SBL yagusa maisha ya wazee Mwika

NA DIRAMAKINI  

KAMPUNI ya Bia ya Serengeti (SBL) imetoa msaada wa mablanketi 150 kwa wazee Mwika mkoani Kilimanjaro ikiwa ni sehemu ya uwekezaji wake wa kuisaidia jamii. Msaada huo kwa wazee ulikabidhiwa kwa niaba yao kwenda kwa Mwika Rotary Club.
Alice Kilembe, Meneja wa Kiwanda cha SBL Moshi (wa pili kulia) akimkabidhi mzee wa Mwika blanketi lake, likiwa ni miongoni mwa mablanketi 150 yaliyotolewa kama msaada na SBL kwa wazee hao kwenye viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Kata ya Mwika mkoani Kilimanjaro hivi karibuni. Wa kwanza ni Awumsuri Masuki,Katibu wa Mwika Rotary Club.

Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi msaada huo, Meneja wa kiwanda cha SBL Moshi, Alice Kilembe alisema kampuni hiyo inajivunia kutoa ushirikiano kwa Mwika Rotary katika kuwathamini na kuwahudumia wazee wanaoishi katika eneo hilo.

"Mchango tunaoutoa leo kwa wazee ni ishara ya upendo na shukrani zetu kwa kazi nzuri waliyoifanyia taifa letu katika enzi za ujana wao." Jamii inapaswa kutunza kikundi hiki, na SBL inajivunia kuwa sehemu hii. Tunaamini mablanketi yatawalinda na baridi kali msimu utakapofika,"alisema.

Sambamba na mchango huo kwa Mwika Rotary Club, Alice alisema kuwa SBL imekuwa ikitekeleza programu kadhaa za kusaidia jamii ambazo hadi sasa zimenufaisha mamilioni ya watu nchini kote.
Alice Kilembe, Meneja wa Kiwanda cha SBL Moshi kwenye picha ya pamoja na uongozi wa Mwika Rotary Club na baadhi ya Wazee wa Mwika mara baada ya kukabidhi mablanketi 150 kwenye viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Mwika hivi karibuni.

"Mnamo mwaka 2019, SBL tulianzisha mpango wa ufadhili wa masomo kwa ajili ya wanafunzi wanaosomea masomo ya kilimo katika vyuo vya ndani ili kuunga mkono jitihada za serikali za kupanua wigo wa wataalamu wa kilimo nchini, na hadi sasa zaidi ya 200 wamenufaika na mpango huu,"alitolea mfano.

"Aidha tumejipanga na tunaendelea na programu nyingi za kusaidia jamii, kama vile kuhakikisha waishio vijijini wanapata maji safi na salama (programu maarufu ijulikanayo kama Water of Life). Hadi sasa tumetekeleza miradi 22 ya maji katika maeneo mbalimbali nchini tangu mwaka 2010, ambapo watu zaidi ya watu milioni mbili wamenufaika,"alikiri.

Programu nyingine alizozitaja meneja huyo wa kiwanda ni pamoja na kilimo biashara, ambacho huwasaidia wakulima wakubwa na wadogo kuongeza uzalishaji huku wakiwaandalia mazingira ya masoko kwa ajili ya mavuno yao.
Wafanyakazi wa SBL Moshi kwenye picha ya pamoja mara baada ya kukabidhi mablanketi 150 kwa Mwika Rotary Club kwenye viwanja vya mahakama ya mwanzo kata ya Mwika mkoani Kilimanjaro.Aliyekuwa Rais wa Mwika Rotary Club, Ester Towo, ambaye alimwakilisha rais wa sasa, Godrick Lyimo, aliishukuru SBL kwa msaada huo, akibainisha kuwa mchango huo ni chachu kubwa kwa shirika hilo, ambalo linategemea michango hiyo ili kuendelea kuihudumia jamii ya Mwika.

"Tunafurahishwa sana na mchango wa blanketi 150 kutoka kwa SBL kusaidia wazee wa Mwika na maeneo ya jirani hasa wakati huu wa mwaka ambapo baridi linakaribia. Mablanketi haya yatawawezesha wazee kupata joto la kutosha wakati wa msimu wa baridi kali hapa Mwika,"alisema.
Ester Towo, mjumbe wa kamati ya Mwika Rotary Club akitoa neno la shukrani kwa SBL mara baada ya kupokea mablanketi 150. Kuanzia kulia kwake ni Anence Kawiche, mjumbe wa Mwika Rotary club, Alice Kilembe, Meneja wa Kiwanda cha SBL Moshi, Mch Elia Saria wa Mwika na Awumsuri Masuki, Katibu wa Mwika Rotary Club. 

"Wazee wengi wanaoishi majumbani mwao wanakosa msaada kwa sababu hawana mtu wa kuwahudumia. Hivyo basi, mchango huu ni mkubwa sana kwao ambao utawafanya wahisi kuthaminiwa na kutambuliwa kwa mara nyingine. Ahsante, SBL,"alisema.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news