Mtume
na Nabii Richard Msigwa wa Huduma ya Ebenezer Deliverance Ministry
(EDM) iliyopo Baruti Manispaa ya Musoma Mkoa wa Mara ameongoza maombi maalumu kanisani kwake ya kuombea Uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika
Oktoba 28 mwaka huu, huku akiwataka Watanzania wote kuhakikisha
wanadumisha amani na utulivu, anaripoti Amos Lufungulo (Diramakini) Mara.
Nabii
Msigwa ameyasema hayo kanisani hapo ikiwa ni siku
ya pili ya maombi yanayofanywa na huduma hiyo chini yake na waumini wa Huduma ya Ebenezer ambapo yatahitimshwa leo kwa
lengo la kumuomba Mungu awezeshe zoezi la uchaguzi liweze kufanyika kwa
amani katika kuwachagua madiwani,wabunge na Rais.
Ameongeza
kuwa, tangu mwanzo watawala walikuwepo na walichaguliwa na Mungu. Hivyo
akasisitiza kuwa Mungu pekee ndiye mwenye uwezo wa kuwaongoza
Watanzania kuchagua viongozi bora watakaotenda haki na kuwaletea maendeleo Watanzania kama ambavyo miaka mitano imekuwa ya neema na
baraka kwa mafanikio makubwa Kktika nyanja za kijamii na kiuchumi na
ndio maana huduma hiyo imechukua jukumu la kuombea uchaguzi huo.
"Kupitia maombi yetu, Mungu atatuwezesha kupata viongozi bora wenye hofu
ya Mungu na watakao tenda haki, tunataka viongozi watakaochaguliwa katika uchaguzi huu watokane na Mungu na siyo waganga wa kienyeji,
tunauhakika Mungu atasikia maombi yetu na kujibu sawa sawa na tulivyo
muomba,"amesema Nabii Msigwa.
Aidha,
Nabii Msigwa amewataka watanzania wote kudumisha amani na utulivu
katika kipindi chote cha uchaguzi. Ambapo amesisitiza kuwa amani ndiyo
msingi na chimbuko la maendeleo katika Taifa, hivyo ameonya wenye
kuchezea amani wasifanye hivyo hata kidogo bali wailinde amani na
kuitunza kama amabvyo Mungu ameagiza kwenye kitabu Kitakatifu yaani
Biblia.
"Tunahubiri injili
kwa sababu ya amani, Watanzania wanafanya kazi za maendeleo yao kwa
sababu ya amani, tuilinde amani yetu kwa maslahi yetu sote Mungu ametupa
Taifa ambalo misingi yake ni ya kupendana, kuthaminiana na kujaliana kupitia maombi haya tunaamini Mungu atasimama na Tanzania na kuivusha
salama kipindi hiki cha Uchaguzi Mkuu na hata baada ya uchaguzi
kufanyika,"amesema Nabii Msigwa.
Ametoa
wito pia kwa viongozi wa dini na Watanzania wote, kuendelea kuombea
amani na utulivu katika kipindi hiki kilichosalia kabla ya uchaguzi
kufanyika, huku akibainisha kuwa kama ambavyo Mungu amesaidia kulivusha
Taifa katika janga la Corona na uchaguzi utafanyika kwa amani na utulivu.
Tags
Habari

