Waziri Dkt.Mwigulu: Mwelekeo wetu kiuchumi ni mzuri duniani

NA DIRAMAKINI

WAZIRI wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Dkt.Mwigulu Nchemba amesema, mfumuko wa bei nchini umeendelea kuwa ndani ya lengo la wigo wa kuwa chini ya asilimia tano.

Ameyasema hayo Juni 15, 2023 bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha taarifa ya Hali ya Uchumi wa Kitaifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa Mwaka 2023/2024.
 
Ameeleza kuwa, Mpango umeandaliwa kwa kuzingatia: Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025; Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/22 - 2025/26; Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020;

Pia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2023/24; na Sera na Mikakati mbalimbali ya kisekta, kikanda na kimataifa zikiwemo Dira ya Maendeleo ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) 2050, Dira ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) 2050, Agenda 2063 ya Maendeleo ya Afrika na Malengo ya Maendeleo Endelevu 2030.

Amesema katika utekelezaji wa Mpango wa mwaka 2023/24, msisitizo mkubwa utawekwa katika sekta za uzalishaji na zinazozalisha ajira zinazowagusa wananchi wengi ambazo ni kilimo, mifugo, na uvuvi.

Aidha, Mpango huo unalenga kukamilisha miradi mingi ambayo ilianza katika utekelezaji wa mpango wa tatu wa maendeleo wa miaka mitano(2021/22-2025/26), ambao ni wa mwisho katika utekelezaji wa Dira 2025.

Vile vile, utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2023/24 unatarajia kuleta matokeo chanya ikiwemo kuimarika kwa ukuaji wa Pato la Taifa; kuimarika kwa miundombinu ya huduma za kiuchumi na kijamii hususan afya, elimu, maji na umeme; kudhibitiwa kwa kasi ya mfumuko wa bei.

Pia kuimarika kwa mazingira ya uwekezaji na biashara, kuvutia ushiriki wa sekta binafsi; na kuimarika kwa maisha na ustawi wa jamii.

“Mwaka 2022, mfumuko wa bei ulifikia wastani wa asilimia 4.3 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 3.7 mwaka 2021, aidha mfumuko wa bei hadi mwezi Mei, 2023 umebaki kama ilivyokuwa katika kipindi hicho hicho mwaka 2022 ikiwa ni wastani wa asilimia 4.0.

“Hali hii imesababishwa na kuongezeka kwa uzalishaji na usambazaji wa bidhaa na huduma na kuongezeka kwa upatikanaji wa mazao ya chakula katika baadhi ya maeneo nchini na nchi jirani kulikosababishwa na upatikanaji wa mvua katika maeneo yanayotegemea mvua,"amesema.

Fedha za kigeni

Mheshimiwa Dkt.Nchemba amesema kwamba, hadi kufikia April 2023, akiba ya fedha za kigeni ilikuwa dola za Marekani bilioni 4.88 ambayo inatosheleza uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi kwa kipindi cha takribani miezi 4.4.

“Akiba ya fedha za kigeni imeendelea kuwa ya kuridhisha kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi, hadi kufikia Aprili 2023, akiba ya fedha za kigeni ilikuwa dola za Marekani bilioni 4.88 ambayo inatosheleza uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi kwa kipindi cha takribani miezi 4.4.

“Mahitaji ya nchi kisheria ni kuwa na kiasi cha fedha za kigeni kinachotosheleza uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi kwa muda usiopungua miezi 4.0,”amesema.

Pato la Taifa

Kwa upande wa uwiano wa uwekezaji na pato la Taifa, Mheshimiwa Waziri Dkt.Nchemba amesema kuwa, umeongezeka kwa asilimia 0.2 kwa kipindi cha mwaka 2022 ukilinganisha na mwaka 2021 ambapo ulikuwa asilimia 41.6 wakati mwaka 2022 ilifikia asilimia 41.8.

Waziri amesema, mwaka 2017 ilikuwa asilimia 30.6, 2018 ikawa 32.9 na kuongeza hadi asilimia 33.1 2019 kabla ya kufikia asilimia 36.9.

Aidha, kuhusu ukuaji halisi wa pato la Taifa kwa miaka hiyo amesema ilipanda na kushuka huku sababu zikitajwa ni virusi vya Uviko-19 na vita vya Ukraine na Urusi ambapo mwaka 2017 ilikuwa asilimia 6.8, 2018 ikawa 6.9, 2019 ilikuwa asilimia 7.0 kabla ya kushuka mwaka 2020 ilipokuwa 4.8, kisha 2021 ikafikia asilimia 4.9 na kushuka tena mwaka 2022 kwa asilimia 4.7.

