Neno kwa neno, Bilionea Rostam Aziz amvua nguo Balozi Dkt.Wilbroad Slaa

NA GODFREY NNKO

MFANYABIASHARA wa Kimataifa, Bilionea Rostam Aziz amemtaka aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Chama wa cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA na baadaye Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Nchi za Nordic, na Baltic, Dkt.Wilbroad Slaa kuacha tabia za Kizabizabina (kuchukua maneno kutoka kwa mtu mmoja na kuyapeleka kwa mwingine kwa nia ya kufarakanisha).

Ameyasema hayo leo Juni 26, 2023 wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kuelezea kuhusiana na uwekezaji wake wa Taifa Gas nchini Zambia.

Neno, Kizabizabina limetajwa ndani ya Qur an Tukufu Surah An-Nisa ayah 143 kuwa ni sifa ya wanafiki na mnafiki kwa mujibu wa Qur an Tukufu ni mtu anayeficha kufuru kisha anadhihirisha imani haina maana.

"Lakini ndugu yangu Slaa (Dkt.Wilbroad Slaa) hakuishia hapo aliendelea kama kawaida yake kusema sema sana mambo mengine ambayo ni ya kukashifu.

"Sasa, mimi ni mfanyabiashara na nimefanya uwekezaji ndani na nje ya nchi yetu. Nimetangaza jina la Tanzania dunia nzima kwa kuwavutia wawekezaji waje wawekeze katika nchi yetu ili tutengeneze fursa nyingi za ajira na tuimarishe uchumi wa nchi yetu.

"Ningependa kuongezea,kwamba mimi sifanyi kazi na Serikali. Huwezi kusikia kwamba Rostam anaomba tenda serikalini, huwezi kusikia Rostam anauza hata sindano serikalini.

"Mimi ni mfanyabiashara ambaye ninafanya biashara na sekta binafsi, ndio maana huwezi kunituhumu ukasema huyu bwana amefanya hivi au kala rushwa au ametoa rushwa ama ni fisadi haya ni maneno ya mropokaji.

"Kwa watu ambao hawafanyi utafiti,ninasema tena mimi sifanyi biashara na Serikali, siombi tenda ya Serikali wala kuomba kuiuzia Serikali chochote kile.

"Mimi ni mfanyabiashara binafsi ninayefanya biashara na sekta binafsi,ndani na nje ya nchi, hilo ninajivunia sana, ninajivunia sana kwa sababu inawezekana kabisa kufanya biashara na sekta binafsi na watu binafsi na makampuni binafsi na ukaimarika.

"Sasa hilo jambo linanipa ushujaa mkubwa, ndiyo maana ninaweza kusimama na kusema haya ninayoyasema. Sasa huyu ndugu yangu Dkt.Slaa sijui nimjibu nini?.

"Maana historia yake haimpi heshima wala uhalali wa kujifanya eti yeye ni mtu anajali maslahi ya Mtanzania. Siku zote amejijali yeye binafsi na maslahi yake binafsi.

"Watanzania tujikumbushe historia yake na rekodi yake, kwamba huyu ni mtu ambaye aliacha kazi ya utumishi wa Mungu kanisani baada ya utovu wa maadili. Na kuona maisha yake binafsi ni bora kuliko utumishi wa Mungu.

"Ni historia ya kukosa uaminifu, na uadilifu, Watanzania pia wajikumbushe historia yake na na rekodi yake mwaka 1995.

"Kwamba huyu mtu (Dkt.Slaa) hakujiunga na upinzani kwa sababu ya imani yake, bali ni kwa sababu jina jina lake lilikatwa wakati amegombea kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) na sababu iliyotolewa ya kukatwa jina lake ni sababu ya kukosa uadilifu alivyokuwa akifanya kazi ya utumishi wa Mungu.

"Hiyo, ndiyo sababu iliyotolewa ya kumkata jina lake, kwa hiyo ndugu waandishi huyu bwana huwa anaangalia maslahi yake binafsi.

