NHC, Absa Tanzania kumilikisha nyumba Watanzania, Waziri Dkt.Mabula afunguka

NA GODFREY NNKO

WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mheshimiwa Dkt.Angeline Mabula amesema,dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan ni kuona sekta binafsi nchini inashirikiana na Serikali katika kutekeleza miradi mbalimbali yenye manufaa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Dkt.Mabula ameyasema hayo Februari 17, 2023 jijini Dar es Salaam katika hafla ya utiaji saini Hati ya Maelewano (MoU) baina ya Benki ya Absa Tanzania na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa lengo la benki hiyo kuwezesha wateja wake kupata mkopo ulioboreshwa kwa ajili ya manunuzi ya nyumba.

"Dhamira ya Mheshimiwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ni kuona sekta binafsi zinashirikiana kwa pamoja na Serikali katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi, mpango huu unaokwenda kutekelezwa na benki kwa kushirikiana na NHC unakwenda kuwezesha wananchi kupata mikopo nafuu kusudi waweze kumudu kumiliki nyumba bora.

"Nizihimize benki nyingine na taasisi zingine za fedha na waendelezaji milki wengine kuiga mfano huu.Tusiachie taasisi peke yake tu za Serikali, lakini tunayo mabenki na makampuni yetu ambayo yanafanya ya uendelezaji milki, muone tunalo soko kubwa, lakini bado halijapata wadau wa kuliendeleza,"amefafanua Waziri Mheshimiwa Dkt.Mabula.
 
Abdi

Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Abdi Mohamed amesema, mkopo huo ulioboreshwa utamuwezesha mkopaji ambaye anataka nyumba kupata hadi asilimia 100 ya hitaji lake.

Amesema, awali walikuwa wanahudumia eneo dogo tu la Dar es Salaam kwa wenye uhitaji wa mikopo hiyo, lakini kwa sasa mikopo ya nyumba itatolewa popote benki hiyo inapotoa huduma nchini.

Pia amesema, jambo la kufurahisha ni kwamba, kiasi cha mkopo kimeongezeka zaidi hadi kufikia shilingi bilioni moja ambapo na muda wa marejesho nao umeongezwa.
 
Waziri tena

Katika hatua nyingine, Waziri Dkt.Mabula amewataka waendelezaji milki waone wanayo fursa ya kuzalisha nyumba za kutosha ili kuweza kukabiliana na changamoto iliyopo kwa sasa ya makazi nchini.

"Hatua hiyo itatuwezesha kukabiliana na changamoto tuliyo nayo, kadhalika matokeo ya awali ya Sensa ya Watu na Makazi imeonesha kiasi kidogo cha nyumba na zile zinazochukua muda mrefu, nitoe rai kwa wadau wote katika sekta ya uendelezaji milki kuona namna ya kutumia teknolojia ya kisasa ambayo inaweza kurahisisha kujenga nyumba nyingi kwa wakati mmoja.

"Wenzetu walioendelea wanajenga nyumba kiwandani, ukienda wewe huko unanua vifaa vyako, ukifika unapachika kwa hiyo waendelezaji milki tutumie fursa hii ya kuwa na teknolojia kwa sababu hitaji ni kubwa, kama tutategemea ujenzi wa matofali ambao tunaendelea nao ni wazi hatutaweza kufikia azima ya Taifa hili,"amefafanua Waziri Dkt.Mabula.

Wakati huo huo, Waziri Dkt.Mabula amesisitiza kuwa, wadau hao wanapaswa kuanzisha na kujenga nyumba za viwango, zinazotosheleza na zenye gharama nafuu.

"Kwa muda mfupi nimepitia mkataba walioingia NHC na benki, nimeona mtakuwa mnafadhili ununuzi wa nyumba za makazi kabla ya nyumba kukamilika, mpango huu utakuwa na manufaa kwa pande zote mbili na ni wazo jema na ni mpango mzuri.