“Uwiano wa akiba kwenye benki na pato la Taifa kwa miaka hiyo pia kumekuwa na mabadiliko ya kupanda na kushuka kutoka mwaka 2017 ilipokuwa asilimia 19.2 na mwaka 2022 ilikuwa 20.9,”amesema.

Amebainisha,akiba ya fedha za kigeni kwa 2021 ilikuwa asilimia 6.2 wakati 2022 ikawa asilimia 4.7, mwaka 2017
ni asilimia 6.1, mwaka 2018 ni asilimia 4.6, 2019 asilimia 5.9 na 2020 asilimia 5.3.

Pia, Mheshimiwa Waziri Dkt.Nchema amesema kuwa katika mwaka 2022 thamani halisi ya pato la Taifa ilifikia shilingi trilioni 141.9 ikilinganishwa na shilingi trilioni 135.47 ya mwaka 2021 ambayo ndiyo iliyofanya wastani wa ukuaji kufikia asilimia 4.7.

Duniani

Pia, amesema kwamba taarifa ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) ya Aprili 2023 inaonesha kuwa, kasi ya ukuaji wa uchumi wa dunia imepungua kutoka asilimia 6.3 mwaka 2021 hadi asilimi 3.4 mwaka 2022.

“Upungufu huo unatokana na sababu mbalimbali ikiwemo kasi ndogo ya ukuaji wa uchumi wa China na India, madhara ya janga la UVIKO-19, vita kati ya Urusi na Ukraine, na sera za kupunguza ukwasi katika chumi za Ulaya ili kukabiliana na mfumuko wa bei.

“Aidha, uchumi wa dunia unatarajiwa kupungua zaidi na kufikia ukuaji wa asilimia 2.8 mwaka 2023 kutokana na kuendelea kwa vita kati ya Urusi na Ukraine, mabadiliko ya tabia nchi na sera za Marekani kuongeza riba.

“Ukuaji wa uchumi kwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara ulipungua kufikia wastani wa asilimia 3.9 mwaka 2022 ikilinganishwa na asilimia 4.8 mwaka 2021, aidha ukuaji wa Pato la nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ulikua kwa wastani wa asilimia 4.1 ikilinganishwa na ukuaji wa wastani wa asilimia 5.3 mwaka 2021.

“Vilevile, wastani wa ukuaji wa uchumi kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ulikuwa ni asilimia 5.3 mwaka 2022 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 6.3 mwaka 2021, upungufu huo ulitokana na madhara ya vita kati ya Urusi na Ukraine uliyosababisha mfumuko wa bei za nishati ya mafuta na vyakula,”amefafanua.

Uchumi wetu

Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Waziri Dkt.Mwigulu amesema,Tanzania bado imeendelea kuwa nchi ya uchumi wa kati ngazi ya chini.

“Kutokana na hatua madhubuti zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali thamani ya pato ghafi la Taifa linatarajiwa kufikia dola za Marekani bilioni 85.42 mwaka 2023/24, mwaka 2022, pato ghafi la Taifa (kwa bei za mwaka husika) lilikuwa shilingi trilioni 170.3 (sawa na Dola za Marekeni bilioni 77.6) ikilinganishwa na shilingi trilioni 156.4 mwaka 2021 (sawa na Dola za Marekani bilioni 69.94).

“Aidha, kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022, idadi ya watu Tanzania Bara ilikuwa 59,851,347 ikilinganishwa na makadirio ya idadi ya watu 57,724,380 mwaka 2021.

"Hivyo, Pato la Taifa kwa Mtu (GDP Per Capital) kwa mwaka 2022 lilikuwa shilingi 2,844,641 ikilinganishwa na shilingi 2,708,999 mwaka 2021, sawa na ongezeko la asilimia 5.0.

"Kiasi hicho ni sawa na dola za Marekani 1,229.1 mwaka 2022 kwa mtu kwa mwaka ikilinganishwa na dola za Marekani 1,173.3 mwaka 2021, hali hii inaendelea kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati ngazi ya chini,”amesema.

