Waziri Ally Kissinger wa The Kilimanjaro Band afariki

NA MWANDISHI DIRAMAKINI

Msanii wa Muziki, Waziri Ally Kissinger wa The Kilimanjaro Band (Wana Njenje) amefariki dunia usiku wa kuamkia leo katika Hospitali ya Mwananyamala mkoani Dar es Salaam.

Mwanamuziki a Mwanzilishi mwenza wa Kilimanjaro Band, Mzee Keppy Kiombile amethibitisha kufariki kwa Waziri Ally (pichani).
“Alianza kujisikia vibaya Jumatano akiwa Tanga ambako Jumamosi alitumbuiza na alisafiri mpaka Tanga akiendesha gari mwenyewe, Jumatano alisema hajisikii vizuri na atakapo rudi Dar es salaam itabidi akacheki sasa jana akarudi na kaka yetu mwingine ndiyo alimuendesha alipofika mchana akaenda Dispensary Mwenge, akahudumiwa na akawekewa drip mbili na alipotoka pale alikuwa fresh.

“Ilipofika jioni jana akawa anasema hajisikii vizuri akaingia ndani kulala, baadae akawa haongei na hali yake ikabadilika na kuwa mbaya zaidi wakati tunampeleka hospitali, tulipofika Hospitali Mwananyamala nafikiri alikuwa ameshakata roho njiani.

“Alikuwa na presha kwa muda mrefu na hata hivyo anashida ya moyo na alishawahi kwenda India kufanya matibabu mwaka jana na alikuwa akitibiwa na dawa za India pia, kuhusu msiba ulipo tumekuja kwa Baba yake Mwembe Chai, hivyo tunajaribu kujadili kuona Baba yake atasemaje,"amesema Keppy Kiombile.


Daaa!! Kaka Waziri.

Kwa nini???????


Nimeumia sana, Nimeumia mno.


Daima nitakukumbuka kwa moyo wake wa upendo, ushirikiano na ubinadamu wa kweli. Najua wengi tunakulilia kwa jinsi ulivyoishi nasi, ulivyotuburudisha, ulivyotutia moyo, ulivyotufundisha utu, furaha na ulivyoipenda kazi yako ya muziki na Wananjenje wenzako (The Kilimanjaro Band).

Uliifanya kazi yangu kuwa nyepesi sana pale Ikulu, uliitika wakati wote ulipotakiwa dhifani na wala hukuuliza malipo, uliiweka Tanzania kwanza na nakumbuka maneno yako ya mwisho kwangu “Mdogo wangu Msigwa nakushukuru sana kwa kutuamini, wakati wowote ukituhitaji tutakuja, hizi shuguli zetu sote” Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa.

Lala salama Gwiji, lala salama Waziri Ally. Tutakukumbuma Daima.

Inna lillahi wa inna ilayhi raji'un.


Kulingana na taarifa zilizokusanywa juu ya mwanamuzi huyo, imefahamika kuwa aliweza kufanya kazi ya sanaa ya muziki kwa zaidi ya miaka 50 na miaka 44 pekee hadi anafikwa na umauti amekuwa ni msanii na kiongozi wa bendi ya The Kilimanjaro Band.

“Leo ni siku ya Jumamosi kwa desturi yake Waziri Ally alikuwa akiamka asubuhi na kufanya shughuli zake za kawaida na ikifika jioni anarudi hapa nyumbani kwa mapumziko ili kujiandaa na maonesho yake ya usiku katika kumbi mbalimbali za burudani akiwa na wananjenje-The Kilimanjaro Band.” Alidokeza Masoud Masoud ambaye ni Mtangazaji Mkongwe wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) na mdau mkubwa wa muziki nchini.

Sasa hatunaye tena, ndiyo ameondoka, kubwa kwa wanamuziki wa Kitanzania ni kuiga mema ya ndugu yetu Waziri, haswa la kuweza kuwaunganisha wanamuziki na kuweza kuwafundisha vijana wengi muziki husasani upigaji wa ala za muziki ameongeza Masoud Masoud.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Sanaa wa Wizara ya Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo Mfaume Said, amesema kuwa amepokea kwa masikitiko msiba huo kwani mchango wa Waziri Ally ni mkubwa na hauna kipimo cha kupimia.

“Kumuenzi ni kuyaiga mazuri yake na kuendelea kukuza sanaa ya muziki nchini kwa manufaa ya kizazi cha leo na kijacho.”Aliongeza Kaimu Mkurugenzi huyo.

Mwaanamuziki Waziri Ally ni mzaliwa wa Pongwe mkoani Tanga ataendelea kukumbukwa na wadau wa muziki na Watanzania wengi kwa nyimbo kadha wa kadha kama vile Kinyanyau, Tupendane Mpenzi , Gere na nyingine nyingi.

…”. Mie na wangu nyumbani,
Mambo yangu Burudani,
Masikio nimeziba,
Sijali ya mitaani,
Wangu nimedhibiti,
Hasiki wala haoni,
Jaribuni Kwengine,
Hapa hamuoni ndani,

Wacha wachawaseme , watasema mchana ehh na usiku watalala .”

Kwa hakika Waziri Ally ametutoka , huu ni wakati mgumu kwa familia, wakati mgumu kwa wapenzi wake wa muziki na wakati mgumu kwa CHAMUDATA na sisi Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

“Basi watu wengi miongoni mwa wanafunzi wake waliposikia, walisema, Neno hili ni gumu, ni nani awezaye kulikisikia.” Kwa hakika maneno hayo ya Kitabu kimojawapo cha dini yanaufunga ukurasa wa maisha ya mwanamuziki Waziri Ally na ni kweli msiba ni neno gumu, Kwaheri Waziri Ally.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news