ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt.Hussein Ali Mwinyi amesema, Serikali kupitia Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana itaendelea kuimarisha huduma za Hijja na kushughulikia changamoto zinazowakabili mahujaji.
Akizungumza leo Mei 3,2026 katika hafla ya kuwaaga mahujaji wanaokwenda Makkah, Saudi Arabia, iliyofanyika Msikiti wa Jamiu Zinjibar, Kiembe Samaki, Mkoa wa Mjini Magharibi.
Aidha,Rais Dkt.Mwinyi amesisitiza umuhimu wa ibada ya Hijja kama Nguzo ya Tano ya Uislamu na kuwataka mahujaji kudumisha nidhamu na mwenendo mwema.
Amesema,Zanzibar imeendelea kupata mafanikio katika usimamizi wa Hijja kila mwaka, hali inayochangia kuongezeka kwa idadi ya mahujaji.
Halikadhalika, ameishukuru Serikali ya Saudi Arabia, taasisi zinazohudumia Hijja, Shirika la Ndege la Saudi Arabia pamoja na Ubalozi wa Tanzania kwa mchango wao katika kuhakikisha huduma bora kwa mahujaji wa Zanzibar.
Rais Dkt. Mwinyi ameongeza kuwa Serikali inaendelea kukamilisha hatua za kisheria kuimarisha Mfuko wa Hijja wa Zanzibar ili kuongeza fursa kwa wananchi wengi zaidi kushiriki ibada hiyo.

