Shabaha

Mheshimiwa Waziri Dkt.Mwigulu amefafanua kuwa,Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2023/24 ni wa tatu katika utekelezaji wa Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2021/22 –2025/26) wenye dhima ya kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Kuhusu Malengo na Shabaha za Uchumi Jumla kwa Mwaka 2023/24 amesema, malengo na shabaha za ukuaji wa uchumi katika kipindi cha mwaka 2023/24, ni Ukuaji wa Pato Halisi la Taifa kufikia asilimia 5.2 mwaka 2023 kutoka ukuaji wa asilimia 4.7 mwaka 2022.

Aidha, mfumuko wa bei kubaki kwenye wigo wa tarakimu moja ya wastani wa asilimia 3.0 hadi asilimia 7.0 katika kipindi cha muda wa kati; Mapato ya ndani kufikia asilimia 14.9 ya Pato la Taifa mwaka 2023/24 kutoka matarajio ya asilimia 14.4 mwaka 2022/23

Pia Mapato ya kodi kufikia asilimia 12.0 ya Pato la Taifa mwaka 2023/24 kutoka matarajio ya asilimia 11.5 mwaka 2022/23; Nakisi ya bajeti (ikijumuisha misaada) kuwa chini ya asilimia 3.0 ya Pato la Taifa mwaka 2023/24; na Kuwa na akiba ya fedha za kigeni kwa kiwango cha kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje kwa kipindi kisichopungua miezi minne (4).

Kuhusu misingi itakayozingatiwa katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2023/24 ameitaja ni kuongezeka kwa ushiriki wa sekta binafsi kwenye shughuli za uwekezaji na biashara, kuendelea kuhimili athari za majanga ya asili na yasiyo ya asili.

Mengine ni kuendelea kuhimili athari zitokanazo na kushuka kwa uchumi wa dunia na kuongezeka kwa bei za bidhaa na huduma katika soko la dunia; kuendelea kuimarika kwa utoshelevu wa chakula nchini; Uwepo wa amani, usalama, umoja na utulivu wa ndani na nchi jirani na Kuendelea kuimarika kwa viashiria vya ustawi wa jamii.

Akizungumzia miradi ya kipaumbele kwa Mwaka 2023/24, Dkt.Mwigulu amesema katika mwaka 2023/24, Serikali itaendelea na utekelezaji wa miradi ya kielelezo. Miradi hiyo inajumuisha: Ujenzi wa Reli ya Kati kwa Kiwango cha Kimataifa (Standard Gauge Railway - SGR)

Pia Mradi wa Kufua Umeme wa Maji wa Julius Nyerere – MW 2,115; Kuboresha Shirika la Ndege Tanzania (ATCL); Kuchakata na kusindika Gesi Asilia kuwa Kimiminika (LNG) – Lindi; Kufua Umeme wa Maji wa Ruhudji (MW 358) na Rumakali (MW 222) – Njombe, Daraja la JPM - Kigongo – Busisi (Mwanza).

Aidha ujenzi wa barabara na Madaraja Makubwa; kuendeleza Kanda Maalumu za Kiuchumi ikiwemo Eneo Maalumu la Uwekezaji Bagamoyo na Programu ya kuendeleza ujuzi adimu.

"Kwa mwaka 2023/24 Serikali itatekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kwa kuzingatia
maeneo matano (5) ya kipaumbele ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano, 2021/22 – 2025/26 ni kuchochea uchumi shindani na shirikishi

"Katika eneo hili nguvu kubwa itaelekezwa kwenye miradi inayolenga kuboresha miundombinu, kuimarisha mifumo ya kitaasisi pamoja na miradi inayolenga kuleta mapinduzi ya TEHAMA. Utekelezaji wa miradi hiyo utaimarisha mazingira wezeshi ya uwekezaji na kuongeza utulivu wa kiuchumi.

"Miradi hiyo ni pamoja na Barabara: miradi itakayotekelezwa ni ile inayolenga
kufungua fursa za kiuchumi, za kuunganisha Tanzania na nchi jirani pamoja na za kupunguza msongamano ikiwemo: Barabara ya Kidatu – Ifakara – Lupilo - Malinyi – Londo -Lumecha/Songea (km 499)

"Barabara ya Ifakara - Kihansi - Mlimba -Madeke – Kibena (km 220); na Barabara ya Makutano
– Natta – Mugumu/Loliondo – Mto wa Mbu (km 235); Handeni – Kibaya – Singida (Km460).Madaraja Makubwa: kuanza ukarabati wa daraja la Kirumi (Mara); kuendelea na ujenzi wa barabara unganishi za Daraja la Sibiti (Singida).

