Mradi wa 7/11 mbioni kuendelea, Waziri Silaa aipa kongole NHC

NA GODFREY NNKO

WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mheshimiwa Jerry Silaa amesema, mwezi ujao wanatarajia Mradi wa 7/11 wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) ambao ulikwama awali kutokana na changamoto mbalimbali utaanza.
Mheshimiwa Silaa ameyasema hayo leo Septemba 11, 2023 baada ya kufanya ziara katika miradi ya NHC ambayo inajumuisha mradi huo, Samia Housing Scheme uliopo Tanganyika Packers na Morocco Square jijini Dar es Salaam.

“La, pili Mradi wa 7/11 ulokwama tumekubaliana ikifika Oktoba uanze, kwa sababu kuna fedha pale ambayo ni ya mkopo imelala.

“Lakini, vile vile kuna wananchi wengi wangependa kupata nyumba, na ni eneo nzuri,na kazi yetu, ninyi na sisi kama Shirika la Nyumba ni kuhakikisha wananchi wanapata nyumba.”

Waziri Silaa amesema, kuendelea kusimama kwa muda mrefu kwa mradi huo kunachangia gharama nyingi hususani mkopo kuongezeka riba.

“Umesimama muda mrefu na unaposimama maana yake mkopo unaongezeka riba, gharama zinaongezeka na mradi umeshaanza, mahitaji ya nyumba yapo, kwa hiyo kuna mazungumzo yanafanyika baina ya Mkandarasi na shirika.

“Basi wapambane kufikia mwezi Oktoba jambo lifike mwisho, tuone mitambo inazunguka, mitambo ikizunguka maana yake kuna ajira za mafundi, wahandisi, mama ntilie zitapatikana, na nyumba zikikamilika wananchi watapata makazi ya kuishi.”

Wakati huo huo,Mheshimiwa Silaa, licha ya kuridhishwa na maendeleo ya Mradi wa Morocco Square ameeleza kuwa, umefikia wakati sasa kwa NHC kuongeza uwekezaji wa miradi ya nyumba ili watanzania wapate nyumba za kupanga na kununua nchini.

“Upo mradi huu wa Morocco Square ambao ni kati ya miradi ya re-development. miradi ya kuchukua nyumba za zamani zilikuwa zinakaliwa na watu wachache ili kujenga miradi mikubwa ya kisasa.

“Tumeona Mradi wa Samia Scheme (Samia Housing Scheme) pale Kawe, ujenzi wa nyumba ambao Watanzania wanaweza kununua moja kwa moja, ambapo mpaka tunavyozungumza umeshauza kwa asilimia kubwa.

“Nilipongeze Shirika la Nyumba (Shirika la Nyumba la Taifa-NHC), kwa kufanya kazi nzuri,waendelee kufanya kazi kwa moyo katika kuhakikisha Sekta ya Nyumba inaboreka.

“La tatu, ni kuhakikisha Mradi wa Morocco Square unakamilika, lakini mengine mawili madogo, moja ni kuhakikisha Samia Scheme (Samia Housing Scheme) inakwenda mikoa mingine hasa kwenye majiji makubwa, pale Dodoma kuna mahitaji makubwa ya nyumba, Mwanza, Mbeya, Arusha.

“Majiji makubwa ambayo yana idadi kubwa ya watu, ambayo watu wana mwingiliano mkubwa ambayo sekta ya nyumba inakuwa kwa kiasi kikubwa kuhakikisha mnaenda huko ili kutengeneza sura, kwamba Samia Scheme (Samia Housing Scheme) si ya Dar es Salaam peke yake.

“Lakini, la pili ninyi mnafahamu pressure ya nyumba za Shirika la Nyumba hata waziri aliyeteuliwa ana pressure ya watu ambao wanahitaji nyumba, hizi re-development ebu muhakikishe mnatengeneza mpango wa kuwa maeneo yote.

“Kwa sababu kuna ile Upanga, kuna City Centre, wale ambao walikuwa wanajenga miaka ya 70 na 60 zile nyumba za ghorofa tatu walikuwa wanajenga kwa idadi ya watu milioni 9 wakati wa Uhuru.

“Leo tupo milioni 61 tunategemea kuona re-development inafanyika katika maeneo ambayo si tabu sana kupata nyumba.”

“Lakini,mna mpango mzuri wa ubia, muangalie mlipofikia, muupime muangalie kuwashawishi watu wenye uwezo wa kifedha, kwa sababu hatuwezi kuendelea wenyewe ndani ya Taifa, kwenye sekta ya nyumba kwa kutegemea mitaji ya ndani.

“Au kwa kutegemea mikopo ya mabenki, wapo watu wenye mitaji, hii inaenda pamoja na Sera ya Ardhi ambayo tunaifanyia mapitio pale wizarani ili kuhakikisha kunakuwa na sura nzuri ya umiliki wa nyumba.

“Ili watu wenye mitaji yao ndani na nje waweze kuja kumiliki nyumba, waweze kupanga nyumba za ili kuongeza uwekezaji, kwa hayo niwapongeze sana.”

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Hamad Abdalah amesema kuwa, mradi wa Morocco Square umeenda vizuri kutokana na maeneo ya jengo hilo kupangishwa.

Amesema, katika nyumba 100 tayari nyumba 40 wameshaziuza. “Ni mradi ambao tunategemea baada ya kupata wapangaji utatuingizia takribani milioni 850 kwa mwezi.”

Pia, amesema huo ni mradi wa mfano nchini ambapo eneo hilo awali lilikuwa linakaliwa na familia tatu, lakini kwa sasa mbali na kupatikana makazi mengi kwa ajili ya watu, yamepatikana maeneo ya maduka, ofisi na hoteli ya kisasa.

Abdalah amesema, wanatarajia ifikapo Novemba, mwaka huu katika mradi wa Morocco Square wenye maduka watakua wamekamilisha kufunga vifaa vyao tayari kwa ajili ya kuanza kutoa huduma.

“Na tarehe Mosi mwezi Desemba tunatarajia sasa, movement itaanza, halikadhalika kwenye eneo la hoteli, tayari mpangaji ameanza kufanya fitout, na itakapofika tarehe Mosi mwezi Desemba naye ataanza kufanya biashara.

“Upande wa pili wa makazi, tayari kuna watu wanaishi, maana yake jengo limeshaanza kufanya kazi, na tunapofanya miradi hii, sisi kama shirika tunalipa kodi zote za Serikali.

“Kwa hiyo, na sisi kwenye uchumi, tuna mchango kupitia kodi hizo, vile vile kwa upande wa ajira, hawa wafanyabiashara wote watakuwa wanalipamkodi zote, maana yake tulichokifanya ni kuweza kutengeneza fursa ili wafanyabiashara waje kufanya biashara na kulipa kodi zao.

“Kwa hiyo, maana yake ni uchumi mkubwa sana ambao utatokana na uwekezaji ambao tumeshaufanya,”amefafanua Mkurugenzi Mkuu wa NHC huku akibainisha mradi wa Morocco Square umebakisha vitu vichache kukamilika kwa asilimia 100.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news