Dkt.Ndika awapa darasa mahakimu nchini

>Watakiwa kutokiuka viapo vyao wakati wa utoaji haki, kuepuka rushwa

NA HADIJA BAGASHA

KAMISHNA wa Tume ya Utumishi wa Mahakama ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Dkt. Gerald Ndika amewataka mahakimu nchini kutokiuka viapo vyao wakati wa utoaji haki ikiwa ni pamoja na kutopokea rushwa.

Pia amezitaka kamati za maadili kushirikiana kwa karibu na mihimili yote mitatu ambayo ni Serikali, Bunge na Mahakama ili kuweza kuboresha utoaji wa haki kwa wananchi.
Dkt.Ndika ametoa kauli hiyo wakati Tume ya Utumishi wa Mahakama imefanya ziara mkoani Tanga kwa lengo la kuangalia namna ya kuboresha miundombinu yake na kuboresha huduma kwa wananchi.

Amesema, lengo la ziara ya tume hiyo mkoani Tanga ni kukaa na kamati za maadili za wilaya na mkoa ili kupokea maoni na changamoto za uvunjifu wa maadili kwa watumishi wa mahakama ili kuboresha shughuli za utendaji na utoaji haki ikiwa ni pamoja, na kuzingatia viapo vyao.

"Mahakama ya Tanzania imeaminiwa na wananchi katika suala la utoaji haki,ukisha kiuka viapo kwa njia yeyote ile aidha kupokea rushwa tayari umeacha ule wajibu wako kama wakili,kutokuchelewesha haki bila sababu za msingi,"aliongeza.
Kamishna Ndika amesema lengo la tume kukutana na watumishi hao ni kujadili changamoto mbalimbali ndani ya mhimili huo huku ikisisitiza utoaji haki kwa wananchi.

Aidha, Kamishna Ndika amewataka Mahakimu na majaji kuzingatia kanuni na sheria mbalimbali zinazowaongoza katika kazi zao bila kukiuka wakati wa utoaji haki pamoja na kutokuchelewesha haki kwa wananchi,

"Tumewasisistiza watumiaji wote wa Mahakama wazingatie sheria kwa kutokwenda na kukiuka maadili yao katika utoaji haki kwa wananchi, ikiwa ni pamoja na kutochelewesha haki za wananchi bila sababu za msingi,"alibainisha Dkt.Ndika.
Aliongeza kuwa, kwa upande wa kamati za maadili, "tunawaasa wale wote wanaoziunda hizo kamati washirikiane kwa karibu na mihimili yote mitatu ili tuweze kuboresha utoaji haki hapa nchini kwa maslahi ya nchi yetu,"alisistiza Dkt.Ndika.

Sambamba na hayo Mkuu wa Mkoa wa Tanga ,Adam Malima amesema kuwa licha ya kufurahishwa na ujio huo wa Tume mkoani Tanga ambao utasaidia kuboresha shughuli za kimahakama, lakini pia amesema watahakikisha wanaimarisha ushirikiano baina yao na watendaji wa mahakama kwa kuzingatia utoaji wa haki kwa kila mwananchi.

"Serikali ya mkoa wa Tanga tumefarijika sana kwa ujio wenu , tutaendelea kufanya kazi kuwa kutegemeana, tutawatumia pia viongozi wa dini tukitambua nafasi ya kila mmoja,"alisema Malima.
Tume hiyo imeketi kwa siku mbili mkoani Tanga kwa lengo la kukutana na watumishi wa mahakama ili kusikiliza changamoto na maoni kwa lengo la uboreshaji shughuli za utendaji wa mahakama ambapo kwa mwaka huu wa 2022 tayari imeshapita katika mikoa mitatu ya Tanga, Morogoro na Pwani.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news