KULIPA KODI NI CHEO

NA LWAGA MWAMBANDE

NOVEMBA 15, mwaka huu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Uledi Abbas Mussa amesema kitendo cha kulipa kodi bila shuruti ni uzalendo wa hali ya juu na ndiyo maana mamlaka hiyo imekuwa ikionesha ufanisi katika makusanyo mara kwa mara.

Ameyasema hayo jijini Dar es Salaam katika kikao kazi baina ya watumishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na wahariri mbalimbali wa vyombo vya habari nchini.

Mwenyekiti huyo amesisitiza kuwa, kwa kutambua thamani ya mlipa kodi nchini hivi karibuni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan aliwaelekeza kwamba wajenge utamaduni wa kukusanya mapato ya Serikali bila kutumia mabavu na ndio maana wanawaelekeza maafisa wao kukusanya mapato bila kutumia mabavu.

"Tunataka walipa kodi wajisikie huru kabisa, tunataka tukae nao, wenye matatizo tukubaline jinsi gani malimbikizo ya kodi zao watayalipa bila kuathiri biashara zao.

Kwa mwezi Septemba TRA imekusanya takribani kiasi cha shilingi trilioni 2.3 ikilinganishwa na lengo la makusanyo ya shilingi trilioni 2. 2 makusanyo haya bado yanaonesha ufanisi wa asilimia 100. 5 ya lengo tulilojipa maana yake ni kwamba kuna dalili nzuri sana ya ukusanyaji wa mapato huko tunakoelekea na tumepata mafanikio haya tukiwa katika mazingira magumu sana Kimataifa.

"Sote tunajua kulikuwepo janga la Corona kabla halijapoa janga hivi sasa tuna vita kati ya Urusi na Ukraine. Mambo haya mawili yameathiri uchumi wa Dunia ikiwemo Tanzania, lakini pamoja na mazingira hayo magumu unalikuta Taifa letu linaendelea kwa kushirikiana na wananchi wake kukusanya mapato ya kuridhisha kwa ajili ya maendeleo,"anasema Mwenyekiti huyo.

Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema, ulipaji kodi bila shuruti umekuwa nyenzo muhimu ya kuwezesha makusanyo ambayo yamekuwa na tija kubwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo nchini, endelea;

1.Kodi pasipo shuruti, ni mkubwa uzalendo,
Fanya kazi pata noti, kulipa kodi ni mwendo,
Usumbufu haupati, yako mazuri matendo,
Mamlaka ya Mapato, Yazidi fanya vizuri.

2.Mamlaka ya Mapato, Yazidi fanya vizuri,
Ikikusanya mapato, taratibu bila shari,
Ulishatolewa wito, mabavu yawe sifuri,
Matokeo twayaona, kodi inaongezeka.

3.Matokeo twayaona, kodi inaongezeka,
Walipaji twawaona, ofisini wanafika,
Miamala twaiona, TEHAMA inahusika,
Makubwa maendeleo, na tena ya kujivunia.

4.Makubwa maendeleo, tena ya kujivunia,
Kulipa kodi ni cheo, ambacho twajivunia,
Kinaonesha upeo, kuipenda Tanzania,
Kuijenga nchi yetu, kwatutegemea sisi.

5.Kuijenga nchi yetu, kwatutegemea sisi,
Tukifanya kazi zetu, tukainuka kwa kasi,
Sehemu mapato yetu, tulipe kodi halisi,
Mapato yakiwa mengi, huduma zaimarika.

6.Mapato yakiwa mengi, huduma zaimarika,
Mahitaji yetu mengi, bajeti inagawika,
Hili jambo la msingi, huduma kote kufika,
Uzidi utamaduni, kupenda kulipa kodi.

7.Uzidi utamaduni, kupenda kulipa kodi,
Kuanzia mashuleni, tufundishe makusudi,
Wana wetu ukubwani, wafurahi lipa kodi,
Kodi ni heshima kwetu, na maendeleo yetu.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news