DAR-Mkurugenzi wa Uendeshaji na Biashara wa vituo vya habari vya EFM na TVE, Denis Busulwa maarufu kwa jina la Ssebo, amefariki dunia usiku wa kuamkia leo akiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili alikokuwa akipatiwa matibabu.
Taarifa za kifo chake zimethibitishwa na Mkurugenzi Mkuu wa EFM na TVE, Francis Ciza maarufu kama Majizzo, kupitia ujumbe aliouchapisha kwenye mitandao ya kijamii.
Katika ujumbe huo, Majizzo amesema kwa masikitiko makubwa amepokea taarifa za kifo cha Busulwa ambaye alikuwa rafiki, ndugu na mfanyakazi mwenzake wa karibu katika taasisi hiyo ya vyombo vya habari.
“Kwa moyo mzito na machozi mengi, nasikitika kutangaza kifo cha rafiki, kaka na mfanyakazi mwenzangu aliyeitumikia EFM na TVE kwa nguvu zake zote, ndugu yangu Ssebo,” ameandika Majizzo.
Ameeleza kuwa Busulwa amefariki dunia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, huku akibainisha kuwa familia pamoja na uongozi wa EFM na TVE wanaendelea na maandalizi ya taratibu za msiba.
Amesema, taarifa zaidi kuhusu msiba huo, ikiwemo ratiba ya mazishi, zitatolewa baadaye mara baada ya mipango ya awali kukamilika.
