Mgombea Urais Dkt.John Magufuli awaacha nyuma wenzake,mambo yanayomg'arisha ni haya

Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Rais Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na wananchi wa Iringa Mjini katika mkutano wa kampeni wa CCM uliofanyika leo Septemba 28, 2020 katika Uwanja wa CCM Samora mjini humo.

Mwanga wa mafanikio kwa Iringa mpya umeanza kuangaza, ni baada ya Septemba 28, 2020 katika Uwanja wa CCM Samora mkoani Iringa, wana Iringa wenyewe kumuonyesha Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.John Pombe Joseph Magufuli kuwa, wapo tayari kwa mabadiliko, anaripoti Mwandishi Diramakini.

Mabadiliko hayo wamekiri mbele ya mkuu huyo wa nchi kuwa, ndiyo yatakayowawezesha kuifanya Iringa kuwa mpya ikiwa ni baada ya Jimbo la Iringa Mjini kuwa chini ya upinzani kwa muda mrefu.
 
"Ndugu zangu wana Iringa, naomba mtuamini kwamba tunataka kuibadilisha Iringa,mambo yaliyofanyika Iringa ni mengi sana naomba msituangushe watu wa Iringa. Katika sura ya pili ya Ilani ya Uchaguzi Ukurasa wa tisa hadi 124 imeelezwa kwamba tutaendeleza juhudi za kuleta mapinduzi ya kiuchumi ya maendeleo ya watu ikiwemo wafanyakazi, wakulima,wafugaji,wavuvi,wasanii na madereva na ili kutimiza azima hiyo wamejiwekea malengo na kutaja mipango na mikakati ya utekelezaji;

Dkt.Magufuli ameyasema hayo mbele ya umati wa maelfu kwa maelfu ya wananchi waliofurika ndani na nje ya Uwanja wa CCM Samora wakati akinadi sera na ilani ya Uchaguzi ya chama hicho.
Diramakini imebaini moja wapo ya kitu kinachozidi kumpa ushindi hata kabla ya Uchaguzi Mkuu, Dkt.John Magufuli ni pamoja na kujikita katika kunadi Sera na kuifafanua Ilani ya chama namna ambavyo wamejipanga kuja kuitekeleza.

Huo ni ushaidi tosha kwamba, kwa wananchi ambao wanakusanyika katika mikutano ya kampeni wanatamani kufahamu kwa kina ni mambo gani wagombea iwapo watapata ridhaa watakuja kuwatendea, wakati Dkt.Magufuli akitekeleza hilo kwa umakini mkubwa, baadhi ya wagombea wengine wameendelea kutumia muda mwingi kufanya mashambulizi binafsi kati ya mtu na mtu ama taasisi, jambo ambalo limekuwa likichukua muda mwingi na pengine kuwafanya wananchi ambao wanataka kujua jambo kutoka kwao kujikuta wanachoka na kuondoka katika mikutano.

Tuyaache hayo, tuendelee na Dkt.Magufuli ambaye leo Septemba 28, 2020 ametimiza mikoa 11 katika kampeni zake ambazo zimejikita kuwaelezea wananchi waliyokusudia kuja kuwafanyia tena iwapo watawapa ridhaa kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.

Dkt.Magufuli amesema, yeye ni Rais wa Watanzania, wala haoni shida kwa mtu yeyote ambaye atakuwa anambeza kwa sababu ya kutosafiri kwenda nje ya nchi, kwani kuwafikia Watanzania tena wanyonge ndiyo faraja yake.

“Mimi lazima niwe mtumishi wa wanyonge,mtumishi wa watu na ndio maana siku zote nimekuwa barabarani kutatua kero za wananchi,”amesema Dkt.Magufuli.

Dkt.Magufuli amesema, Ilani ya Uchaguzi 2020-2025, imezungumzia kwa kina juu ya namna ya kuendeleza juhudi za kujenga taifa linalojitegemea kiuchumi kwa kutumia rasilimali mbalimbali zilizopo hapa nchini.

Amesema, rasilimali hizo nii pamoja na watu ,ardhi,madini,gesi asilia,misitu,wanyama,kutoka majini,bahari na nyinginezo nyingi. Dkt.Magufuli amebainisha, kutokana na uongozi imara watahakikisha rasilimali hizo zinazidi kuwa baraka kwa Watanzania wote ikiwemo kunufaisha kizazi cha sasa na kijacho.

“Ndugu zangu, siku zote nazungumza Tanzania ni tajiri na ina mambo mengi na haya yote yapo katika ilani yetu ya chama sura ya kwanza na ya pili,”amesema Dkt.Magufuli huku akiongeza kuwa, ilani yao imeeleza mipango na mikakati iliyopangwa kutekelezwa ndani ya miaka mitano ijayo kwa manufaa ya Taifa na Watanzania wote.
Amesema, iwapo Watanzania watawapa ridhaa katika miaka mitano ijayo watahakikisha wanakuza uchumi kwa wastani usiopungua asilimia nane. “Miaka mitano iliyopita tumetoka katika nchi masikini za kutupwa na kuingia katika uchumi wa kati,na tumeingia katika uchumi wa kati wakati Dunia nzima 'imejilock down' watu hawafanyi kazi wamejifungia majumbani,wamefunika pua na midomo.

