TANZANIA NA KENYA ZAKUBALIANA KUONDOA VIKWAZO 30 VYA BIASHARA VISIVYO VYA KIUSHURU, VIKWAZO VINGINE 34 VIPO KWENYE MKAKATI WA UTEKELEZAJI

 Na Eliud Rwechungura

Waziri wa Viwanda na Biashara Prof. Kitila Mkumbo (Mb) amewahamasisha wafanyabiashara wa Kitanzania kuendelea kufanya biashara na kwenda kuwekeza nchini Kenya kwa kuzingatia sheria, taratibu na miongozo iliyopo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na amewataka kuwasiliana na Wizara iwapo kutakuwa na changamoto zozote.
Waziri wa Viwanda na Biashara nchini Tanzania Prof. Kitila Mkumbo na Waziri wa Viwanda, Biashara na Maendeleo ya Wajasiliamali nchini Kenya, Mhe. Betty Maina na ujumbe kutoka hizo nchi mbili wakiwa majidiliano ya masuala mbalimbali ya biashara ikiwemo kuondoa vikwazo vya biashara visivyokuwa vya kiushuru baina ya nchi ya Tanzania na Kenya katika kikoa kilichofanyika ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa (AICC) jijini Arusha, 29 Mei 2021.

Hayo ameyasema katika Mkutano wa tano (5) baina ya Tanzania na Kenya kwa ajili ya kujadili masuala mbalimbali ya biashara ikiwemo vikwazo vya biashara visivyokuwa vya kiushuru (NTBs) baina ya nchi hizo uliofanyika kuanzia tarehe 26 hadi 29 Mei 2021 katika ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa (AICC) jijini Arusha.

Katika mkutano huo Waziri wa Viwanda na Biashara Prof. Mkumbo ameongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki Mkutano huo ambao ulijumuisha Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu – Uwekezaji, Waziri wa Kilimo, Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda – Zanzibar, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto, wakati ujumbe wa kenya ukiongozwa na Waziri wa Viwanda, Biashara na Maendeleo ya Wajasiliamali Mhe. Betty Maina aliyeambana na Balonzi wa Kenya nchini Tanania
Waziri wa Viwanda na Biashara nchini Tanzania, Prof. Kitila Mkumbo na Waziri wa Viwanda, Biashara na Maendeleo ya Wajasiliamali nchini Kenya, Mhe. Betty Maina wakisaini makubaliano ya kutatua masuala mbalimbali ya biashara katika sekta za kilimo, forodha, uhamiaji na usafirishaji kwenye kikao cha Pamoja cha nchi hizo katika ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa (AICC) jijini Arusha, 29 Mei 2021.

Aidha, Waziri amesema kuwa mkutano huo ni utekelezaji wa maelekezo ya kuimarisha mahusiano ya biashara na nchi jirani yaliyotolewa katika Ziara ya Kiserikali iliyofanywa nchini Kenya na, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan tarehe 4-5 Mei 2021.

Prof. Mkumbo amesema Mkutano huo wa kibiashara baina ya nchi hizo ulilenga kujadili masuala mbalimbali ya biashara katika sekta za kilimo, forodha, uhamiaji na usafirishaji. Jumla ya masuala 64 yamejadiliwa ambapo kati ya hayo masuala 30 yametatuliwa na mengine 34 yaliyobaki yamewekewa mkakati maalum na muda wa utekelezaji.

Miongoni mwa masuala yaliyotatuliwa kwa upande wa Tanzania ni pamoja na kuwezesha upitishaji wa bidhaa mpakani, hususan vinywaji baridi kama vile juisi kutoka Tanzania kwenda Kenya, kuondolewa kwa tozo za ukaguzi (inspection fees) zilizokuwa zinatozwa na Mamlaka za Kenya kwenye bidhaa za Tanzania, ikiwemo unga wa ngano, zenye alama ya ubora kutoka Mamlaka husika Tanzania, kuwezesha upitishaji wa mahindi kutoka Tanzania kwenda Kenya na Kuondoa ushuru wa asilimia 25 kwenye bidhaa za kioo kutoka Tanzania kwenda Kenya. Amefafanua Prof. Mkumbo.
Waziri wa Viwanda na Biashara nchini Tanzania, Prof. Kitila Mkumbo na Waziri wa Viwanda, Biashara na Maendeleo ya Wajasiliamali nchini Kenya, Mhe. Betty Maina wakibadilishana nyaraka zilizosainiwa makubaliano ya kuondolewa kwa masuala 30 na mengine 34 yaliyobaki yamewekewa mkakati maalum na muda wa utekelezaji ya kuondoa kuondoa vikwazo vya biashara visivyokuwa vya kiushuru baina ya nchi ya Tanzania na Kenya katika ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa (AICC) jijini Arusha, 29 Mei 2021.

