Mwanaharakati apangua hoja za Mbowe dhidi ya Hayati Magufuli

Sadicki Godigodi ambaye ni Mwenyekiti wa Taasisi isiyo ya Kiserikali ya Tanzania Peace Foundation amesema hotuba iliyotolewa na Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe jana mkoani Dar es Salaam imejaa ghilba na upinzani kwa Taifa, anaripoti Mwandishi DIRAMAKINI (Dar es Salaam).
 
Amesema ni upinzani usiokuwa na tija badala yake unalenga kuligawa taifa.Ameyasema hayo leo Aprili 12, 2021 wakati akizungumza na waandishi wa habari.
 
Mheshimiwa Freeman Mbowe jana Aprili 11, 2021 wakati akizungumza kupitia kwenye mitandao ya kijamii alianisha mambo mbalimbali aliyodai yalijiri kipindi cha uongozi wa aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Dkt.John Magufuli, ambaye alifariki Machi 17, mwaka huu katika Hospitali ya Mzena, Dar es Salaam alipokuwa kipatiwa matibabu.

Godigodi amesema, taasisi hiyo inayojishughulisha na misingi ya amani nchi, wameona watoe tamko na ushauri wao kwa Mbowe, chama chake, vyama vya siasa na viongozi wengine wenye mitazamo kama ya kwake (Freeman Mbowe).
 
Pia amesema,Hayati Rais Magufuli alikuwa na msimamo thabiti katika kusimamia rasilimali za taifa na katika kuwatetea wanyonge kiasi cha kujisikia wapo huru katika Taifa lao.
 
Mbali na hayo amempongeza Mbowe kwa kuzungumzia kipaji cha Hayati Rais Magufuli katika kufanya maamuzi magumu katika mambo mbalimbali yaliyohusu Taifa na kutaka watu kufanyakazi.
 
Amesema, kwa kutambua hayo tunampongeza Mbowe kwa maneno yake hayo, kwa maana ni kweli Magufuli alikuwa na misimamo isiyoyumba, iliyokuwa thabiti.

Godigodi amesema kuwa,kwa masikitiko makubwa wao kama taasisi ya amani wamesikitishwa na baadhi ya matamshi ya Mbowe aliyodai yalijaa hila chafu yenye mlengo wa kuvunja umoja wa kitaifa na amani ya nchi.
Amesema, miongoni mwa mambo aliyoyazungumzia Mbowe ni pamoja na mikataba mingi mibovu, kipindi ambacho yeye kama kiongozi wa upinzani Bungeni alikuwa akilalamikia sana juu ya mikataba mibovu na kwenye hotuba zake Bungeni aliyazungumza hayo na kutoa ushauri juu ya kurekebishwa kwa mikataba hiyo au kuvunjwa kabisa.

"Baada ya Hayati Magufuli kuingia madarakani alifanya yale ambayo wao walikuwa wakiyashauri kama upinzani kwa kuvunja mikataba mibovu isiyokuwa na tija na kurekebisha iliyorekebishika, kwa hiyo sio kweli kuwa utawala wa Rais Magufuli ulifukuza wawekeza, bali wawekezaji wanyonyaji waliondoka baada kukataa kurekebisha mikataba isiyokuwa na tija kwa taifa letu,"amesema Godigodi.

Hata hivyo, amesisitiza kuwa, wawekezaji wengi katika sekta mbalimbali walikubali kurekebisha mikataba yao na kuwa yenye haki na usawa kwa maslahi ya Taifa ili waendelee kufanyakazi zao na kulipa kodi stahiki kwa mujibu wa mikataba hiyo.

Amefafanua kwamba, CHADEMA ilikuwa na sera katika ilani yake ya uchaguzi mwaka 2015 ya kutoa elimu bure kuanzia darasa la awali hadi kidato cha nne, dhana ambayo Hayati John Magufuli ameitekeleza kwa vitendo.

Amesema, Mbowe alitakiwa kujua kuwa nchi yetu imeingia uchumi wakati katika kipindi kigumu cha Corona cha uongozi wa Rais Magufuli, ambapo mataifa makubwa yenye nguvu na uchumi yaliporomoka katika kipindi hicho.

"Tunauliza hivi ni kweli dhana ya Hayati Magufuli kukataa kuwafungia watu ndani na badala yake kutaka Watanzania kufanyakazi lilikuwa ni kosa? Hivi msimamo wa Dkt. Magufuli kuwatoa hofu wa Watanzania wakati wa Corona ilikuwa ni dhambi," alisema na kuongeza kuwa hayo ni mambo ambayo tunatakiwa kujiuliza kama Watanzania. 

Pia amesema, CHADEMA ilikuwa ikidai kuwa tulikuwa na Rais mpole kabla ya Hayati Magufuli, hivyo tunahitaji Rais jasiri na mkali, na hivyo hivyo Hayati Magufuli alikuwa jasiri na mkali kwa raslimali za umma.

"Leo hii CHADEMA kupitia kwa Mbowe wanaituhumu Serikali ya Rais Magufuli kwa chuki, haikuwa haki hata kidogo na sisi kama taasisi tunajiuliza wanafanya hivyo kwa maslahi ya nani, kama si kuligawa taifa,"ameongeza.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news