Mandonga akabidhiwa zawadi gari la pili,kutoka Sugunyo hadi Kantangaze

NA DIRAMAKINI

BONDIA Mtanzania Karim Mandonga (Mtu Kazi) amekabidhiwa gari mpya aina ya Subaru Impreza na Kampuni ya Mo Green International

Makabidhiano hayo yamefanyika Januari 20, 2023 maeneo ya Mwenge jijini Dar es Salaam huku bondia huyo akiendelea kuonesha moyo wa shukurani kwa wadau mbalimbali.

Hilo linakuwa gari la pili baada ya lile la awali alilokabidhiwa kutokana na ahadi ya endapo angeshinda pambano lake nchini Kenya dhidi ya Mkenya Daniel Wanyonyi.

Alipewa zawadi ya gari hilo aina ya Nadia na mfanyabiashara Dick Sound bila mashariti yoyote ikiwa ni sehemu ya kutimiza ahadi aliyokuwa ameahidiwa endapo angeshinda pambano hilo.

Tukio hilo lilifanyika katika Ofisi za DickSound Mall maeneo ya Magomeni jijini Dar es Salaam ambapo Dick alisema. “Nimempa kama zawadi siyo kwa ajili ya Ubalozi, alikuja kwangu wakati anaenda kupambana nikamuahidi akishinda nitaweza kumpa gari.

"Wakati akiwa Kenya nikaona video nikamtumia kumwambia umeniangusha ushapigwa, akasema hapana sio kweli. Mimi ndio napanda kupambana, hivyo leo tumemkabidhi kumpongeza na kutimiza ahadi”

“Namshukuru sana DickSound Kwa hili leo ndoto yangu imetimia, Mandonga anaondoka na usafiri Mungu mkubwa,"alisema Mandonga.

Baada ya kukabidhiwa gari hilo la pili ikiwa ni mwendelezo wa furaha ya ushindi dhidi ya Mkenya Daniel Wanyonyi ambaye alimshinda katika raundi ya tano kwa TKO akitumia ngumi aliyoipa jina la Sugunyo, Mandonga ametangaza ngumi mpya inayoitwa 'Mo Strong Kantangaze'.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news