JUKATA:Serikali iache kutoa elimu Katiba ya mwaka 1977

DAR ES SALAAM-Jukwaa la Katiba Tanzania (JUKATA) wameishauri Serikali kuachana na mpango wa kutoa elimu ya Katiba ya mwaka 1977 kwa miaka mitatu kama ilivyoseema aliyekuwa Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt.Damas Ndumbaro na badala yake kupeleka miswada ya sheria za mchakato wa Katiba bungeni kwa ajili ya marekebisho.
Ushauri huo umetolewa jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa JUKATA,Bob Chacha Wangwe wakati akizungumza na Waandishi wa habari juu ya kauli hiyo ya serikali iliyotolewa kupitia aliyekuwa Waziri wa Sheria na Katiba juu ya msimamo wa serikali kuhusu mchakato huo.

“Ni kweli ufufuaji wa mchakato wa katiba unahitaji uwepo wa Sheria zinazoendana na wakati na mahitaji ya sasa, JUKATA baada ya maandalizi ya muda mrefu ya kuandaa sheria mfano kwa ajili ya mchakato wa katiba mpya ambapo Wadau mbalimbali muhimu kutoka kada na maeneo tofauti tofauti wakiwemo wanasisasa, wanahabari, wanazuoni,”alisema Bw.Wangwe.

Alisema, Viongozi wa Dini, Asasi za kiraia, Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria, Time za marekebisho ya sheria kutoka pande zote za Muungano

Alisema, walishiriki kwa namna moja ama nyingine katika ukamilishaji wa sheria hizo akitolea mfano sheria ambazo zinalenga kuwasaidia watunga sheria katika kupata sheria zitakazokidhi mahitaji ya sasa.

Hivyo amesema, JUKATA tayali imetangaza kutoa sheria mbili za mfano ambazo ni sheria mfano ya marekebisho ya Katiba na Sheria mfano ya kura ya maoni pamoja na nyaraka mbili zinazotoa ufafanuzi juu ya sifa za upatikanaji wa kamati ya wataalam pamoja na namna bora ya usimamizi na utatuzi wa migogoro inayoweza kutokea katika hatua za mchakato wa Katiba mpya.

“Sheria mfano ya Mchakato wa Katiba imetoa hatua za mchakato, upatikanaji wa kamati ya wataalam, majukumu na kadhalika,” amebainisha Wangwe na kuongeza,

“Pia imeainisha namna migogoro inayoweza kutatuliwa na kusimamiwa katikati ya Mchakato, imependekeza masuala ya kibajeti na vitu gani vinaweza kufanyika katika hatua za mpito wa nchi kupata katiba mpya.”

Bob Wangwe ametumia fursa hiyo kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kumuondoa Dkt. Ndumbaro kwenye Wizara ya Katiba na Sheria kwani wanaamini aliona haja ya kutafuta mtu mwingine kwa ajili ya kumsaidia kupitia Wizara hiyo.

Kadhalika amempongeza Balozi Dkt. Pindi Chana kuwa Waziri wa Katiba na Sheria ambapo wameahidi kumpa ushirikiano lakini pia kumtakia kola lakheri katika majukumu mapya.

Ameongeza kwamba, JUKATA bado wanaamini hatua iliyotangazwa na Wizara ya Katiba na Sheria hivi karibuni ya kutoa elimu ya Katiba kwa miaka mitatu ni hatua ambayo inapaswa kuangaliwa upya kwani wanaamini ni ucheleweshaji wa kuanzisha mchakato wa Katiba na kutumia vibaya Fedha za Watanzania kwani hatua hiyo tayari ilishafanyika na iliyokuwa Tume ya marekebisho ya Katiba.

Hivyo amesema ujio wa Balozi Dkt. Pindi Chana katika Wizara ya Katiba na Sheria, wanaamini utaleta nuru ya upatikanaji wa Katiba na kuondoa vikwazo ambavyo kwa namna moja au nyingine vinaweza kukwamisha kama hilo la kutoa elimu ya Katiba ya 1977 kwa miaka mitatu litatekelezwa.

Bob Wangwe ametoa wito kwa Serikali kuona umuhimu wa kutumia nyaraka hizi muhimu za mchakato wa Katiba kwani zimezingatia mahitaji ya sasa ya nchi pamoja na uzoefu wa mchakato uliokwama Mwaka 2014.

Ametoa wito kwa Waziri Balozi Pindi Chana kutoa ratiba ya hatua za mchakato wa Katiba mpya ili kuondoa sintofahamu ambayo imetawala miongoni mwa Wadau wa Katiba na Watanzania la ujumla.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news