NA DIRAMAKINI
SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu barani Afrika (CAF) limeendesha na kukamilisha Droo ya hatua ya Makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika katika studio za Mshirika wa CAF Broadcast Partner SuperSport jijini Johannesburg leo Novemba 3,2025.
Katika droo hiyo mabingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania, Young Africans Sports Club (Yanga SC) imepangwa Kundi moja la B la hatua ya Makundi ya Michuano ya Ligi ya Mabingwa barani Afrika na miamba ya soka Afrika Ahly ya Misri.
Mbali ya Al Ahly, timu nyingine ambazo imepangwa nazo katika Droo iliyofanyika leo Novemba 3,2025 mjini Cairo, Misri ni ASFAR ya Morocco na JS Kabylie ya Algeria.
Aidha, Simba SC imepangwa Kundi D la Michuano ya Ligi ya Mabingwa barani Afrika hatua ya makundi ikiwa na miamba ya Tunisia Espérance Sportive de Tunis, Atlético Petróleos de Luanda ya Angola na Stade Malien ya Mali.
Katika droo hiyo timu za RS Berkane na Pyramids FC ambao ni Washindi wa Kombe la Shirikisho na CAF Champions League msimu uliopita wamepangwa Kundi A Pamoja na Rivers United ya Nigeria na Power Dynamos ya Zambia.
Kundi C wapo Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini, Al Hilal SC ya Sudan, MC Alger ya Algeria Pamoja na St Éloi Lupopo ya DR Congo.
Kwa upande wa Singida Black Stars ya Tanzania imepangwa kundi C la Michuano ya Kombe la Shirikisho hatua ya makundi ikiwa pamoja na wababe CR Belouizdad ya Algeria, Stellenbosch FC ya Afrika Kusini na AS Otohô ya Congo.
Nayo Azam FC imeangukia kundi B la Michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika wakipangwa na miamba ya Morocco Wydad AC ya akina Aziz Ki, AS Maniema ya Congo pamoja na Nairobi United FC ya Kenya.
