TAKUKURU ilivyomsomea ramani askari wa usalama barabarani wakati akipokea rushwa maeneo ya Ipogolo mjini Iringa

NA MWANDISHI DIRAMAKINI

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa mkoani Iringa imethibitisha kumkamata askari wa usalama barabarani kwa kosa la kupokea rushwa kwenye mabasi maeneo ya Ipogolo Manispaa ya Iringa siku ya Januari 18, 2022.
Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Iringa,Domina Mukama amesema kuwa,walimkamata Koplo Steven Mchomvu akipokea rushwa kwenye mabasi ambayo yanapita katika barabara ya Ipogolo.

Amesema kuwa, picha ambazo zimesambaa kwenye mitandao ya kijamii zilipigwa na maafisa wa TAKUKURU Mkoa wa Iringa mara baada ya kumkamata askari huyo wa usalama barabarani akipokea  rushwa kutoka kwenye basi.

Mukama amesema kuwa, polisi huyo bado anashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa na taratibu zote zikikamilika atapelekwa, ndio watatoa taarifa nini kitafanyika kwa mujibu wa sheria za nchi.

Amesema kuwa, walimkuta na kiasi cha shilingi laki moja na nusu pesa taslimu ambazo alikuwa nazo mfukoni ambazo alikuwa akipokea rushwa kwa magari mbalimbali.
Mkuu huyo ametoa onyo kwa watumishi wote wa serikali waache mara moja tabia ya kutoa na kupokea rushwa kwa kuwa ni kinyume cha sheria za utumishi wa  umma kama abavyo walikula kiapo wanapoanza
kazi.

Mukama amesema kuwa, mara baada
ya kumkamata askari wa usalama barabarani Koplo Steven Mchomvu alimshirikisha OCD wa Iringa kwa sababu vyombo vya ulinzi na usalama vinafanya kazi kwa pamoja.
Pia amesema TAKUKURU Mkoa  wa Iringa  wamefanikiwa kukagua jumla ya miradi 12
yenye thamani ya shilingi bilioni 7,135,579,015.

Amesema kuwa, miradi hiyo ni ya sekta ya elimu,ujenzi (barabara) na afya ambayo miradi hiyo ilikaguliwa kwa lengo la kujua thamani halisi ya pesa iliyotumika na ubora wa miradi husika kama inaendana na miradi yote ilikaguliwa na kukuta inaendelea vizuri na kwa ubora unaotakiwa.

Mukama amesema kwa kipindi cha Oktoba na Desemba mwaka 2021 walipokea jumla ya malalamiko 48 yanayohusiana na rushwa, lakini baada ya uchunguzi waligundua kuwa taarifa za rushwa zilikuwa 26 na 22 hazihusiani na rushwa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news