Waziri Bashungwa:Tunakwenda kurejesha heshima ya michezo

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa amesema kuwa katika uongozi wake atahakikisha heshima ya michezo hapa nchini inarejea, anaripoti Shamimu Nyaki (WHUSM) Dar es Salaam.

Bashungwa ameyasema hayo jijini Dar es Salaam ambapo alifanya kikao na makocha pamoja na wanamichezo wa zamani na ameeleza kuwa Serikali imeanza kutenga fedha kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Michezo.

"Lengo la kikao hiki ni kupokea mawazo kutoka kwenu namna bora ya kuendesha michezo ili tupate mafanikio kama ambayo tulipata hapo zamani wakati nyie mkilitumikia taifa letu katika soka" alisema, Waziri Bashungwa.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa akisalimiana na mmoja wa mchezaji wa zamani baada ya kikao na Wachezajia pamoja na Makocha wa zamani kuhusu maendelo ya michezo nchini.

Bashungwa ameongeza kuwa marekebisho yaliyofanywa katika Sheria za Baraza la Michezo la Taifa (BMT) ya mwaka 1967 kuhusu michezo ya ridhaa na kulipwa, kwa sasa inatambua michezo ya kulipwa ambapo kuna wachezaji zaidi ya 2000 wanaocheza michezo ya kulipwa ndani ya nchi na wanamichezo takriban 28 wanacheza michezo ya kulipwa nje ya nchi. 

Aidha, Waziri Bashungwa amewapongeza wachezaji wa zamani kwa jinsi walivyojituma kwa nidhamu na moyo wa kizalendo kuipigania nchi na kufanikiwa kufuzu katika mashindano ya AFCON mwaka 1979.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa (katikati), Naibu Waziri Abdallah Ulega wakiwa katika picha ya pamoja na Wachezaji pamoja na Makocha wa zamani baada ya kikao hicho.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Abdallah Ulega ameiagiza Idara ya Michezo kusimamia maazimio yote ya kikao hicho kufanyiwa kazi na matokeo yaonekane.

"Nia yetu ni kuendeleza michezo, na hili tutalisimamia vyema hivyo tunaomba mawazo mazuri kutoka kwenu namna ya kuendeleza michezo,"amesema Ulega.

Ulega ameongeza kuwa dhamira ya vikao na wadau wa michezo ni kutathmini michezo ilipotoka, ilipo na wapi ielekee kwa maslahi ya taifa.

Naye kiungo wa zamani wa Yanga na timu ya taifa, Ally Mayai Tembele ameishukuru Serikali kwa kuandaa vikao vya kukutana na wadau kupokea mawazo kuhusu maendeleo ya michezo nchini, huku akieleza kuwa michezo inahitaji nidhamu na kuwekeza kwa Watoto wa shule za msingi na sekondari, vifaa vya michezo na miundombinu bora ya michezo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news