"Ni fursa kwa Watanzania kuweza kuona jinsi gani watatumia fursa hii, hatua hii pia itasaidia kutatua changamoto za nyumba na itasaidia uuzaji wa mikopo ya nyumba kwa upande wa mabenki na kuwezesha upatikanaji wa nyumba bora kwa wakati na uwezo wa kumudu kujenga na kununua nyumba kwa upande wa wanunuzi wa nyumba,"amefafanu waziri Dkt.Mabula.

Aidha, amesema NHC watahakikisha upatikanaji wa fedha kwa haraka kwa ajili ya kukamilisha miradi ya nyumba kwa kasi zaidi na ndio maana wanaingia makubaliano hayo.

"Nichukue fursa hii kuwapongeza NHC kwa ubunifu na utekelezaji wa mipango yenu ambapo matokeo ya utekelezaji wake utakwenda kuwanufaisha Watanzania wote kadhalika hatua hii itawezesha upanuzi wa soko la nyumba ambalo kwa sasa linajumuisha Watanzania wanaoishi nje ya nchi kwa maana ya Diaspora na wafanyakazi wa mikataba katika maeneo mbalimbali walikoajiriwa na ninaamini kuna watu wengi pia ambao wangependa kununua nyumba kwa ajili yao na jamaa zao.

"Hata hivyo, wameshindwa kufikia malengo hayo kutokana na kutokuwa na fursa ya kupata mkopo wa nyumba na hivyo ninaamini kupitia fursa hii itasaidia Watanzania wengi walioko nje kuweza kumiliki nyumba, kwa sababu haya yanakwenda sambamba na jinsi ambavyo uwekezaji umekaribishwa nchini.

"Tunatambua sheria na miongozo ambayo tulikuwa nayo kwa upande mwingine haikuwa rafiki sana, lakini tunapokuwa na mabadiliko tunawawezesha kuwapa kumiliki nyumba.

"Tunao wengine hawajapata nyumba wako nje ya nchi ambao nao watapata nyumba. Katika hafla hii naomba tuwe mabalozi wa kutangaza fursa hii kwa ndugu zetu ambao wako Ughaibuni na pia kuwataarifu wanaweza kupata mkopo kutoka benki hii vile vile kiasi ambacho mteja anaweza kukopa kutoka Absa kimeongezeka kutoka shilingi milioni 500 mpaka shilingi bilioni moja.

"Fursa hiyo wameitoa, ni jukumu la kuchukua hiyo pesa, hatua hii pia itavutia wateja wengi kwa muda wa marejesho hadi kufikia miaka 25 na pia wamepanua wigo wa ukopaji wa nyumba umefikia hadi nje ya Mkoa wa Dar es Salaam, kwa hiyo na mimi ninawahimiza Watanzania wengi katika mikoa mbalimbali na wewe umesema una mabenki katika mikoa isiyopungua minane na una matawi 15, maana yake ni kwamba katika mikoa 26 ya Tanzania bado hatujawafikia Watanzania wengi.

"Tunaanza na hiyo mikoa minane na hayo matawi 15 tuliyonayo, lakini lengo liwe kufikia Watanzania wote katika mikoa yote. Niwahimize Watanzania kuchangamkia hiyo fursa, biashara inapokuja mapema wewe uwahi wakiona mnashindwa kuchangamkia wanaweza kubadilisha mawazo wakaleta product nyingine,"amefafanua na kusisitiza Waziri Dkt.Mabula.

Mheshimiwa Waziri Dkt.Mabula ameendelea kufafanua kuwa, "Watanzania niwaombe wachangamkie hii fursa waweze kumiliki nyumba bora kwa kuanzia zile zilizoko Morocco Square, ningependa kuwahikikishia dhamira ya Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt.Samia Suluhu Hassan itaendelea kufanya mageuzi ya kimuundo ili kuweka mazingira mazuri kwa Watanzania.

