Namtumbo kufungua stendi ya wilaya kuongeza mapato

NA YEREMIAS NGERANGERA 

MKURUGENZI wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Chiriku Hamis Chilumba amesisitiza kufunguliwa kwa stendi ya wilaya kwa lengo la kuongeza ukusanyaji wa mapato na kuwa na stendi iliyopo kisheria tofauti na ilivyo hivi sasa. 

Akiongea na wakuu wa idara na vitengo ofisini kwake alisema ipo haja ya kuanzisha na kubuni vyanzo vya mapato vipya vitakavyoiingizia Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo fedha badala ya kusubiri ushuru wa mazao pekee . 

Chilumba katika kikao hicho aliteua baadhi ya wakuu wa idara akiwemo mkuu wa idara ya ujenzi,mkuu wa idara ya ardhi na maendeleo ya jamii ili kuhakikisha stendi ya wilaya ya Namtumbo inafanya kazi ili kuweza kuongeza ukusanyaji wa mapato. 
Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo, Paul Ambokile alisema maagizo ya mkurugenzi wa Halmashauri yamefanyiwa kazi ipasavyo hivyo stendi ya wilaya inatarajia kufunguliwa Februari 10,2022 ambapo magari yote yatapakia na kushusha abiria katika stendi ya wilaya tofauti na ilivyo sasa ambapo wamiliki wa magari wanapaki magari yao na kupakia abiria maeneo yasiyo rasmi. 

Baraza la Madiwani la Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo limempongeza Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kwa maamuzi hayo na kumhaidi kumpa ushirikiano wa hali na mali katika kusimamia hilo wakidai uhitaji wa stendi ya wilaya kwa wananchi wa Namtumbo kwa sasa ni mkubwa . 

Juma Pandu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo kwa upande wake alidai msimamo wa Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo katika kuimarisha vyanzo vya mapato utaifanya halmashauri ya wilaya ya Namtumbo iwe na vyanzo vya kudumu vya mapato tofauti na ilivyo huko nyuma na kusisitiza kumuunga mkono katika kusimamia utekelezaji wa malengo hayo. 

Rashidi Changana dereva wa bodaboda na bajaji wilaya ya Namtumbo alimpongeza mkurugenzi huyo kwa dhamira yake ya kusimamia ufunguzi wa stendi ya wilaya kwa kile alichokidai haiwezekani wilaya ikose stendi iliyopo kisheria. 

Changana pamoja na pongezi hiyo alisema Halmashauri itapata ushuru kutoka kwenye magari tofauti na hivi sasa ambapo magari mengi hayalipi ushuru na kuikosesha Halmashauri fedha nyingi katika chanzo hicho cha mapato na kuongeza kuwa madereva bodaboda na bajaji watapata ajira ya kubeba abiria na kujipatia kipato.

Stendi ya Wilaya ya Namtumbo inatarajia kufunguliwa tarehe 10 mwezi huu ambapo kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Namtumbo ikiongozwa na mkuu wa wilaya ya Namtumbo, Dkt.Julius Kenneth Ningu imeridhia kupaki na kushusha abiria katika eneo la stendi hiyo ya wilaya na kinyume cha hapo hatua kali zitachukuliwa kwa wale watakaokaidi agizo hilo. 

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news