NA DIRAMAKINI
MKUU wa Jeshi la Polisi nchini, Camillus Wambura amemteua Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Twaha Juma Lulengelule kuwa Kamanda mpya wa Polisi Mkoa wa Tabora (RPC).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi Makao Makuu,DCP David Misime uteuzi huo umefanyika kufuatia uhamisho wa ACP Lulengelule kutoka nafasi yake ya Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (RCO) Mkoa wa Tabora kwenda kushika wadhifa wa Kamanda wa Polisi wa mkoa huo.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa,uteuzi huo unalenga kuziba nafasi iliyokuwa wazi baada ya aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Richard George Abwao, kufariki dunia Juni 20, 2026, alipokuwa akipatiwa matibabu jijini Dar es Salaam.
Jeshi la Polisi limesema mabadiliko hayo ni sehemu ya utaratibu wa kawaida wa kuimarisha uongozi na kuhakikisha shughuli za ulinzi, usalama na utekelezaji wa majukumu ya Jeshi la Polisi zinaendelea bila kuathiriwa.
ACP Lulengelule anaingia katika nafasi hiyo akiwa na uzoefu wa kazi za upelelezi wa makosa ya jinai, ambapo anatarajiwa kuendelea kusimamia shughuli za ulinzi na usalama pamoja na kuimarisha mapambano dhidi ya uhalifu katika Mkoa wa Tabora.
