Wiki ya Sheria yazinduliwa Geita

NA MWANDISHI WETU

WIKI ya Sheria mkoani Geita imezinduliwa kama ilivyo kwa nchi nzima kwa kuanza na maandamano yaliyojumuisha watumishi, wadau mbalimbali pamoja na wananchi ambao wote walishiriki kikamilifu.
Maandamano hayo yalipokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Geita,Mhe.Wilson Shimo akiwa pamoja na mwenyeji wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mhe. Cleofas Waane.

Wakati anamkaribisha Mkuu wa Wilaya, Mhe. Waane aliwakaribisha wananchi wote kufika katika vituo vilivyoandaliwa ili waweze kunufaika na elimu itakayotolewa katika Wiki ya Sheria nchini.
“Leo ni siku nzuri na maalumu kwa ajili ya wananchi na wadau wa sheria wote mkoani Geita ambayo sasa inafungua fursa kwa wote kuweza kupata elimu juu ya masuala mbalimbali ya kisheria,” alisema.

Akizungumzia kauli mbiu ya mwaka huu ambayo ni “Umuhimu wa utatuzi wa Migogoro kwa njia ya usuluhishi katika kukuza uchumi endelevu: Wajibu wa Mahakama na wadau.”

Mhe. Waane alibainisha kuwa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi unatambulika kisheria, huchochea ukuaji wa uchumi na kuimarisha amani na mahusiano.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Geita, akizungumza katika hafla hiyo, aliipongeza Mahakama kwa kudumisha maazimisho hayo kila mwaka ambapo wananchi hupata fursa ya kujifunza mambo mbalimbali ya kisheria.

Alisema kuwa uwepo wa Wiki ya Sheria hukumbusha kila mwananchi kwamba hakuna aliye juu ya sheria na Mahakama ndiyo chombo pekee kilichoidhinishwa kikatiba kutoa haki.

Mhe. Mkuu wa Wilaya amesisistiza na kuwaomba wananchi wote kuitumia fursa hiyo kupata elimu ya kisheria. “Tunapaswa kuitumia vyema fursa hii ili tuweze kujifunza kupitia vituo hivi na jambo zuri ni kwamba wanaotoa elimu katika wiki hii ndiyo wale wanaotoa tafsiri ya sheria, hivyo tuitumie fursa hii,” alisisitiza.

Akielezea kauli mbiu ya mwaka huu, Mkuu wa Wilaya huyo alisema kuwa imebeba ujumba muhimu kwa kuwa inakumbusha kusuluhisha migogoro kwa kukaa pamoja bila kufika mahakamani, hivyo kuipunguzia Mahakama mlundikano wa mashauri.
Mhe. Shimo alitumia fursa hiyo kumshukuru Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma kwa kuweka mpango wa kuanzisha Mahakama Kuu katika Mkoa wa Geita kwani itasaidia kuwapunguzia wananchi gharama za kuifuata huduma hiyo katika Mkoa wa Mwanza.

Ameomba kama ikiwezekana huduma ya Mahakama Kuu ianze hata kabla ya jengo linalotarajiwa kujengwa kwa kupitia majengo mengine na yeye mwenyewe yupo tayari kutoa ushirikiano kufanikisha mpango huo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news