Kwa upande wa Kenya, masuala yaliyotatuliwa ni pamoja na kutoa upendeleo kwa bidhaa za sementi zinazozalishwa nchini Kenya ambazo zinakidhi matakwa ya vigezo vya uasili wa bidhaa vya na Jumuiya ya Afrika Mashariki, kutoa upendeleo maalum kwa vinywaji kutoka Kenya ikiwemo juisi za nanasi (Pineapple Juices) baada ya kukidhi vigezo vya uasili wa bidhaa vya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Masuala mengine ni pamoja na kuhakikisha bidhaa zinazoharibika haraka kama vile maziwa zinapewa kipaumbele zinapovuka mpaka kutoka Kenya kuingia Tanzania kwa kuzingatia taratibu za Sheria ya Forodha na kuongeza muda (validity period) wa kibali cha kuingiza bidhaa za mifugo kutoka siku 15 hadi siku 30. Amefafanua Prof. Mkumbo.

Pia, Prof Mkumbo amesema kabla ya Mkutano wa Mawaziri ulitanguliwa na Mkutano wa Makatibu Wakuu kutoka nchi hizo uliofanyika Mei 28, 2021 jijini Arusha. Ujumbe huo wa Tanzania ulijumuisha Makatibu Wakuu kutoka kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara; Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda – Zanzibar,Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Uchukuzi), Kaimu Katibu Mkuu –Wizara ya Mifugo na Uvuvi,Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Balozi wa Tanzania nchini Kenya, na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania.
Mawaziri wa Tanzania na Kenya na ujumbe walioambatana nao wakiwa kwenye kikao cha majidiliano ya masuala mbalimbali ya biashara ikiwemo kuondoa vikwazo vya biashara visivyokuwa vya kiushuru baina ya nchi ya Tanzania na Kenya katika sekta za kilimo, forodha, uhamiaji na usafirishaji kwenye kikao kilichofanyika ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa (AICC) jijini Arusha, 29 Mei 2021. (Picha zote na Eliud Rwechungura).

Aidha, wajumbe wa mkutano huo baina ya nchi hizo walipata fursa ya kutembelea mpaka wa Namanga pande zote mbili na kujionea jinsi biashara na shughuli za upitishaji wa bidhaa na huduma zinavyofanyika katika mpaka huo ikiwa na Lengo la kuwahakikishia wafanyabiashara kuwa maagizo ya Waheshimiwa Marais wa Tanzania na Kenya yamefanyiwa kazi kikamilifu na wanatakiwa kufanya biashara kwa kuzingatia sharia taratibu na miongozo iliyopo

Katika makubaliano hayo, nchi hizo zilikubaliana kuunda Timu ya Maafisa Wanne(4), yaani Maafisa Wawili (2) kutoka kila Nchi, kwa ajili ya kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa maazimio ya Mkutano huu, na kuhakikisha kuwa vikwazo vilivyotatuliwa havijitokezi tena.

Pia, amesema kuwa nchi hizo zimekubaliana kudumisha ushirikiano baina yake hususan katika nyanja za uchumi, biashara na uwekezaji kwa kufuata taratibu zote zinazokubalika kupitia Jumuiya ya Afrika Mashariki ambapo nchi hizo mbili ni wanachama.

Naye Waziri wa Viwanda, Biashara na Maendeleo ya Wajasiliamali nchini Kenya Mhe. Betty Maina amesema amefurahishwa na mkutano huo kwani umeweza kutekeleza maagizo ya Marais wa nchi hizo mbili na kufanikiwa kutatua masuala 30 na ameahidi ndani ya miezi mitatu watahakikisha changamoto zilizobaki watazimaliza na kufanya wafanyabiashara wa hchi mbili hizo wanafanya biashara bila vikwazo vyovyote.

Hata hivyo, amewataka wafanyabiashara kati ya nchi hizo mbili kufuata taratibu na sheria zilizopo katika biashara baina yao ili kukuza uchumi wa nchi zao kwa kushirikiana na kutumia bidhaa zinazozalishwa kati ya nchi hizo.

Nchi hizi mbili zimekuwa na utaratibu wa kukutana mara kwa mara kujadili masuala mbalimbali yanayohusu Biashara na Uwekezaji. Mikutano hiyo imekuwa ikiwakutanisha Wataalamu kutoka Wizara, Taasisi za Serikali wawakilishi wa Sekta Binafsi pamoja na Wafanyabiashara. Kupitia mikutano hiyo, masuala mbalimbali vya biashara yamekuwa yakijadiliwa na vikwazo vya biashara vinavyojitokeza kupatiwa ufumbuzi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news