"Hakuwa mwanachama wa CHADEMA, lakini alivyoona jina lake limekatwa akahamia CHADEMA, Watanzania wajikumbushe, huyu mtu aliyekuwa CHADEMA mwaka 2015 aliamua kusaliti chama chake ambacho kilikuwa kinaenda kwenye uchaguzi, alisaliti chama chake baada ya kuhongwa, alihongwa akakiasi chama chake.

"Akakaa pale Hoteli ya Serena, baadaye akaondoka akaenda zake Canada na baadaye akapewa Ubalozi. Sasa mtu ambaye hana msimamo, mbinafsi anayeangalia maslahi yake hajawahi kusaidia chochote katika uchumi wa nchi yetu, kazi yake ni kupigapiga tu maneno, ni mtu ambaye kumjibu pia unapata shida, lakini saa nyingine inabidi umjibu.

"Kwa kifupi, hana uadilifu wala uaminifu wa kusema, historia yake inatosha kabisa kuonesha kwamba huyu mtu (Dkt.Slaa), yupo tayari kupandikiza chuki, uhasama kwa ajili ya maslahi yake binafsi kwa Kiswahili kifupi, huyu bwana ni kizabizabina.

"Ni mfitina, mbinafsi na ni mtu yupo tayari kusema chochote, lolote wakati wowote kwa maslahi yake binafsi. Ndugu waandishi, ninadhani huyu ni mtu wa kuogopwa kama ukoma, ningependa kuwasihi Watanzania wenzangu tuangalie historia yake, na ndipo tutakapoamua huyu mtu anatakiwa kusikilizwa au la.

"Hilo ni la Slaa na jambo zima la kunihusisha mimi na DP World au kuniita mimi fisadi. Sasa, fisadi anakuwaje mtu ambaye anafanya biashara na sekta binafsi tu, kwa hiyo ninawafisadi watu wangu wa sekta binafsi watakubali kweli? Sijwahi kumba tenda ya Serikali, sijawahi kuuza hata sindano serikalini, sasa ufisadi unatoka wapi?.

"Baada ya kusema hayo, ninadhani litakuwa ni jibu kamili ya yale ambayo Dkt.Slaa (Padri) aliyoyasema hivi karibuni katika Club House, asanteni sana," amefafanua mfanyabiashara Bilionea Rostarm Aziz mbele ya waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo.

Baada ya maswali...

"Nadhani, ningejibu,ni maswali mazuri sana haya. Kwanza, hili na DP World kama wakija, sisi kama wafanyabiashara binafsi labda tuna mipango ya kufanya nao biashara, mimi ninadhani hilo halikutakiwa kuwa la kuhofiwa, watakuwepo Watanzania wengi ambao watafanyabiashara na DP World, mat-ranspoters,wabeba mizigo, wanaohifadhi makontena, na kadhalika na kadhalika.

"Wengi, kwa mamia au kwa maelfu sasa kama Watanzania ndiyo watapata fursa hizo, kwa nini watu wahofie labda Rostarm na yeye ataomba hiyo fursa, hilo ni la kujibu kiujumla.

"Lakini, ningependa niseme kitu kimoja, mimi katika biashara zangu hamna mahala ambapo ninafanya biashara ambayo inahusiana na masuala ya bandari.

"Sina historia ambayo inaonesha nina Transpots company au nina ICD ya kuweka makontena au sijui nina, hamna sasa hiyo hofu ya kwamba labda, kwani Rostam anayetoka Tabora akiipata fursa na akiona hiyo fursa au baadaye akaona inafaa kuna tatizo gani, kama wanatakavyokuwa Watanzania mamia kwa maelfu baadaye watafaidika kuna tatizo gani.

"Lakini, kwa sasa niseme, sina mpango wowote na sina biashara yoyote ambayo inahusiana na masuala ya bandari, hilo ningependa kukutoa hofu, kwamba kama tatizo la kina Slaa na Rostam atafanya, Rostam ni mfanyabiashara kama hamna biashara Tanzania ataenda kufanya kazi Zambia, ataenda Kenya, ataenda Ulaya ataenda Marekani.

