ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Dkt.Hussein Ali Mwinyi amesema,Serikali inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kuimarisha Sekta ya Utalii Ili kuwa Endelevu na kuifanya Zanzibar kuwa Kituo Muhimu cha Utalii kinachotambulika na kuvutia Ulimwenguni.

Amefahamisha kuwa, Utalii ni Sekta Muhimu na nguzo ya Uchumi wa Zanzibar ambayo mbali na kukuza uchumi, sekta hiyo inawaunganisha watu wa mataifa mbalimbali Ulimwenguni.
Dkt.Mwinyi amesema, Serikali imechukua juhudi kubwa za Uimarishaji wa Viwanja vya Ndege kwa lengo la kutoa huduma bora kwa watalii,upanuzi wa miundonbinu ya barabara pamoja na huduma za afya,umeme na upatikanaji wa maji ni hatua muhimu za kufanikisha kuwa na Utalii unaovutia na endelevu.
Amesema, ufunguzi wa Terminal 3 na ujenzi wa kilomita 800 za barabarra nchini kote kulilenga kuyaunganisha maeneo ya utalii ili kufikiwa na watalii wengi zaidi kwa urahisi.
Amebainisha kuwa, kuchukua hatua hizo nchi imekuwa ikipokea idadi kubwa ya watalii kila mwaka wanaofikia takribani milioni mbili na kuiunganisha Zanzibar na mashirika ya Kimataifa ya Ndege 34 yanayoleta watalii hapa nchini
Aidha, Dkt.Mwinyi amesema, Zanzibar ni miongoni mwa nchi za awali iliyofanikiwa kukabiliana kwa haraka na changamoto za Ugonjwa wa Covid19, hatua iliochangia kuaminika na kuchochea ongezeko la idadi ya watalii.
Rais Dkt.Mwinyi ameielezea, Filamu ya Royal Tour ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan na ziara yake kuwa ni nyenzo muhimu zilivyovitangaza vivutio vya Utalii wa Tanzania kwa mafanikio Ulimwenguni.
Akitoa takwimu za watalii walioitembelea Zanzibar amefahamisha kuwa, kabla ya Ugonjwa wa Covid 19 mwaka 2019, Zanzibar ilipokea Watalii 538,264 hatimaye Idadi Hiyo kushuka hadi kufikia 260,644 wakati wa Maambukizi ya Covid19.
Hata hivyo amesema,Mikakati ya Uwekezaji imewezesha kupokea watalii 548,503 Mwaka 2022 na Mwaka 2023 imepokea Wageni 736,755 na kutunukiwa Tuzo ya World Travel Award kwa kuwa kituo kinachoongoza kwa Matamasha na Mikusanyiko ya Kimataifa.

Rais Dkt.Mwinyi amesema,Sekta Binafsi ina mchango mkubwa katika kukuza Sekta ya Utalii hapa nchini katika nyanja tofauti na kusisitiza Serikali kuendelea kushirikiana na sekta binafsi Ili kuwa na Utalii Endelevu.
Mabalozi wa mataifa takribani 34 wanaoziwakilisha nchi zao Tanzania walikuwa na Ziara Maalum ya kuvitembelea Vivutio vya Utalii Ngorongoro jijini Arusha na Zanzibar ili hatimaye kuvitangaza katika nchi zao.
Ziara hiyo imeandaliwa na Wizara ya Utalii na Mali Asili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.