TANZANIA, BORA KUISHANGILIA-13: Karibu mkoani Mara,Penye utajiri mkubwa

NA LWAGA MWAMBANDE

HISTORIA inaonesha kuwa,Mkoa wa Mara una eneo la kilomita za mraba 30,150. Kati ya eneo hilo kilomita za mraba 10,942 ni eneo la maji sawa na asilimia 36 na kilomita za mraba 19,208 sawa na asilimia 64 ni eneo la nchi kavu.

Aidha, katika eneo la nchi kavu,kilomita za mraba 9,452.34 sawa na asilimia 49.2 ziko katika hifadhi za wanyamapori, ikiwemo Hifadhi ya Taifa Serengeti, Mapori ya Akiba ya Ikorongo na Grumeti na Hifadhi za Jamii Grumeti na Ikorongo.

Ukiondoa eneo hilo mkoa unabakiwa na kilomita za mraba 9,755.66 sawa na asilimia 50.7 ya eneo la nchi kavu kwa ajili ya kilimo, mifugo na makazi.

Mara wanapakana na nchi ya Kenya na Uganda kwa upande wa Kaskazini,mikoa ya Kagera na Mwanza upande wa Magharibi, Mkoa wa Simiyu kwa upande wa Kusini na Mkoa wa Arusha kwa upande wa Mashariki.

Muonekano wa Mji wa Musoma ambao ni makao makuu ya Mkoa wa Mara, Mei 18, 2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Kiutawala, mkoa umegawanyika katika wilaya sita ambazo ni Musoma, Butiama, Bunda, Serengeti, Tarime na Rorya zenye halmashauri tisa ambazo ni Manispaa ya Musoma, Butiama, Bunda, Bunda Mji, Serengeti, Tarime, Rorya na Tarime Mji.

Historia ya Mkoa wa Mara inaanzia mwaka 1961 ukiwa pamoja na mikoa ya Mwanza na Shinyanga ya sasa wakati huo ikijumuishwa kwenye Jimbo la East Lake Province huku makao makuu yakiwa Mwanza.

Miongoni mwa wilaya zilizounda East Lake Province ni pamoja na wilaya za North Mara na South Mara ambazo ndiyo chimbuko la Mkoa wa Mara ulioanzishwa mwaka 1963 ukiwa ni miongoni mwa mikoa 26 ya Tanzania Bara na mikoa 31 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sasa.

Tangu wakati huo makao makuu ya Mkoa wa MARA yakawa Musoma. Mkuu wa Mkoa wa kwanza akiwa Mhe.John S. Malecela kati ya mwaka 1963 hadi 1965.

Vile vile, Mkoa wa Mara ni chimbuko la viongozi mashuhuri akiwemo Rais wa Kwanza na Muasisi wa Taifa la Tanzania, Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambaye alizaliwa Aprili 13, 1922 katika Kijiji cha Butiama na kufariki na kuzikwa katika kijiji cha Butiama tarehe 14 Oktoba, 1999.

Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ndiye Muasisi wa Chama cha TANU kilichoongoza harakati za Uhuru. Aidha, Mwalimu alikuwa Muasisi wa Chama Cha Mapinduzi tarehe 5 Februari, 1977 baada ya vyama vya siasaTANU na AFRO SHIRAZI kuungana.

Viongozi wengine wa Kitaifa ambao ni wazaliwa wa mkoa huo ni Waziri Mkuu mstaafu Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba ambaye alikuwa Waziri Mkuu tangu mwaka 1985 hadi mwaka 1990,wakuu wa majeshi wastaafu Jenerali David Msuguri na Joseph Waitara.

Mbali na hayo, mkoa huo umejaliwa kutoa viongozi wa ngazi za juu serikalini wakiwemo mawaziri,mabalozi na wakuu wa taasisi mbalimbali za Serikali.

Uchumi wa Mkoa wa Mara unategemea zaidi kilimo ambacho huchangia kiasi cha asilimia 60 ya pato la mkoa huku sekta nyingine ambazo huchangia kwenye uchumi wa mkoa ni za mifugo, madini, uvuvi na utalii.

Mkoa wa Mara umegawanyika katika kanda tatu kijiografia ikiwemo Nyanda za Juu ambayo hupata mvua mara mbili kwa mwaka, wastani wa mm.1500.

Nyanda hizi zina ardhi nzuri yenye rutuba na zina wakazi wengi. Eneo kubwa la nyanda za juu liko mpakani Kaskazini Mashariki ya Wilaya ya Tarime.

Shughuli kuu ya kiuchumi katika eneo hilo ni kilimo cha nafaka hasa mahindi,ndizi,viazi na mihogo. Pia kuna mazao ya biashara ya kahawa,chai na tumbaku.

Ukanda wa kati ambao una miinuko michache na mbuga pana zenye nyasi zinazofaa kwa malisho ya mifugo unaanzia Wilaya ya Tarime na kuenea wilaya yote ya Serengeti na kuishia Mashariki ya Wilaya ya Musoma.

Hupata mvua za wastani wa mm.1000 kwa mwaka na shughuli kuu za kiuchumi kwa wakazi wa eneo hili ni ufugaji wa ng’ombe,mbuzi,kondoo na kilimo cha mazao kama vile mahindi,mtama,ulezi na mihogo.

Kwa upande wa ukanda wa chini ambao upo katika mwambao wa ziwa unachukua sehemu kubwa ya eneo la mkoa huo katika wilaya za Bunda, Musoma na Rorya.

