DAR-Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania BoT, Dk. Rahma Salim Mahfoudh, ametembelea banda la Bodi ya Bima ya Amana (DIB) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya ya Dar es Salaam yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa.
Katika ziara hiyo, Dkt. Mahfoudh alipokelewa na viongozi pamoja na wafanyakazi wa DIB na kupatiwa maelezo kuhusu majukumu ya DIB, huduma inazotoa, na jitihada zinazoendelea kufanywa katika kutoa elimu kwa umma kuhusu Mfumo wa Bima ya Amana.
Aidha, Naibu Gavana alipata fursa ya kufahamu mchango wa Bodi ya Bima ya Amana katika kulinda amana za wateja wa benki na taasisi za fedha, pamoja na kuimarisha uthabiti wa sekta ya fedha nchini.
Akizungumza baada ya kutembelea banda hilo, Dkt. Mahfoudh aliwahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kutembelea Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam ili kujifunza kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi za umma, kampuni binafsi na wafanyabiashara wanaoshiriki katika maonesho hayo ikiwemo DIB.
Alieleza kuwa,maonesho hayo ni jukwaa muhimu linalowawezesha wananchi kupata elimu, kuona bidhaa na ubunifu mbalimbali, pamoja na kujionea teknolojia mpya zinazotumika kuboresha utoaji wa huduma na kuchochea maendeleo ya uchumi wa nchi.
"Ninawahimiza wananchi kutumia fursa hii kutembelea maonesho haya ili kujifunza mambo mbalimbali kutoka kwa taasisi na kampuni zinazoshiriki. Hapa kuna huduma, bidhaa, ubunifu na teknolojia zinazoweza kuongeza uelewa wao na kuwasaidia kufanya maamuzi sahihi katika shughuli zao za kila siku," alisema Dk. Mahfoudh.
Kwa upande wake Bi. Joyce Shala ambaye ni Afisa Mwandamizi wa DIB ameeleza kuwa, ushiriki wa Bodi ya Bima ya Amana katika Maonesho ya Sabasaba 2026 unalenga kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu majukumu ya Bodi katika kulinda amana za wateja wa benki na taasisi za fedha, pamoja na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa mfumo wa Bima ya Amana katika kudumisha utulivu na kuimarisha imani katika sekta ya fedha.
Aidha, Bi Shala amewakaribisha wananchi wote kutembelea banda la Bodi ya Bima ya Amana katika Maonesho hayo ili kupata elimu kuhusu mfumo wa Bima ya Amana, kufahamu huduma zinazotolewa na Bodi, na kujionea mchango wake katika kulinda amana za wateja na kuimarisha uthabiti wa sekta ya fedha nchini.


