahia. Tulimkamata mchepuko wake tukamnyonga mbele yake kisha tukamlaza kitandani kwake akiwa hana uhai.

Tulifanya taratibu za kumchukua mbunge huyo kisha tukaondoka na mbunge wetu huyo. Tulikwenda eneo tulilokuwa tumeacha usafiri wetu, baada ya muda tulifika eneo husika kisha tukapanda na kuondoka.

Tulifika kambini muda wa saa nane za usiku, lakini kabla hatujatua tulifanikiwa kuona moto mkubwa chini. Tulibaini moto huo ulikuwa ni miale ya kichawi, kulikuwa na kundi kubwa la wachawi waliokuwa maeneo hayo. Lengo letu ilikuwa ni kutua eneo la ujenzi wa GAMBOSHI MPYA, ili tumchinje mbunge huyo lakini tukaenda kutua kambini tukiwa na kafara wetu.

Ndugu msomaji, unadhani nini kitatokea katika kisa hiki. Usikate tamaa, endelea kufuatilia kisa hiki cha kusisimua.

WABONYE?
THE BOMBOM

Ukitaka kupata mkasa huu sehemu ya 1-40 usisite kuwasiliana nasi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news