"Lengo la Mheshimiwa Rais ni kuwezesha Watanzania wawe na maisha bora kwa kupata nyumba zenye gharama nafuu. Kama tutapata wadau wanaokuja na bidhaa hizi inakupa nafuu ya kupata makazi bora na pia watu hawa wanamuunga mkono Mheshimiwa Rais, maisha bora ni pamoja na kuwa na nyumba bora.

"Nitoe rai pia kwa kampuni kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa kupanua huduma na vile vile Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini. Katika kuhakikisha maendeleo ya nchi yanakwenda kwa haraka na Wawekezaji wanapata usaidizi au huduma ambayo wanahitaji kuipata,"amefafanua Waziri Dkt.Mabula.

NHC

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Nehemia Mchechu amesema, jambo ambalo amelibaini kulingana na ripoti ya benki kuhusu utekelezaji wa utaratibu huo wa kutoa mikopo ya nyumba inadhirisha wazi kuwa, wamelisoma soko, kusoma mazingira na kuona ni aina gani ya bidhaa wailete kwa manufaa ya Watanzania.

"Kwa hii structure mlioifanya tunatembea kipaumbele ukiwa covered na bima, unakwenda asilimia 100 kama ni nyumba ya milioni 100 utaratibu unakutaka ulipe asilimia 10, maana yake milioni 10. Watanzania wengi tuna mishahara yetu, lakini ina bajeti hakuna mtu mwenye serving ya milioni 10, unaweza ukasema una nyumba ya milioni 300 huna serving ya milioni 30, lakini maana yake kama ulikuwa unachukua nyumba ya milioni 300 ile milioni 30 unakwenda insurance na wanafanya kama unavyofanya kwenye gari.

"Una lipa haizidi hata 500,000 na CRI haizidi hata laki tano kwa sababu haizidi 0.5 yaani one percent. Sasa badala wewe ya kulipa milioni 30, unalipa 500,000 unapata asilimia 100 ya mkopo.

"Ndio maana nimesema hawa jamaa tutatembea nao, tutapiga nao kelele halafu sisi tutakuwa wehu wa maendeleo. Hawa wanakwambia kama bondi peleka wanakupa.

"Kwa sababu sisi tuna watu tumewauzia viwanja tutakwenda kwa wale watu kuwajengea kwa sababu wanaruhusiwa kupata home construction loan, tutawapa desgin zetu tulizonazo ili waweze kununua kwa urahisi kupata mikopo kwa urahisi na wajengewe.

"Sasa wanaosema kwamba tuna viwanja vyetu tuwajengee, hii ndio maana yake ingawa hatuwezi kumjengea kila mtu kwenye kiwanja alipo kwa sababu wakati mwingine kiwanja chako kiko sehemu ngumu na uko sehemu mbali, lakini kwenye maeneo ambayo sisi tunayauza ni rahisi sana sisi kwenda kufanya kazi.

"Diaspora home loan, watu walikuwa wanalalamika kwa sababu jamaa katembea miaka mitatu, watu wa benki wanamwambia mshahara wako unapitia huko Bongo, anasema sasa mimi ninafanya kazi Google mshahara wangu unapitaje Bongo, lakini hapa una benki inatambua kwamba mshahara wako utapitia huko huko, Diaspora wao wamejitosa huko huko, lakini unakuja kusaidia, kwa hiyo Abdu na timu yote ya Absa, hapa lazima tukimbie, tutembee na pia tushirikiane.

"Kama NHC tumewapata wabia kama hawa, hawa ni wadau watatusaidi kuchalenges partinership tuliyonayo, tuna partinership ya mabenki 20, lakini niseme nafikiri katika products zote 20, mabenki yote tuliyonayo benki iliyowasoma Watanzania na kuwaelewa ni hii Absa, nawapongezeni katika hili,"amefafanua Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Nehemia Mchechu.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news