"Na kuanza ujenzi wa Madaraja ya Chakwale (Morogoro), Nguyami (Morogoro) na Mbambe (Pwani). Usafiri wa Majini ni pamoja na Ujenzi na Ukarabati wa Meli katika Maziwa Makuu ikijumuisha kukamilisha ujenzi wa meli mpya ya MV. Mwanza Hapa Kazi Tu, "amesema Dk.Mwigulu.

Ameongeza pia kukamilisha ukarabati wa meli za MV Umoja na MT. Sangara; kuanza ujenzi wa meli mpya (Wagon ferry) katika Ziwa Victoria na meli mpya (Barge/Cargo ship) ya kubeba shehena ya mizigo katika Ziwa Tanganyika,

Bandari: Bandari ya Dar es Salaam, kuendelea uchimbaji wa kina na upanuzi wa lango la kuingilia na kugeuzia meli na uboreshaji wa Gati Na. 8 – 11 na kuendelea na upembuzi yakinifu wa ujenzi wa gati na. 12 -15; kuendelea na uboreshaji wa Bandari ya Tanga na maandalizi ya ujenzi wa miundombinu ya gati la mafuta ghafi kutoka Hoima (Uganda) hadi Chongoleani (Tanga).

Pia bandari ya Mtwara, kuendelea na maboresho ya maeneo ya kuhudumia shehena za mizigo; Bandari ya Bagamoyo, kuanza maandalizi ya utekelezaji wa bandari; kuendelea na uboreshaji wa Bandari za Bukoba, Kemondo Bay na Mwanza North katika Ziwa Victoria.

Aidha kuendelea na ujenzi wa Access Road, Cargo Shed, Passenger Wharf and Lounge) pamoja na kuendelea na ujenzi wa Passenger Lounge na ukuta wa mizigo wa Lighter Quay katika Bandari ya Kibirizi na gati la Bandari ya Ujiji katika Ziwa Tanganyika.

Maeneo mengine ni Usafiri wa Anga kwa kuendelea na ujenzi na ukarabati
wa viwanja vya ndege vya Msalato, Mwanza, Mtwara, Kigoma, Sumbawanga, Shinyanga, Songwe, Mpanda, Tabora, Bukoba, Geita, Iringa, Ruvuma (Songea), Simiyu, Lake Manyara, Tanga, Moshi, Lindi na Mara (Musoma), Dodoma, Manyara na Arusha.

Kwa upande wa nishati kuendelea na utekelezaji wa miradi ya kufua, kusafirisha na kusambaza umeme (nishati) ikiwemo: Kufua Umeme wa Maji Kikonge (MW 300); Kufua Umeme wa Maji Malagarasi (MW 49.5).Pia uimarishaji wa Gridi ya Taifa (National Grid Stabilization).

Pia njia ya Kusafirisha Umeme wa Msongo wa kV 400 Rufiji – Chalinze – Dodoma na Chalinze – Kinyerezi; na Njia ya Kusafirisha Umeme wa Msongo wa kV 400 – North – West Grid Extension (Iringa – Mbeya – Sumbawanga – Mpanda – Kigoma – Nyakanazi).

Dk.Mwigulu ameendelea kueleza miradi mingine ya kipaumbele ni Mapinduzi ya TEHAMA: Kuendelea na ujenzi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano; kuendelea na utekelezaji wa miradi ya Anwani za Makazi na Tanzania ya Kidijitali.

Pia kuendeleza Ubunifu na Utengenezaji wa Vifaa vya TEHAMA; na ujenzi wa Kituo Kikuu na Vituo vidogo vya Kuendeleza Ubunifu katika TEHAMA ,kuimarisha uwezo wa uzalishaji viwandani na huduma.

"Miradi itajielekeza katika kukuza sekta za uzalishaji ikiwemo kilimo, mifugo na uvuvi. Miradi hiyo ni pamoja na: programu ya kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili; mradi wa kuimarisha miundombinu ya masoko ya mifugo na mazao yake.

"Kuimarisha miundombinu ya umwagiliaji kwa kujenga skimu mpya 25 na kukarabati skimu 30 zenye jumla ya hekta 95,005 katika mikoa mbalimbali na kuimarisha huduma za ugani. 
 
"Aidha, msukumo wa pekee utawekwa katika kuboresha Viwanda Vidogo – SIDO na Kiwanda cha Mashine na Vipuri KMTC; kuendeleza maeneo maalum ya kiuchumi (SEZ) na kongani za viwanda,"amesema Mheshimiwa Waziri Dkt.Mwigulu.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news