Mtangazaji mahiri nchini Tanzania, Elisha Elia wa Shirika la Utangazaji
Tanzania ( TBC ) amefariki Dunia leo Oktoba 24,200 katika Hospitali ya
Taifa Muhimbili iliyopo jijini Dar es Salaam, anaripoti Mwandishi
Diramakini.
Hayo yamethibitishwa na Mkurugenzi Mkuu wa TBC,
Dkt.Ayub Rioba ambaye amebainisha kwa kifupi kuwa, ndugu Elisha Elia
alikuwa akipatiwa matibabu hospitali hapo.
Aliyekuwa Mtangazaji wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Elisha Elia ambaye amefariki dunia leo Oktoba 24,2020 wakati akiendelea na matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
"Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Dkt. Ayub Rioba anasikitika kutangaza kifo cha mfanyakazi, Mwandishi wa Habari Elisha Elia, kilichotokea tarehe 24/10/2020 katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, alikokuwa amelazwa kwa matibabu,"imeeleza sehemu ya taarifa fupi ya Dkt.Rioba iliyotolewa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).
Wakati huo huo, Msemaji Mkuu wa Serikali ambaye pia ni Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Hassan Abbasi ametoa salamu za pole kwa ndugu jamaa na marafiki.
"Kwa niaba ya Serikali tumepokea kwa masikitiko kifo cha Mtangazaji mahiri wa TBC, Ndugu Elisha Elia, kilichotokea leo Dar es Salaam. Elisha atakumbukwa kwa kipaji chake adhimu katika uandishi wa habari za magazeti na baadaye kuwa mtangazaji galacha,"ameeleza Msemaji Mkuu wa Serikali kupitia ukuta wake wa Twitter. Mwandishi Diramakini atakuwa anakujuza mara kwa mara kinachojiri katika blog hii, usikae mbali.