Kufuatia agizo la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,Aboubakar Kunenge kuitaka Taasisi ya TICTS kuhakikisha kontena sita zenye vifaa vya ujenzi wa stendi mpya ya Mbezi Louis zilizokuwa zimekwama bandarini kutoka ndani ya saa mbili, hatimae taasisi hiyo imetekeleza mara moja agizo hilo.

Mapema leo RC Kunenge amefika stendi mpya ya Mbezi Louis kujihakikishia kama kontena hizo zimefika ambapo amethibitisha kujionea kontena zote sita zimefika na kufanya idadi ya kontena zilizotoka kufikia 14.


Aidha,RC Kunenge amebainisha kuwa, kontena zilizofika ndani yake kuna vifaa mbalimbali ikiwemo vioo, fremu za madirisha, mabati na kueleza kuwa vifaa hivyo vimeanza kutumika mara tu vilipofika.
Hata hivyo,RC Kunenge ameendelea kumtaka Mkandarasi kufanya kazi usiku na mchana ili stendi hiyo ikamilike kabla ya Novemba 30,mwaka huu kama alivyoagiza, Rais Dkt. John Magufuli wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi.
Itakumbukwa jana Oktoba 23,mwaka huu RC Kunenge alifanya ziara ya kushtukiza kwenye Bandari ya Dar es Salaam kufuatilia kinachokwamisha kutoka kwa kontena hizo na kubaini kasoro za kiutendaji na kuamua kutoa maagizo ya kutaka kontena hizo zitoke ndani ya saa mbili.
Tags
Habari