Prof.Mchembe: Acheni kupandisha gharama za vipimo

Serikali imezitaka hospitali zinazopokea wagonjwa wenyewe matatizo ya magonjwa ya upumuaji katika mfumo wa hewa kuacha kutoza gharama kubwa kwa wagonjwa hao, anaripoti Mwandishi Diramakini.
 
Pia imesema fedha hizo zinatozwa huku wakiwa hawajui kuwa mgonjwa huyo anasumbuliwa na tatizo gani, kwani matatizo ya upumuaji katika mfumo wa hewa ni dalili ya magonjwa mengi na sio corona peke yake.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto (Idara Kuu ya Afya),Prof.Mabula Mchembe ameyasema hayo leo Februari 3, 2021 jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kutembelea Hospitali ya AghaKhan na Kairuki ikiwa ni muendelezo wa kuangalia wingi wa wagonjwa waliopo hospitalini kama wana matatizo ya kupumua tu, kama mitandao ya kijamii inavyoripoti.

Prof.Mchembe amesema, hospitali hizo zinapaswa kuweka gharama zinazostahili na sio wenye tatizo la kupumua ndio wanatozwa gharama kubwa.

“Niwaase kwende kwenye gharama zinazostahili, kwani mgonjwa anayeumwa anashindwa kupata hiyo fedha ya kulipia kwa sababu anaumwa na hapo hajui anachoumwa ni kitu gani, kwani anaweza kuwa na tatizo la pumu au moyo, halafu unaweka gharama kubwa kwa mgonjwa.

“Hospitali zisitumie nafasi hii ya matatizo ya kupumua katika mfumo wa hali ya hewa ambayo sio mgonjwa ya corona kwa kuweka gharama kubwa ya matibabu,wakati mlikuwa mnawahudumia wagonjwa kabla ya hili tatizo kwa gharama ya kawaida,”amesema Prof.Mchembe.


Prof.Mchembe ameziasa hospitali binafsi zisitumie nafasi hii kuweka gharama ambazo sio za kumuhudumia binadamu bali za kumuongezea maumivu na kumuharibia maisha mgonjwa baada ya kumuhudumia.

“Leo nimefika Hospital ya AghaKhan na Kairuki kama muendelezo wangu wa ziara ambayo nilianza juzi kuona yanayosemwa mitandaoni kama ni kweli,ila nimejiridhisha kuwa bado hospitali zipo wazi kwa matibabu yote.

“Wagonjwa wote wanaotibiwa katika hospitali hizi sio wagonjwa wa corona ila kuna wagonjwa wa mfumo wa hali ya hewa, hivyo watu wasiogope kwenda hospitalini kwa nia kwamba ya kusikia Aghakhan au Kairuki imejaa wagonjwa ambao wana corona sio kweli,”amesema.

Amesema, ameshuhudia kwa Hospitali ya AghaKhan ina vitanda 170 na mpaka sasa vitanda hivyo havijajaa na wodi moja ina vitanda 33 na vingine 35 huku kwa hospitali ya Kairuki ikiwa na vitanda 150 ambapo sio vyote vimejaa wagonjwa.

“Hapo wanahudumiwa mama wajawazito wanaojifungua,wenye matatizo ya kupumua wapo na wasiokuwa na matatizo ya kupumua nao wapo,kwa ujumla sio kwamba hospitali zimejaa wagonjwa wa corona kama taarifa za mitandaoni zinavyosema,”amesema.

Amezishukuru hospitali binafsi hizo kwa kushirikiana na Serikali katika kujitoa kuwahudumia watanzania wenzao,huku wakitumia njia za kawaida katika kujilinda.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Hospitali ya Kairuki,Dkt. Asser Mchomvu amesema, asilimia 80 ya wagonjwa wao wanatumia huduma ya bima hivyo hawawezi kutoza bei kubwa kwa wagonjwa katika matatizo ya kupumua katika mfumo wa hewa.
Naye Dkt.Mukiza Ngemera kutoka Kairuki amesema, jumla ya wagonjwa wenye matatizo ya mfumo wa hewa wapo 28 kati yao wagonjwa 15 hadi 16 wapo wanaosumbuliwa na magonjwa ya kisukari,Moyo,Dalili za magonjwa ya figo na mmoja mama mjamzito.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news