Kampuni ya Taifa Group tarehe 28 Julai,2026 imetangaza kurejea kwa shughuli za kampuni yake tanzu ya Nation Media Group nchini Uganda kufuatia idhini iliyotolewa na Mheshimiwa Rais Yoweri Kaguta Museveni.
Uamuzi huu ni hatua muhimu katika uwekezaji wa kikanda, maendeleo ya sekta ya habari na ustawi wa ushirikiano wa Afrika Mashariki. Kupitia kampuni tanzu yake, Taarifa Limited, Taifa Group ndiyo mbia mkuu wa Nation Media Group na inaendelea kujitolea katika uwekezaji wenye uwajibikaji, utawala bora wa kampuni na maendeleo endelevu kote katika kanda hii.Akizungumzia hatua hiyo, Mwenyekiti wa Taifa Group, Bw. Rostam Azizi, ametoa shukrani zake za dhati kwa Mheshimiwa Rais Yoweri Kaguta Museveni kwa kuruhusu kurejea kwa shughuli za Nation Media Group nchini Uganda. Pia alitoa shukrani kwa Jenerali Muhoozi Kainerugaba, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ya Uganda (UPDF), kwa uungaji mkono wake katika mchakato mzima uliopelekea matokeo haya chanya akisema,
“Ningependa kutoa shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais Yoweri Kaguta Museveni kwa uamuzi huu muhimu, na kwa Jenerali Muhoozi Kainerugaba kwa uungaji mkono wake katika mchakato mzima uliopelekea matokeo haya chanya.








"Tunajivunia uamuzi huu na tunadumisha azma yetu thabiti ya kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi ya Uganda kupitia uwekezaji wenye uwajibikaji, ushirikiano wa muda mrefu na ujenzi wa thamani endelevu.
"Kama mbia mkuu wa Nation Media Group, tunaunga mkono kikamilifu dhamira ya Kampuni hiyo ya kufuata misingi ya uandishi wa habari wa haki, uwiano, uhuru na uwajibikaji, unaotoa taarifa, kuelimisha na kuchangia vyema katika mijadala ya umma. Tunashiriki dhima kuu ya Kampuni hiyo ya kuleta athari chanya katika jamii, na tunaamini kuwa vyombo vya habari imara, vya kitaalamu na vinavyozingatia uwajibikaji vina jukumu muhimu katika kusaidia maendeleo ya taifa, utawala bora na ushirikiano wa kikanda.”
Tags
Kurasa za Magazeti
Kurasa za Mbele na Nyuma za Magazeti
Magazeti
Magazeti ya Leo
Magazetini
Magazetini leo
Yaliyojiri Magazetini Leo











