DODOMA-Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imetoa mafunzo kuhusu majukumu yake kwa wanafunzi zaidi ya 80 wa Shule ya Msingi Prince Junior kutoka Wilaya ya Chamwino, mkoani Dodoma. Mafunzo hayo yalifanyika tarehe 9 Aprili 2025, wakati wa ziara ya wanafunzi hao katika makao makuu ya BoT jijini Dodoma.

Mafunzo hayo yaliendeshwa na Mchumi kutoka Tawi la BoT Dodoma, Bi. Regina Mwaipopo, pamoja na Afisa Mwandamizi wa Benki hiyo, Bw. Atufigwege Mwakabalula.
Akizungumza baada ya mafunzo, Mratibu wa ziara hiyo, Bw. Sadam Nyika, aliishukuru BoT kwa kutoa fursa hiyo adhimu kwa wanafunzi, akisema kuwa kupitia ziara hiyo wamejifunza masuala muhimu ya kiuchumi na kuitambua Benki Kuu kama taasisi nyeti katika ustawi wa nchi, huku akiipongeza BoT kwa kuweka utaratibu rafiki wa elimu kwa vitendo.
Ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za BoT katika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu majukumu ya Benki Kuu na mchango wake katika kukuza uchumi wa nchi.