"Hauwezi kumfungia milango, kwamba asifanye biashara, lakini hapa Tanzania biashara mimi pia nina haki kama Mtanzania kufanyabiashara yoyote ambayo ni halali, kama nikiona fursa nikiona inanifaa na nikiweza kupata hiyo fursa kihalali, siwezi kusita, lakini kwa sasa sina mpango wowote na wala sina biashara yoyote ambayo inahusiana na bandari wala sina au na DP World ama na mtu yeyote anayefanya biashara inayofanana na hiyo.

"Hilo ni la kwanza, la pili kwa nini inahusishwahusishwa na haya mambo, ikumbukwe kwamba mimi nimewahi kuwa mwanasiasa, mwanasiasa wa chama tawala (CCM), sasa wakati huo nikiwa mfanyabiashara kwa hiyo, ilikuwa ni rahisi sana watu ambao hawafikiri vizuri sana kuhusisana jina la Rostam na mambo mbalimbali, inakuwa na mvuto fulani wa kuwafanya watu wasikie.

"Wasikilize au waamini, lakini hakuna mtu yeyote amewahi kuthibitisha au kuleta tuhuma mezani au mbele yangu ikathibitishwa, au kama hao watu waliona mimi nimefanya hiki na kile wangeenda mahakamani, kwa sababu tuna mahakama ya kuweza kumshtaki mtu ambaye anafanya kitu ambacho si halali, sasa mbona hawajafanya hivyo?.

"Wamebakia kupigapiga tu maneno, kuropokaropoka tu, lakini mimi ninasema sifanyi biashara na Serikali na ningeweza kufanya biashara na Serikali kama wafanyabiashara wengi nchini, sijafanya hivyo kwa makusudi kabisa kwamba nina uwezo wa kufanya biashara na sekta binafsi na nikasonga mbele.

"Hilo ningependa niliseme kwmaba, kumtaja Rostam inavutia...inavutia, inawafanya watu waamini, inawafanya watu wakubali kile kinachosemwa, lakini hizi ni stori, ni porojo ambazo hazina mashiko. Mimi nina challenges mtu yeyote ambaye anaona nimefanya kitu tofauti aende mahakamani, si ndiyo mahakama ipo, wanabakia porojo tu, tena watu wenyewe kama kina Slaa (Dkt.Slaa) ambaye yeye mwenyewe ana histori chafu kabisa.

"Kanisani katoka kwa utovu wa uadilifu, kaenda Chama cha CCM katoka baada ya kufanya kosa alilolifanya alipokuwa kwenye utumishi wa Mungu, wakamkata jina akahamia chama kingine, baadaye mwaka 2015 akakihama chama chake ambacho alikijenga kwa kupewa vitu vidogo vidogo.

"Na kusaliti na kwenda kupewa mpaka Ubalozi, na ukicheki historia yake kama Balozi hajawahi kuleta ajira hata moja Tanzania, hajawahi kusaidia chochote, hajawahi kuleta uwekezaji kutoka huko alikokuwa miaka minne, sasa hiyo kazi imeisha muda wake anatafuta kazi nyingine.

"Kwa kupitia migongo ya watu, kwa kutukana kina Rostam saasa, Watanzania si wajinga kama mnavyodhani wanaelewa kila kitu, wanasoma na wanaangalia huyu ni mtu gani, uadilifu wake kiasi gnai cha kumpima, mimi ni mfanyabiashara ninaweza kutuhumiwa vitu mbalimbali.

"Na hata nikituhumiwa kuna vitu vingine ninaweza kuwa nimekosea mahala, mimi ni mfanyabiashara, lakini mtu ambaye ni padri ambaye anajifanya yeye ni kiongozi wa kutetea Watanzania halafu yeye mwenyewe anakosa uadilifu na uaminifu, sasa huyo ndiye mwenye problem (tatizo), siyo mimi, mimi ninaendelea na biashara zangu.

"Nitafanya kiasi ninachoweza kuendesha biashara zangu kihalali, kwa kuhakikisha kwamba nipo ndani ya sheria hapa na nje ya nchi, leo mtu ukiwa na tuhuma za namna hiyo hata benki haiwezi kukuamini kukupa pesa, sasa ningewezaje kuendesha biashara zote hizi kama mimi ningekuwa ni mtu ambaye hizi tuhuma ni za kweli?.

