RUWASA mkoani Ruvuma yazidi kufanya makubwa kupitia fedha za UVIKO-19

NA DIRAMAKINI

KATIKA mkakati wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Rais Samia Suluhu Hassan wa kumtua ndoo mama kichwani, Wakala wa Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Mkoa wa Ruvuma umeendelea kutekeleza miradi ya maji kupitia fedha za Ustawi za UVIKO-19 zilizotolewa na Serikali.
Meneja wa Wakala wa Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Rebman Ganashonga akifafanua jambo wakati akielezea hatua mbalimbali za utekelezaji wa miradi inayotekelezwa kwa fedha za Ustawi za UVIKO-19 ambazo zimetolewa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.Katika mkoa huo kuna miradi saba ya maji inayotekelezwa kwa fedha ambayo itagharimu sh.bilioni 4.8.

Kupitia fedha hizo za Ustawi, RUWASA Mkoa wa Ruvuma wanatekeleza miradi saba ya maji katika wilaya mbalimbali za mkoa huo na kwa sasa ujenzi umefikia wastani wa asilimia 52 na matarajio ifikapo Mei 15 mwaka huu wananchi waliopo maeneo ya miradi hiyo wataanza kupata maji safi na salama.

Akizungumza na waandishi wa habari waliopo kwenye ziara ya kutembelea miradi ya maji inayotekelezwa kwa fedha za Ustawi za UVIKO-19, Meneja wa RUWASA Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Rebman Ganshonga amefafanua hatua kwa hatua kuhusu utekelezaji wa miradi hiyo.

Ambapo amesema, utekelezaji wa miradi ya maji kupitia fedha za ustawi za UVIKO-19 kwa Mkoa wa Ruvuma iko miradi saba inayogharimu fedha Sh. Bilioni 4.8 na fedha hizo zinajumuisha ununuzi wa bomba,pampu na shughuli nyingine za ujenzi.
"Kwa Mkoa wa Ruvuma nafasi ya RUWASA katika kumtua ndoo mama kichwani ,niseme tu RUWASA ni moto wa kuotea mbali na inaupiga mwingi na Waziri wetu wa Maji Juma Aweso amekuwa na msemo wake unaosema ukiona Kobe kapanda juu ya mti ujue ana mwenyewe,kwa hiyo RUWASA inafanya kazi sana na wote ni mashahidi.

"Na itakapofika mwaka 2025 ili kumtua mama ndoo katika Mkoa wetu isiwe chini ya asilimia 85 ya upatikanaji maji ndani ya Mkoa wetu.Hilo linawezekan kwa sababu Rais wa nchi yetu Mama Samia Suluhu Hassan ameendelea kuhangaika kutafuta fedha kwa ajili ya miradi ya maji na hatimaye kumtua ndoo mama kichwani.

"Kwani hata hizi fedha za Ustawi za UVIKO-19 hazikuwa kwenye sekta ya maji, lakini kwa kuwa anaujua uchungu wa akina mama akaamua sehemu ya fedha hizo ziende kwenye ujenzi wa miradi ya maji,hivyo kwa juhudi alizonazo Rais, Waziri wetu pamoja na Mtendaji wetu Mkuu wa RUWASA tunaamini kwa Mkoa wa Ruvuma mwaka 2025 kwa baadhi ya Wilaya wanasiasa hawatakuwa na ajenda ya kuzungumzia changamoto ya uhaba wa maji,"amesema Mhandisi Ganshonga.
Moja ya tenki la maji ambalo limejengwa katika Kijiji cha Amani Makoro kama linavyoonekana ambalo kwa sasa liko hatua za mwisho za umaliziwaji .Tanki hilo ni sehmu ya mradi unaotekelezwa kwa fedha za Ustawi za UVIKO-19.

Ametoa mfano kuwa katika Wilaya kama Mbinga Mjini wanaamini kama mambo kama yatakwenda kwa nguvu aliyonayo Rais Samia basi upatikanaji wa maji utafika asilimia 100 kwa Mbinga Mjini.Ukienda Madaba ni hivyo hivyo."Kwa hiyo tunaomba Mungu aendelee kumpa nguvu Rais wetu, aendelee kumpa mbinu nyingine za kutafuta fedha ili tutekeleze miradi mingi zaidi na kwa wakati mfupi ili tumtue ndoo mama kichwani".

Aidha amesema kwa ujumla kwa Mkoa wa Ruvuma kuna miradi mingine inayoendelea kutekelezwa ukiondoa miradi inayotekelezwa kwa fedha za Ustawi, hivyo miradi hiyo imefanya upatikanaji maji kufikia asilimia 68 kutoka asilimia 56 ndani ya Mkoa huo maeneo ya Vijijini na kwa Mjini miradi ikikamilika watafika asilimia 86."Kwa hiyo tunategemea miradi ikikamilika yote ambayo inatekelezwa kwa kila Wilaya, upatikanaji maji utafikia asilimia 75 kwa Vijijini na Asilimia 88 kwa maeneo ya mijini.
Baadhi ya mabomba ambayo ni maalum kwa ajili ya kusambaza maji yanayotokana na mradi wa fedha za Ustawi za UVIKO-19 ambazo zimetolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yakiwa yamehifadhiwa kabla ya kufukiwa kwenye mitaro kwa ajili ya kusambaza maji kwa baadhi ya vijiji vya Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma.

Akizungumza uharibifu wa vyanzo vya maji kwa Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Ganshonga amesema uharibifu ni mkubwa sana lakini wanamshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia Mkuu wa Mkoa huo ambaye amekuwa mstari wa mbele wa kukemea uharibifu wa vyanzo vya maji na amekuwa akisisitiza vyanzo hivyo kulindwa kwa nguvu zote.

"Mkuu wa Mkoa kwa kushirikiana na Bodi ya Bonde la Ziwa Nyasa tunaendelea kuvilinda vyanzo hivyo na kuwaondoa wale wote wanaofanya shughuli mbalimbali ambazo zinaharibu vyanzo hivyo.Tumekuwa tukiweka mipaka ili wananchi wasiingie kwenye maeneo ya vyanzo vya maji,"amesema.

Ameongeza kwa Mkoa wa Ruvuma maeneo ambayo yamekuwa na uharibifu mkubwa wa vyanzo vya Maji ni katika Wilaya Mbinga na Wilaya ya Halmashauri ya Madaba ambako kuna mto tegemeo kwa halmashauri ya Madaba mto Mgombezi ambako kwenye chanzo muhimu sana wananchi wamelima na wamejenga nyumba lakini kwa juhudi za Mkuu wa Mkoa wanashirikiana kulinda vyanzo hivyo ikiwa pamoja na kuweka mipaka.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news