Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha ADC, Queen Sendiga amesema kuwa mgombea yeyote atakayeshinda katika kinyang'anyiro hicho ni muhimu kushirikiana na ilani ya vyama vingine ili kuwaletea maendeleo wananchi, anaripoti Fatma Ally (Diramakini) Dar es Salaam.
Kauli hiyo ameitoa jijini Dar es Salaam mapema leo wakati akizungumza na waandishi wa habari ikiwa bado siku moja wananchi kupiga kura na kuchagua viongozi ambao wataweza kuwaongoza miaka mitano ijayo.
Amesema kuwa, kila mgombea wa Urais aliyeshiriki katika uchaguzi mkuu mwaka 2020 ana nia ya kuleta maendeleo na mabadiliko katika Tanzania, hivyo ni vyema mgombea yeyote atakayeshinda kushirikiana na wagombea wa vyama vingine na kuchukua ilani zao japo kwa uchache.
Aidha, amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi kesho ya Oktoba 28,2020 kupiga kura kwani kura mmoja ya mtanzania inaweza kubadilisha maisha yao katika kukuza maendeleo.
Hata hivyo, amelishukuru jeshi la polisi kwa kufanya kazi zao kwa weledi wa kuwalinda viongozi hao pamoja na waandishi wa habari kwa kutoa ushirikiano kwa chama hicho na kwa kuripoti habari zao tangu walipozindua kampeni zao Septemba 11,mwaka huu.
Aidha, amesema wamehitimisha kampeni zao kwa kuzunguka wilaya 40, kata 140 pamoja na mikoa 20, ambapo leo ndio watafunga kampeni zao rasmi saa 10 jioni katika Kata ya Buguruni (Sheli) Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam.