Ujumbe wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) watembelea Ujerumani

BERLIN-Ujerumani ni miongoni mwa mataifa yaliyopiga hatua kubwa katika maendeleo hasa kwenye sekta ya elimu hususani matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika ufundishaji na ujifunzaji.
Jambo hili limekipa msukumo Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) kutuma ujumbe wa wanataaluma wake kwenda kufanya ziara ya kukitembelea kituo cha ufundishaji na ujifunzaji katika chuo Kikuu cha Bremen nchini Ujerumani kuona namna wenzetu wanaweza kutumia teknolojia kwa ufanisi katika swala zima la kujifunza na ufundishaji.

Kiongozi wa ujumbe huo, Prof. Alex Makulilo, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania anayeshughulikia Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalamu akiwa katika ziara hiyo kwenye Chuo Kikuu cha Bremen amesema ziara hii imekuwa ni ya muhimu sana hasa ukizingatia ukuaji wa matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na kujifunza kwa wenzetu.
"Tumekuja kujifunza namna wenzetu wanavyotoa mafunzo kupitia mifumo ya TEHAMA, tumetembelea kituo cha ufundishaji na ujifunzaji mtandao (E-Learning centre) pamoja na kituo cha kutathimini wanafunzi kupitia mtandao (E-assessment centre) katika Chuo hiki mashuhuri na maarufu duniani cha Bremen. 

"OUT ni wadau muhimu katika kutumia mifumo hii kwa ufundishaji na ujifunzaji wa wanafunzi wetu, tunaamini tunayojifunza hapa yatatusaidia kuimarisha zaidi mifumo yetu na kuendelea kutoa elimu bora kwa wanafunzi wetu," amesema Prof. Makulilo.
Ameongeza kuwa, ziara hii ni zao za ushirikiano uliopo baina ya OUT na Chuo Kikuu cha Bremen, kupitia mashirikiano hayo taasisi hizi mbili hubadilishana uzoefu na kuimarishana zaidi katika maeneo ya ufundishaji, ujifunzaji, utafiti na Ushauri wa Kitaalamu kwa jamii zao. Eneo la kuwafanyia tathimini wanafunzi kupitia mifumo ya TEHAMA ni eneo nyeti ambalo linahitaji umakini mkubwa na OUT tumekuwa tukijifunza kupitia wenzetu ili nasi tuendelee kubuni mifumo bora zaidi katika eneo hili.

Wanataaluma wengine walioambatana katika ziara hiyo ni pamoja na Prof. Matobola Mihale ambaye ni Mtiva wa Kitivo cha Sayansi, Teknolojia na Taaluma za Mazingira, Dkt. Harrieth Mtae Mkurugenzi wa Utafiti, machapisho na ubunifu, Dkt. Thimoth Lyanga mratibu msaidizi wa mradi wa HEET wa OUT na Dkt. Halima Kilungu ambaye ni Mkuu wa Idara ya Jografia, Utalii na Ukarimu ya OUT ambao kwa pamoja wanakiri kwamba ziara hii ni muhimu sana katika kupata uzoefu wa wenzetu katika matumizi ya TEHAMA katika kutoa elimu.
Akizungumza kwa niaba ya wajumbe wengine Dkt. Harrieth Mtae anasema ni jambo la kuishukuru Menejimenti ya OUT kuwezesha ziara hiyo katika Chuo Kikuu cha Bremen nchini Ujerumani kwani wenzetu wamepiga hatua kubwa kwenye mambo mbalimbali ikiwemo matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji.

“Tumechota mengi ambayo tutayatumia kujiimarisha zaidi kutoa taaluma bora kwa wanafunzi kupitia kuimarisha mitaala, kuandaa zana za kufundishia na kujifunzia na kufanya tafiti kwa manufaa ya nchi yetu," amesema Dkt. Mtae.
Ujumbe huo wa OUT umeanza ziara hiyo ya kikazi Mei 6, 2024 na inatarajiwa kukamilika Mei 11, 2024 na itaongeza chachu ya mashirikiano baina ya OUT na Bremen kwa manufaa ya taasisi zote mbili na pia ziara hii ikiwa ni sehemu ya mradi wa HEET wajumbe wamejifunza mengi ikiwemo Umataifashaji wa elimu ya juu, utafiti, ubunifu na uanzishaji wa miradi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news