Mazungumzo ya Rais Dkt.Mwinyi, Mabalozi wa NORDIC yafana Ikulu Zanzibar

Na Diramakini (diramakini@gmail.com)

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameeleza kuwa azma ya nchi za Denmark, Finland, Norway na Sweden ya kuendelea kuiunga mkono Zanzibar kiuchumi na kimaendeleo inaleta faraja.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Ujumbe wa Mabalozi kutoka Nchi za Nordic (kutoka kulia) Balozi Elizabeth Jocobse Nchini Norway,Balozi Anders Sjoberg nchini Sweden,Balozi Mette Nargaard Dissing-Spandet nchini Denmark na Balozi Ritta Swan Nchini Finland (hayupo pichani) walipofika Ikulu Jijini Zanzibar leo .[Picha na Ikulu] 25/05/2021. 

Ameeleza hayo leo Mei 25, 2021wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Mabalozi wa nchi hizo akiwemo Balozi  Mette Norgaard Dissing-Spandet kutoka nchini Denmark, Balozi Riitta Swan kutoka nchini Finland, Balozi Anders Sjoberg kutoka nchini Sweden na Balozi Elizabeth Jacobse kutoka Norway.

Katika maelezo yake Rais Dkt.Mwinyi amewaeleza mabalozi hao hatua za makusudi zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Nane katika kuuimarisha uchumi na kukuza maendeleo ikiwa ni pamoja na kuanzisha uchumi wa Buluu.

Aidha, Rais Dkt.Mwinyi amewaleza mabalozi hao juhudi za makusudi zilizochukuliwa na Serikali katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji ikiwa ni pamoja na kuweka Sera na sheria rafiki na kuanzisha kituo maalum cha uwekezaji ambacho kitawahushisha watendaji wote kwa pamoja “One Stop Center”.

Rais Dkt.Mwinyi ametoa shukurani kwa utayari waliouonesha mabalozi hao kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha utalii, afya, elimu, uchumi wa buluu, sekta ya nishati, viwanda, utoaji wa mafunzo kwa wafanyakazi na uhifadhi wa mazingira na mengineyo.
Mabalozi kutoka Nchi za Nordic wakifuatilia kwa makini wakati wa Mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi (hayupi pichani) yaliyofanyika Ikulu Jijini Zanzibar leo (kutoka kulia) Balozi Elizabeth Jocobse Nchini Norway,Balozi Anders Sjoberg nchini Sweden,Balozi Mette Nargaard Dissing-Spandet nchini Denmark na Balozi Ritta Swan Nchini Finland.[Picha na Ikulu] 25/05/2021.

Kwa upande wa sekta ya afya, Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, itakuwa ni vyema iwapo nchi hizo zitaisadia Zanzibar katika uimarishaji wa mifumo na ujenzi wa miundombinu ya afya.

Aidha, amewataka mabalozi hao kushirikiana nja Serikali katika utekelezaji wa azma ya Serikali iliyopo ya kuanzisha Bima ya Afya, kamka hatua muhimu ya kupunguza gharama za uendeleshaji wa sekta hiyo.

Kadhalika, Rais Dkt.Mwinyi ameeleza juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika kuimatrisha sekta ya utaliii ambayo ndio muhimili mkuuu wa uchumi wa zanzibar.

Amesema kwamba, kuzuka kwa maradhi ya COVID-19 kumeathiri sana maendeleo ya sekta hiyo na hatimae kuathiri kasi ya uchumi wa Zanzibar na ukusanyaji wa mapato na kuzitaka nchi hizo kuunga mkono juhudi katika kuimarisha sekta hiyo.

Amesema kwamba, Serikali yake imejipanga kushirikiana na sekta binafsi na washirika wa maendeleo hasa katika kuziendeleza sekta zote muhimu za kiuchumi na kijamii na kutoa nafasi kwa wawekezaji kutoka nchi mbalimbali kuja kuwekeza Zanzibar.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi alipokuwa akiagana na Ujumbe wa Mabalozi kutoka Nchi za Nordic ikiwemo Denmark,Finland,Norway na Sweden walipofika Ikulu jijini Zanzibar baada ya mazungumzo yao yaliyofanyika leo .[Picha na Ikulu] 25/05/2021.

Mabalozi hao wote walitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa ushindi wake mkubwa alioupata katika uchaguzi mkuu uliopita wa mwaka 2020 na kumuwezesha kuiongoza Zanzibar chini ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa ambayo imeanza kupata mafanikio makubwa.

Mabalozi hao pia, walieleza kufarijika na mwanga wa matumaini ya Zanzibar kupata maendeleo ya haraka kutokana na kasi ya uongozi wa Rais Dkt.Mwinyi huku wakieleza matarajio yao makubwa ya kuimarika kiuchumi, kisiasa na kijamii.

Katika mazungumzo hayo Balozi wa Denmark nchini Tanzania, Mette Norgaard Dissing-Spandet alimueleza Rais Dkt.Mwinyi azma ya nchi yake kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuendeleza miradi mbali mbali ya maendelo ikiwemo miradi katika sekta ya afya.

Nae Balozi Riitta Swan kutoka nchini Finland alimpongeza Rais Dkt.Mwinyi kwa Serikali anayoiongoza kuja na Sera za uchumi wa buluu na kueleza kuwa hatua hiyo itaipa kwa kiasi kikubwa Zanzibar kutokana na mazingira yake sambamba na kuwepo vyanzo vingi vya uchumi huo.

Hivyo, Balozi Swan alimuhakikishia Rais Dkt.Mwinyi kwamba Serikali yake itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kuimarisha uchumi wa Buluu.
 
Balozi wa Anders Sjoberg kutoka nchini Sweden alimueleza Rais Dkt. Mwinyi kuwa nchi yake itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo miradi ya elimu, mazingira

Nae Balozi wa Norway, Elizabeth Jacobse alieleza azma ya Serikali yake kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuendeleza sekta ya nishati hasa katika kuliimarisha Shirika la Umeme la Zanzibar (ZECO) pamoja na kuuimarisha Mfuko wa TASAF.

Wakati huo huo, Rais Dkt.Mwinyi alikutana na Timu ya Madaktari kutoka China waliopo Zanzibar wakiongoza na  Wang Yiming ambapo aliwapongeza kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kutoa huduma kwa jamii kwa miaka mingi.

Rais Dk. Mwinyi aliieleza timu hiyo ya madaktari kwamba wananchi wa Zanzibar wanafurahishwa na huduma zao wanaozitoa kwa jamii huku akieleza juhudi wanazozichukua za kutoa mafunzo kwa madaktari wazalendo kwamba hatua hiyo imekuwa ikileta tija kubwa kwa Taifa.

Nao ujumbe huo kupitia kiongozi wao Wang Yiming alieleza kuwa timu hiyo ya 30 ya Madaktari kutoka nchini China jumla yao ni 21 wakiwemo madaktari 18 ambao wanatoa huduma katika hospitali ya Mnazi Mmoja na Hospitali ya Abdalla Mzee.

Wang Ying alieleza kwamba mbali ya kutoka huduma katika hospitali hizo kubwa hapa Zanzibar pia, wamekwua wakitoa huduma za afya katika jamii zikiwemo hospitali ndogo ndogo ikiwemo kutoa dawa, tiba hasa katika siku za mwisho wa wiki pamoja na kutoa mafunzo ya udaktari kwa madaktari wazalendo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news