Ukanda huu hupata mvua za wastani mm.700 kwa mwaka na kwa kipindi kirefu cha mwaka hubakia kame. Wakazi wa eneo hili hujishughulisha zaidi na kilimo cha pamba, mihogo na nafaka. Ufugaji nao ni shughuli muhimu kama ilivyo uvuvi. Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema karibu Mkoa wa Mara uweze kujifunza mengi, Endelea;


1. ‘Haroo’ ukisikia,
Jua Mara waingia,
Hao nawafagilia,
Ni ngangari na makini.

2. Kona kona nakwambia,
Hawataki kusikia,
Mambo ya tamthilia,
Kasimulie uwani.

3. Ni wazuri nakwambia,
Akili wanatumia,
Kazi wanajifanyia,
Wako mbioni mbioni.

4. Samaki wanajilia,
Wa Ziwa Victoria,
Wengine wawavulia,
Kutoka Mara mtoni.

5. Serengeti twatambia,
Mbuga huko yapitia,
Uchumi inachangia,
Fedha nyingi za kigeni.

6. Mbuga hii nakwambia,
Maajabu ya dunia,
Wanyama wamejazia,
Wasikika duniani.

7. Sijafika nasikia,
Na picha naangalia,
Mandhari inavutia,
Kuwaona burudani.

8. Wanyama tunachangia,
Wakenya Watanzania,
Wanyama wajipitia,
Nchi kavu na majini.

9. Wanyama wanapitia,
Hatari nyingi za njia,
Hasa wanapovukia,
Mto Mara bila honi.

10. Mamba nao hupania,
Chakula kujipatia,
Minyama wanajilia,
Wakivizia mtoni.

11. Hii nikiangalia,
Changamoto ya dunia,
Mengi tunayapitia,
Wengine hufa njiani.

12. Msimu ukifikia,
Wazalia Tanzania,
Kenya wanakurudia,
Tanzania ni nyumbani.

13. Nyumbu wanavyohamia,
Kenya wewe nakwambia,
Maajabu nakwambia,
Yatangazwa duniani.

14. Wageni wakimbilia,
Kuja kuwaangalia,
Waende kusimulia,
Wakirejea nyumbani.

15. Kuja kwao nakwambia,
Pesa tunajipatia,
Hivyo tunajivunia.
Ni utajiri nchini.

16. Mara kwa kilimo pia,
Mambo yao yavutia,
Mazao wajipatia,
Kwa chakula na sokoni.

17. Chai kahawa sikia,
Huko utajipatia,
Mazao mengine pia,
Utayapata shambani.

18. Ufugaji natajia,
Mara watajirikia,
Ng’ombe wanajivunia,
Wajaa wengi zizini.

19. Nyama kweli wajilia,
Na maziwa kujazia,
Japo kupo kuibia,
Na ugomvi vijijini.

20. Mara ni vichwa sikia,
Watu huko wajazia,
Akili twajivunia,
Mabingwa wengi nchini.

21. Huko tunajivunia,
Viongozi Tanzania,
Waliotutumikia,
Miaka mingi zamani.

22. Nyerere nakutajia,
Uhuru lipigania,
Tena akasimamia,
Umoja pia amani.

23. Ukitaja Tanzania,
Jina linalokujia,
La kwanza kulisikia,
Ni la Mwalimu nchini.

24. Sifaze kukutajia,
Muda ntakumalizia,
Itoshe kukuambia,
Ni mwanzilishi nchini.

25. Muasisi Tanzania
Kisha akatangulia,
Hawezi kuturudia,
Vyema tumuombeeni.

26. Hakuwa wa Tanzania,
Mwalimu ninakwambia,
Huyo tunajivunia,
Kotekote duniani.

27. Ukombozi nakwambia,
Kote aliuchangia,
Haki alipigania,
Kote kote duniani.

28. Msumbiji lichangia,
Angola na Namibia,
Zimbabwe na tena pia,
Afrika ya kusini.

29. Burundi watakwambia,
Amani lishadidia,
Hadi sasa wafikia,
Wanaishi kwa amani.

30. Kusini Kusini pia,
Nyerere lipigania,
Waweze kujipatia,
Uchumi pia amani.

31. Kwa hoja alitulia,
Jinsi alipangilia,
Hapa ninamsifia,
Hata kote duniani.

32. Kote utakopitia,
Nyerere wamsifia,
Kwa Mandela, Namibia,
Jina liko midomoni.

33. Barabara kisikia,
Jinale mezipatia,
Zimbabwe ukiingia,
Hata Maputo jijini.

34. Butiama nakwambia,
Ndiyo kwake fwatilia,
Vile alijiishia,
Hakujikweza thamani.

35. Mungu ametusazia,
Mama Maria sikia,
Huyu tunajivunia,
Anatupamba nchini.

36. Maisha twamtakia,
Afya inayozidia,
Tuzidi kujipatia,
Hekima zake makini.

37. Mara walitupatia,
Warioba nakwambia,
Msomi alobobea,
Kuwemo serikalini.

38. Yeye aliwahi pia,
Ukuu kuupitia,
Sote tunamjulia,
Kwa utumishi makini.

39. Mengi alitufanyia,
Alipotutumikia,
Hata baadaye pia,
Liongoza bila soni.

40. Mkapa limtumia,
Rushwa kutuchunguzia,
Aliyotukusanyia,
Yamekuwa darubini.

41. Kikwete hakumwachia,
Katiba kuangalia,
Msingi ushatimia,
Ni nyingine darubini.

42. Jaji huyu wa dunia,
Nje alitumikia,
Hata Afrika pia,
Jina lake ni madini.

43. Mara kwake asilia,
Sisi twamshangilia,
Maisha twamtakia,
Tuchote kwake maoni.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news