AUMIE SEMA KWELI, ACHUKIE SEMA KWELI

NA LWAGA MWAMBANDE

LEO Machi 12,2023 katika mahubiri yake huko Masasi mkoani Mtwara, Askofu wa Kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la Mashariki, Lawi A.Mwankunga amesema, kusema ukweli kuna faida nyingi katika maisha ya binadamu hususani anayemtegemea Mungu katika mambo na mipango yake yote.
"Kanisa la Mungu, mtu akikuambia ukweli, ukweli unauma, lakini unaponya. Hata kama utaona yamkini amekudhalilisha, lakini ukweli ubaki kuwa ukweli.

"Wala palipo paovu usipake rangi. Na wote tuna macho, ukipaka rangi ambayo siyo itaonekana tu unapendezesha kitu kichafu, katika jina la Yesu kichafu kibaki kuwa kichafu na kizuri kibaki kuwa kizuri, ila kichafu ili kiwe kisafi ni kwa njia ya toba. Kwa hiyo ukiambiwa ukweli, nikiambiwa ukweli, usifanye moyo wako kuwa mgumu, bali tuwe na moyo wa toba,"amefafanua Askofu huyo.

Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwmabande anasema kuwa, toba haina kanuni maalumu bali kanuni maalumu ni kile kitokacho ndani ya moyo,kama unahitaji kuomba toba basi huna budi maombi yako yatoke kwenye moyo na umaanishe kuacha dhambi, uasi, makosa au uovu.

Rejea, Biblia Takatifu kitabu cha Matendo 2:37-38,Matendo 26:20)...Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine,tutendeje, ndugu zetu? Petro akawaambia,tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu...Endelea;


1. Ukweli ubaki kweli, uchafu sio ukweli,
Ukiambiwa ukweli, nikiambiwa ukweli,
Hata uwe ni dhalili, ukweli ubaki kweli,
Kichafu kiwe kichafu, kitakasike kwa toba.

2. Aumie sema kweli, achukie sema kweli,
Wala siyo ukatili, unaposema ukweli,
Hii ni njema kauli, kweli ibakie kweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

3. Pale palipo uovu, usipindishe ukweli,
Sema huo ni uovu, hiyo hasa ndiyo kweli,
Sipake rangi uovu, tutauona ukweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

4. Kupaka rangi uovu, huenendi na ukweli,
Tutauona uovu, kwa hali hata kauli,
Mbichi si sawa na mbivu, baki wasema ukweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

5. Tambua tunayo macho, rangi chafu si halali
Kwa kile kitokeacho, wewe onyesha ukweli
Usipake rangi hicho, unapotoa ukweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

6. Ukiambiwa ukweli, huo ujumbe halali,
Ukubali ni ukweli, ukatae ni ukweli,
Uongo siyo ukweli, ukweli ndiyo ukweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

7. Upake rangi uchafu, haugeuki ukweli
Hata watu wakusifu, uongo siyo ukweli
Kupendezesha kichafu, hakukifanyi ni kweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

8. Kutaka utakatifu, ukumbatie ukweli,
Tuukemee uchafu, kweli ibaki ukweli,
Anika wote uchafu, hapo watangaza kweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

9. Kweli kakudhalilisha, kukuambia ukweli,
Lengo ni kukusafisha, na Mungu usiwe mbali,
Pazuri tajifikisha, ukiukiri ukweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

10. Kanisa hili tambua, ukweli uwe ukweli,
Ule unaoujua, useme ndiyo ukweli,
Unauma tunajua, unabakia ukweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

11. Kupendezesha kichafu, hudhalilisha ukweli,
Kwa kanisa udhaifu, Mungu anabaki mbali,
Uchafu tusiusifu, ututawale ukweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

12. Kama rangi unapaka, ukweli wabaki kweli,
Popote hautafika, usiposema ukweli,
Taka itabaki taka, huo hasa ni ukweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

13. Dhalilika kwa ukweli, ni gharama za ukweli,
Adhirika kwa ukweli, ni thamani ya ukweli,
Takufikisha mahali, ukidhihiri ukweli,
Kichafu sema kichafu, kitakasike kwa toba.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news