Waziri Mkuu asisitiza ajira kwa wananchi wanaoishi karibu na kiwanda

NA MWANDISHI MAALUM

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Masha Mshomba atoe kipaumbele wakazi wa eneo la Ngomeni katika suala la ajira kwenye kiwanda cha kuzalisha bidhaa zinazotokana na zao la mkonge cha Sisalana.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiangalia zulia lililotengenezwa na zao la mkonge, wakati alipokagua kiwanda cha Mkonge cha Sisalana (T) Co. Ltd, Novemba 18, 2021 jijini Tanga. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Kiwanda hicho kilichopo katika eneo la Ngomeni Mkoani Tanga ambacho NSSF ilitoa takribani shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kukifufua ikiwa ni utekezaji wa kampeni ya ujenzi wa viwanda.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo Novemba 18, 2021 alipotembelea kiwanda hicho ambacho kabla ya kufanyiwa maboresho kilikuwa kinazalisha tani 1.5 hadi 2.5 kwa siku ambapo kwa sasa kinazalisha tani 20 kwa siku.

Mheshimiwa Majaliwa amesema kwa kuwa kiwanda hicho ambacho kipo katika kata ya Ngomeni wilayani Muheza ni vema kwa uongozi wa NSSF ukatoa kipaumbele cha ajira kwa wananchi wanaozunguka eneo ili waweze kunufaika na uwepo wake.

Kadhalika, Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwahamasisha wananchi hao watumie uwepo wa kiwanda hicho kwa kulima zao la mkonge kwa wingi kwani wanasehemu ya uhakika ya kuuza zao hilo ambalo lina faida.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama amewaagiza Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF pamoja na Afisa Kazi wa Mkoa wa Tanga wakutane na waliokuwa wafanyakazi wa kiwanda hicho na kushirikiana nao kutatua changamoto zinazowakabili.

Kampuni ya Sisalana ilianza kazi rasmi kiwandani Machi 12, 2021 ambapo ilikuta hali ya uzalishaji ikiwa ni ya kusuasua kutokana na ukosefu wa mtaji wa kuendeshea biashara na uchakavu wa mitambo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news