NCAA yaendesha Operesheni Maalum ya kufyeka mimea vamizi ndani ya hifadhi

Na Kassim Nyaki (NCCA), Arusha

Watumishi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) wakiongozwa na Kamishna wa Uhifadhi wa NCAA, Dkt. Freddy Manongi wamefanya Operesheni Maalum ya kufyeka mimea vamizi ambayo imeathiri maeneo mbalimbali ya eneo la hifadhi.
Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Dkt. Freddy Manongi (kushoto) akiongoza zoezi la kufyeka mimea vamizi aina ya Bidens schimperi ambayo imeota ndani ya Kreta ya Ngorongoro, mimea hiyo inatarajiwa kufyekwa yote ndani ya wiki mbili zijazo.
Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Dkt. Freddy Manongi akiongea na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu operesheni maalum ya kufyeka na kung’oa mimea vamizi ndani ya eneo la Hifadhi hiyo.

Akizungumza wakati wa Operesheni hiyo, Dkt. Manongi ameeleza kuwa mimea vamizi ya aina mbalimbali imeathiri maeneo ya ndani ya Hifadhi hususan maeneo ya Ndutu, Olduvai na eneo la Kreta ya Ngorongoro ambalo takribani hekta 5000 sawa na asilimia 22 ya eneo lote la Kreta limeathirika na mimea hiyo.
Kamishna wa Uhifadhi wa NCAA Dkt. Freddy Manongi (wa kwanza kulia) akitoa maelekezo kwa baadhi ya wajumbe wa Menejimenti ya NCAA na wananchi waliohudhuria zoezi la kufyeka mimea vamizi ndani ya eneo la Hifadhi.

Dkt. Manongi ameongeza kuwa pamoja na kuwa kazi hiyo imekuwa ikifanyika miaka yote lakini mimea hiyo imeongezeka kutokana na kuwepo kwa mvua nyingi za mwaka jana hivyo ofisi yake imeamua kushirikisha wadau mbalimbali wa uhifadhi ili kukabiliana na changamoto hiyo kwa uharaka zaidi.
Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa NCAA (Fedha na Uhasibu) Mathew Mkunda akishiriki zoezi la ufyekaji wa mimea vamizi katika kreta ya Ngorongoro.

"Tumeamua ofisi ihamie hapa kwa muda ili watumishi wote washiriki kazi hii maalum, utaona kuwa asilimia 22 ya eneo lote la kreta ya Ngorongoro limepata athari ya mimea hii ambayo imeongezeka sana kutokana na mvua nyingi za mwaka jana, tutaweka kambi hapa kwa zaidi ya wiki mbili kuhakikisha tunapunguza ama kumaliza kabisa tatizo hili,” alisisitiza Dkt.Manongi.
Mhadhiri Mwandamizi kutoka Chuo cha Wanyamapori (MWEKA) akielezea namna chou hicho kilivyoamua kutoa Wakufunzi na wanafunzi 320 kushiriki zoezi la kufyeka mimea vamizi ndani ya eneo la Hifadhi ya Ngorongoro kama sehemu ya wadau muhimu katika Sekta ya Uhifadhi.
Mfano wa muonekano wa mimea vamizi aina ya bidens Schimperi iliyoota kwa wingi katika eneo la Kreta ya Ngorongoro ambayo kwa sasa inafanyika operesheni maalum ya kuteketeza mimeo hiyo.
Kamishna huyo wa NCAA ameeleza kuwa kampeni hiyo inayoshirikisha watu zaidi ya mia saba inajumuisha watumishi zaidi ya 250 wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, wakufunzi na wanafunzi 320 kutoka Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapri (MWEKA), Askari wa mafunzo zaidi ya 30 kutoka Shirika la Palm Foundation, Vibarua 115 kutoka Wilaya ya Karatu pamoja na Wananchi wanaosihi ndani ya Hifadhi.

Kwa upande wake Kaimu Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayesimamia Idara ya Wanyamapori na Nyanda za Malisho Bi. Vicktoria Shayo ameeleza kuwa uwepo wa mimea vamizi katika eneo la hifadhi husababishwa na mambo mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya tabia nchi, vifaa vya ujenzi, mazao kama mahindi na mifugo inayoingia ndani ya Hifadhi ambapo kwa pamoja huchangia uwepo wa mimea hiyo.

Ametaja mimea Vamizi iliyopo katika eneo hilo kuwa ni pamoja na Bidens schimperi, gutenbergia cordifolia, Datura, stramonium na argemone Mexicana ambapo njia za kitaalamu zinazotumika kuangamiza mimeo hiyo ni pamoja na kufyeka, kufyeka na kuchoma.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news