NA DIRAMAKINI
WIZARA ya Fedha imewataarifu wastaafu wote waliopo kwenye Daftari la Pensheni na wanaolipwa pensheni ya kila mwezi na Wizara ya Fedha (HAZINA) kuwa,itaanza rasmi kugawa vitambulisho vipya vya wastaafu katika mikoa yote ya Tanzania Bara na Zanzibar.
Ni kuanzia tarehe 15 Juni 2026 hadi 30 Juni 2026, saa 3:00 asubuhi hadi saa 11:30 jioni (kuanzia siku ya Jumatatu hadi Ijumaa).
Hayo ni kwa mujibu wa tangazo ambalo limetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kupitia Wizara ya Fedha.
Ili kupata kitambulisho hicho kipya, mstaafu anatakiwa kufika katika Ofisi za Hazina Ndogo katika mikoa yote ya Tanzania Bara; Ofisi za Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar (Unguja na Pemba) akiwa na Kitambulisho cha zamani cha Mstaafu au Kitambulisho cha Taifa (NIDA).
"Aidha,tangazo hili haliwahusu wastaafu wanaolipwa pensheni na Ofisi ya Msajili wa Hazina pamoja na wale wanaolipwa na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.Wastaafu wote wanaarifiwa kuwa hakuna gharama yoyote ya kulipia huduma hii,ni bure kabisa."