"Nisingeweza kufanya biashara, mimi ninafanya biashara na benki za hapa, ninafanya biashara na benki za nje zinaniamini, ndiyo maani ninaweza kukuza biashara zangu Magufuli ( Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Dkt.John Pombe Joseph Magufuli) asingweza kuja kufungua ule mtambo wangu wa gesi angejua mimi si mfanyabiashara halali.

"Asingekuja kufungua kiwanda cha Morogoro ningekuwa mimi si mfanyabiashara halali, kwa hiyo lazima tuangalie kwamba kuna porojo, na kuna ukweli, lazima tuweze kutofautisha pumba na mchele, sasa nadhani hilo limeeleweka,"amesisitiza mfanyabiashara Bilionea Rostam Aziz.

DP World

"Juzi katika mdahalo pale hoteli ya Serena nilisema kuwa sihusiki na hili jambo (mkataba wa bandari) kibiashara. Ningekuwa nahusika nisingekuwa jasiri wa kuyasema yale niliyoyasema katika mdahalo ule.

"Unapohusika na jambo huwezi kulijadili, na pia huwezi kuwa na uwezo au neutrality (hali ya kutofungamana na upande wowote) ya kuzungumzia jambo lenyewe, hivyo ningekaa pembeni na kuacha wengine wajadili.

"Mimi kama Rostam na kampuni zangu hatuhusiki na uwekezaji au utakaokuwa uwekezaji wa kampuni ya DP World,"amebainisha Rostam Aziz.

Uwekezaji Zambia

Katika hatua nyingine, Kampuni ya Taifa Gas ya Tanzania imetangaza uwekezaji mkubwa nchini Zambia wa uzalishaji umeme kwa kutumia gesi itokanayo na mafuta (LPG).

Taifa Gas itashirikiana na Kampuni ya wazawa ya Delta Marimba Limited kuzalisha megawati 100 za umeme ambao utaingizwa kwenye gridi ya Taifa nchini Zambia.

Makubaliano hayo yametangazwa na pande hizo mbili leo jijini Dar es Salaam ambapo Mkurugenzi wa Kampuni ya Taifa Gas, Hamis Ramadhan amesema, kampuni hiyo itakua ya kwanza ya uzalishaji wa umeme kwa kutumia gesi ya LPG na mradi huyo utatekelezwa nchini Zambia.

Pia,Ramadhan amesema Taifa Gas itatazama fursa nyingine za biashara ya gesi ikiwemo matumizi ya kupikia biashara amabyo tayari inafanywa hapa nchini.

“Taifa Gas itaongoza uwekezaji kwenye mradi huu nchini Zambia ambao utafikia dola za Marekani milioni 100. Uamuzi huu wa kuwekeza Zambia umechochewa na mazingira mazuri ya uwekezaji na sera madhubuti za Rais Hakainde Hichilema na chama chake cha UPND,”amesema.

Naye Mwenyekiti wa Taifa Gas, Rostam Azizi amesema, Tanzania na Zambia zimekuwa na uhusiano wa muda mrefu huku akisisitiza kuwa, “na uhusiano huu unapaswa kuuendeleza kwenye shughuli za kiuchumi.

“Zambia ni nchi ambayo kwa sisi Watanzania tumekuwa na historia nao wakati wa shida na raha na mambo yanapokwenda vizuri kwenye uchumi maana yake tunapaswa kutafasiri mahusiano ya nchi mbili hizi kwa kuangalia fursa,”amesema Rostam.

Pia, Rostam amesema kampuni zake zitaendelea kutafuta fursa maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi. Kwa upande wake,Padmore Muleya ambaye ni mwakilishi wa kampuni ya Delta amesema, mradi huo unatarajiwa kumakilika ndani ya miezi 24 kuanzia sasa huku akieleza umuhimu wa uwekezaji huo kwa maendeleo ya wana Zambia.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news