REA yampa tuzo Mkandarasi STEG International kwa utendaji bora

NA VERONICA SIMBA-REA

WAKALA wa Nishati Vijijini (REA) umetunuku tuzo ya Utendaji Bora kwa Kampuni ya Ukandarasi ya STEG International Services ambayo imetekeleza Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili kwa wakati na ufanisi, ikishika nafasi ya kwanza kati ya Kampuni 21 za Ukandarasi zinazotekeleza Mradi huo katika maeneo mbalimbali nchini.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy (wa pili – kushoto) na Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi kutoka REA, Mhandisi Jones Olotu (wa kwanza-kulia), wakikabidhi Tuzo ya Utendaji Bora kwa Makamu Mkuu wa Kampuni ya Ukandarasi ya STEG International Services, Rached Daghfous (wa pili-kulia) aliyeambatana na Mratibu Mradi, Zouheir Khlifa jijini Dar es Salaam, Februari 15, 2023. Kampuni hiyo imetekeleza kwa wakati na ubora Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili katika mikoa ya Simiyu na Morogoro.

Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy amemkabidhi Tuzo hiyo Makamu Mkuu wa Kampuni hiyo, Rached Daghfous aliyeambatana na Mratibu Mradi, Zouheir Khlifa jijini Dar es Salaam, Februari 15, 2023.

Kabla ya kukabidhi tuzo hiyo, Mhandisi Saidy ameielezea Kampuni hiyo ya Ukandarasi kama mfano wa kuigwa kutokana na utendaji wake mzuri.

Amesema, REA kwa niaba ya Wizara ya Nishati na Serikali kwa ujumla wanapongeza kazi nzuri iliyofanywa na kampuni hiyo na wameona ni busara watambue utendaji wake mzuri kwa kuwapatia tuzo ili iwe kumbukumbu na motisha kwao na wakandarasi wengine, ili waige mfano wao.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy (kushoto) akikabidhi Tuzo ya Utendaji Bora kwa Makamu Mkuu wa Kampuni ya Ukandarasi ya STEG International Services, Rached Daghfous, Februari 15, 2023 jijini Dar es Salaam. Kampuni hiyo imetekeleza kwa wakati na ubora Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili katika mikoa ya Simiyu na Morogoro.

“Tunasherehekea kampuni pekee ya ukandarasi ambayo imeweza kupeleka umeme kwa wakati katika vijiji vyote vya eneo ililopangiwa kimkataba,” amebainisha Mhandisi Saidy.

Kwa upande wake, Daghfous ameishukuru Serikali ya Tanzania kupitia REA kwa kutambua na kuthamini viwango bora vya utendaji kazi vilivyodhihirishwa na kampuni yake na kuahidi kuwa kamwe hawatarudi nyuma bali wataendelea kuchapa kazi kwa umakini, kwa wakati na kwa viwango vya hali ya juu.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy (kushoto) akikabidhi Tuzo ya Utendaji Bora kwa Mratibu Mradi wa Kampuni ya Ukandarasi ya STEG International Services, Zouheir Khlifa jijini Dar es Salaam, Februari 15, 2023. Kampuni hiyo imetekeleza kwa wakati na ubora Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili katika mikoa ya Simiyu na Morogoro.

Naye Mratibu Mradi wa kampuni hiyo, Zouheir Khlifa amekiri kuwa mfumo unaotumiwa na Tanzania katika kupeleka umeme vijijini ni wa kipekee kwa sehemu kubwa ya Bara la Afrika na akaongeza kuwa nchi nyingine za Bara hilo hazina budi kujifunza kutoka kwake.

“Nikiri kuwa nimefanya kazi katika nchi mbalimbali Afrika lakini sijawahi kuona mfumo bora kama huu unaotumika Tanzania ambapo kuna Taasisi maalumu inayoshughulikia kazi ya kupeleka umeme vijijini na Serikali inatenga fungu maalumu kwa kazi hiyo,” amepongeza.

Mkandarasi STEG International Services anatekeleza miradi ya umeme vijijini katika Mikoa ya Morogoro na Simiyu.

Wakandarasi wengine wanaotekeleza Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili ni Urban and Rural Engineering Services Ltd, Sagemcom Energy and Technology Ltd, OK Electrical & Electronics Ltd, CRJE – CTCE Consortium, JV Pomy Engineering & Qwihaya na Electrical Transmission and Distribution Co. Ltd (ETDCO).
Tuzo ya Utendaji Bora iliyotolewa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa Kampuni ya Ukandarasi ya STEG International Services, Februari 15, 2023 jijini Dar es Salaam. Kampuni hiyo imetekeleza kwa wakati na ubora Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili katika mikoa ya Simiyu na Morogoro.

Wengine ni State Grid Electrical and Technical Works Ltd, Nakuroi Investment Company Ltd, JV White City and Guangdong Ltd, GIZA Cable Industries Ltd, HNXJDL JV, Namis Corporate Ltd, Tontan Project Technology & Group Six International Ltd, SUMA JKT Construction Co. Ltd na Sengerema Engineering Services Ltd.

Pia ni pamoja na Central Electricals International Ltd, Derm Electrics Ltd, Ceylex Engineering (PVT) Ltd, JV SILO Power and Guangzhou Yidian Equipmeny Instal, China Railway Construction & Electrification Bureau Group pamoja na Tontan Project Technology & Group Six International Ltd.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news