DCEA yabaini vinywaji vya Energy vyenye dawa za kulevya Dar

NA GODFREY NNKO

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imebaini uwepo wa vinywaji vya kuongeza nguvu mwilini (energy drinks) vyenye kemikali ya Tetrahydrocannabinol (THC) inayopatikana kwenye dawa za kulevya aina ya bangi, baada ya kufanya operesheni maalumu ya ukaguzi katika duka la Village Supermarket jijini Dar es Salaam.
Kamishina Jenerali wa DCEA, Aretas Lyimo ameyabainisha hayo leo Julai 2,2026, jijini Dar es Salaam alipokuwa akitoa taarifa ya operesheni za kudhibiti dawa za kulevya zilizotekelezwa nchini katika kipindi cha Mei na Juni,mwaka huu.

Amesema ugunduzi huo ulifanyika kupitia operesheni ya pamoja iliyoshirikisha Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), ambapo uchunguzi wa bidhaa mbalimbali ulifanyika katika duka la Village Supermarket.

Kamishna Jenerali Lyimo amesema,katika ukaguzi huo wamebaini uwepo wa vinywaji hususan energy drinks vyenye viambata vya kemikali ya THC, ambayo hupatikana kwenye dawa za kulevya aina ya bangi.

Ameeleza kuwa, katika operesheni hiyo, makopo 122 ya kinywaji chenye chapa ya TRIP, kila moja likiwa na ujazo wa mililita 250 sawa na lita 30.5 yalikamatwa.
Kwa mujibu wa DCEA, watuhumiwa wawili walikamatwa kuhusiana na bidhaa hizo ambao ni Syed Abdul Bast (43) raia wa Pakistan na Dhirendra Kumar Gorodhan (45), Mtanzania mwenye asili ya Asia.

Amesema,THC ni kemikali inayopatikana kwenye bangi na matumizi yake yanaweza kusababisha madhara mbalimbali kwa afya ya binadamu, ikiwemo kuamsha magonjwa ya akili, kuathiri utendaji wa mfumo wa fahamu, pamoja na kuongeza uwezekano wa kujihusisha na vitendo vya uhalifu kama vile wizi, unyang'anyi na ukatili.

Pia,amesema kemikali hiyo inaweza kuchochea matumizi ya aina nyingine za dawa za kulevya na kuhatarisha usalama wa jamii.

Kutokana na ugunduzi huo, DCEA imetangaza kuanzisha operesheni ya ukaguzi wa bidhaa katika maduka mbalimbali nchini kwa kushirikiana na mamlaka za udhibiti ili kuhakikisha bidhaa zinazouzwa kwa watumiaji hazina viambata vya dawa za kulevya.

Amesema,wataendelea kufanya ukaguzi wa kina katika maduka mbalimbali ili kuhakikisha bidhaa zote zinazouzwa nchini ni salama kwa matumizi ya wananchi na hazina viashiria vya dawa za kulevya.
Akijibu swali la waandishi wa habari kuhusu asili ya bidhaa hizo, Kamishina Jenerali Lyimo amesema,vinywaji hivyo vilitengenezwa nje ya Tanzania na kuingizwa nchini kinyemela.

Amefafanua kuwa,nyaraka za bidhaa hizo hazikuonesha uwepo wa kemikali ya THC, jambo ambalo linaashiria kuwa taarifa muhimu kuhusu muundo wa bidhaa hizo zilifichwa ili kukwepa mifumo ya udhibiti.

Vilevile,Kamishina Jenerali Lyimo amewataka wafanyabiashara kuzingatia sheria za uingizaji na usambazaji wa bidhaa nchini, huku akiwahimiza wananchi kuwa waangalifu wanaponunua bidhaa mbalimbali na kutoa taarifa kwa mamlaka husika wanapobaini bidhaa zenye viashiria vya kuhatarisha afya au usalama wa jamii.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Know matter how large or small your business is, advertising here