KWA KUPENYEZA RUPIA:Madhara yanaingia, rushwa ikituingia

NA LWAGA MWAMBANDE

UKITAKA kujua kuwa, rushwa si adui wa haki tu bali adui wa maisha yako, jaribu kuingia katika anga za Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).

TAKUKURU, hiki chombo huru cha umma kilichoundwa kwa mujibu wa Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11 ya Mwaka 2007.

Kifungu cha 4 cha sheria hii, kikisomwa pamoja na kifungu cha 7 kinaeleza majukumu ya TAKUKURU ambayo yamegawanyika katika dhana kuu mbili ambazo ni Kuzuia Rushwa na Kupambana na Rushwa.

Aidha, katika kuzuia vitendo vya rushwa, TAKUKURU inafanya utafiti ili kubaini mianya ya rushwa na kushauri namna ya kuondoa mianya iliyobainika.

Vilevile, TAKUKURU inafuatilia matumizi ya rasilimali za umma zilizotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili rasilimali hizo zitumike kwa kadri ya malengo yaliyokusudiwa.

Waswahili wanasema, bora utembee umbali mrefu kwa miguu, lakini si kujitafutia ya kujitakia kwa kujihusisha na masuala ya rushwa, kwani TAKUKURU ina macho zaidi ya mawili.

Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema kuwa,rushwa ni upofu mbaya na kama hiyo haitoshi,madhara yake huwa yanaingia baada ya rushwa kutuingia, endelea:

1.Pale palipo udhia, wewe penyeza rupia,
Nini walifikiria, hilo kutuanzishia,
Ona tunavyotumia, tena tunafurahia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

2.Udhia twauchukia, mbali twaufagilia,
Wengine wakiumia, wenyewe tajijulia,
Sisi tukifurahia, waacheni wakilia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

3.Haki wengine udhia, chini wanaiminyia,
Na wenye mpini pia, ndiyo wajifaidia,
Wanyonge hao walia, wapi kwa kukimbilia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

4.Wale wanaotumia, kuipenyeza rupia,
Wengi twawashangilia, maisha wayajulia,
Waso pesa wasalia, meno wakijisagia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

5.Ni wapi tutafikia, usawa kuujulia,
Wapi tutakopitia, haki kuisimikia,
Nani anakujulia, atuelekeze pia?
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

6.Madhara yanaingia, rushwa ikituingia,
Wengine wanaishia, na hatutawasikia,
Wabaya wafurahia, pasipo wanasalia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

7.Kwa kupenyeza rupia, mazuri kujipatia,
Wengine kuharibia, ili wazidi fifia,
Tunakwisha nakwambia, mwisho hatutafikia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

8.Michezoni twasikia, mambo ni kama rupia,
Ya Blatter lisikia, kule alikoishia,
Pini unazisikia, watu zinawashukia?
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

9.Vipofu waangalia, maamuzi yalovia,
Hata mkifanyizia, viza weshawatupia?
Kesho mkiwafungia, chao kishajipatia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

10.Wapi utanitajia, kusikochafu rupia?
Ambako wakufikia, bila kitu tangulia?
Hii ya kwetu dunia, ndiyo hivyo yaishia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

11.Rushwa kama watumia, pahala kupafikia,
Wengine wanaumia, chini wawakanyagia,
Pazuri hutafikia, aibu itakujia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

12.Imani kitangulia, ya kumwogopa Jalia,
Kote tukiangalia, mambo tutafurahia,
Yale tutajipatia, ya halali nakwambia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

13.Vinginevyo twatitia, vile tunashikilia,
Tutakapokufikia, hongo ikiwa ni nia,
Hatuwezi kufikia, chini ndipo tasalia,
Rushwa hongo wabugia, kujisafishia njia.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news