“Hii ilani ndio mkataba wa Serikali itakayoingia madarakani na wananchi,ambapo pia tunatakiwa kutengeneza ajira milioni nane ambapo miaka mitano iliyopita ajira zilizotengenezwa zilikuwa milioni sita,”amefafanua Mgombea Urais huyo.

Dkt.Magufuli amesema, ajira hizo zimetokana na kuwepo zahanati 1198,Vituo vya afya 487,ununuaji wa ndege 11 ambapo nane zimefika tayari,ukarabati wa barabara zaidi ya kilomita 300,utengenezaji wa reli ya kisasa ya umeme zaidi ya ajira 10,000, Bwawa la Mwalimu Nyerere zaidi ya ajira 10,000 zimetengenezwa ambapo wapo wanaojenga,wanaouza vyakula,wanaofanya kazi na wakandarasi pamoja na watumishi mbalimbali wa maeneo hayo.

“Tunataka kipindi cha miaka mitano mingine tutengeneze ajira zaidi ya milioni nane na huo ndio uchumi wa kati kuliko uchumi wa mwanzo wa kimasikini,ili kufikia malengo haya tutaboresha mazingira ya uchumi na biashara kwa kuendelea kufanya mageuzi katika sheria na kanuni,Kodi,tozo na utendaji wa sekta ya umma kwa kuzingatia muongozo wa uboreshaji wa mazingira nchini,”amesema.
 
Dkt.Magufuli amesema, pia wataimarisha usimamizi wa sekta ya fedha na kuanzisha makundi maalum kujiunga kwenye kampuni ili kuwapatia mafunzo ya elimu ya ujasiriamali itakayowezesha kujiajiri au kuajirika.

Amesema, Ilani ya chama chao ya uchaguzi inaeleza misingi au nguzo muhimu za Serikali ya CCM, endapo itachaguliwa itaendelea kusimamia ikiwemo kulinda uhuru wa nchi,kudumisha amani,umoja,mshikamano na Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Muungano.

Amesema, uchaguzi huu ni muhimu kuendelea na mageuzi ya sasa na kupata viongozi watakaobeba maendeleo ya nchi huku akiwasisitiza kuwa, Chama Cha Mapinduzi (CCM) ndio chama kinachoweza kuleta maendeleo kwa kasi kubwa.

Wakati huo huo amesema, miaka mitano ijayo Serikali inatarajia kufanya mageuzi makubwa ya kiuchumi mkoani Iringa ambayo yatakuwa ni mwendelezo wa yale yaliyofanyika awali.

Miongoni mwa mafanikio ya awali ni pamoja na upanuzi wa chumba cha wagonjwa mahututi,kujenga jengo la wagonjwa wa dharura katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa,Upanuzi wa Hospitali ya Wilaya Manispaa ya Iringa na kujernga hospitaliu tatu mpya. Pia amesema wamefanya upanuzi wa vituo vya afya vitano ambapo viwili vinaendelea kujengwa na zahanati 23.

“Tumeleta kiasi cha shilingi Bilioni 33.74 katika elimu kwa ajili ya elimu bila malipo kwa watoto hapa Iringa, upanuzi Chuo Kikuu Mkwawa,kukarabati Chuo cha Walimu,Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Ilula na Shule ya Ufundi Ifunda,Tosamanganga, pia tumejenga mabweni,madarasa na vyuo vya ufundi,kwa upande wa maji Serikali imetekeleza miradi ya maji 43 yenye thamani ya sh.bilioni 20.3 na miradi 79 inaendelea kwa gharama ya sh.bilioni 22.94,”amesema. 

Mbali na hayo amesema,upatikanaji wa maji vijijini katika Mkoa wa Iringa umefikia asilimia 72 kutoka asilimia 60 hadi 66,kuhusu umeme wamefikisha umeme katika vijiji 242 ambapo vijiji 37 ndio vilivyobaki katika kuwashwa umeme na vinatarajiwa kupata nishati hiyo mapema.

Dkt.Magufuli amesema kwa upande wa miundombinu wamekarabati barabara ya Mafinga zaidi ya kilomita 74.1 pamoja na kupanga kuupanua uwanja wa ndege Nduli ili kuwa mkubwa na kufanya Mkoa wa Iringa kuwa kitovu cha utalii katika Nyanda za Juu Kusini huku akisisitiza kuwa, wakipewa ridhaa kuna mambo mengi zaidi ya hayo watayatekeleza ikiwemo kuboresha, kuanzisha na kuimarisha sekta ya utalii ili ifungue fursa nyingi za ajira.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news