NA DIRAMAKINI
UONGOZI wa Klabu ya Young Africans Sports Club (Yanga) umetangaza rasmi kusitisha ajira ya Kocha Mkuu wa kikosi cha kwanza,Pedro Gonçalves kuanzia leo.
Taarifa iliyotolewa na Mtendaji Mkuu wa klabu hiyo imeeleza kuwa, uamuzi huo umefikiwa na uongozi wa juu wa klabu, ingawa haukuweka bayana sababu mahsusi zilizopelekea hatua hiyo.Hata hivyo, klabu imesisitiza kuthamini mchango wa kocha huyo katika kipindi chake cha uongozi.
“Uongozi wa klabu unamshukuru Kocha Pedro Gonçalves kwa mchango wake alioutoa ndani ya klabu yetu, na unamtakia kila la kheri katika majukumu yake yajayo,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Kufuatia mabadiliko hayo ya benchi la ufundi, Yanga imetangaza kuwa kikosi chake kitaendelea kuongozwa na makocha wasaidizi, Abdihamid Moalin na Patrick Mabedi ambao watasimamia timu hiyo hadi mwisho wa msimu wa mashindano unaoendelea.
Hatua hiyo inakuja katika kipindi ambacho klabu hiyo kongwe nchini inaendelea kushiriki mashindano mbalimbali ya ndani na kimataifa, hali inayoweka shinikizo kwa benchi jipya la ufundi kuhakikisha linaendeleza ushindani na mafanikio ya timu.
Wadau wa soka nchini sasa wanasubiri kuona athari za mabadiliko hayo katika mwenendo wa timu hiyo, hususan katika hatua za mwisho za msimu ambapo ushindani unazidi kupamba moto.