Shinyanga wadhamiria kutokomeza Malaria,maagizo yatolewa

NA KADAMA MALUNDE

SERIKALI Mkoa wa Shinyanga imewataka watoa huduma katika vituo vya afya kuboresha huduma za matibabu na kutoa elimu ya kutambua dalili za Malaria na jinsi ya kujikinga ili kupunguza kiwango cha maambukizi na vifo ambavyo vinaweza kuzuilika kwa kuweka nia ya pamoja ya kutokomeza Ugonjwa wa Malaria.
Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Kahama Mhe. Festo Kiswaga wakati akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Sophia Mjema kwenye Maadhimisho ya Kilele cha Malaria Mkoani Shinyanga ambayo yamefanyika leo Jumatatu Aprili 25,2022 katika kijiji cha Didia kata ya Didia halmashauri ya Shinyanga. (Picha na Malunde 1 blog).

Kiswaga pia amevitaka Vituo vya afya vihakikishe vinatoa huduma za upimaji wa malaria kwa wagonjwa wote wenye homa kabla ya kuanzishia matibabu ya malaria “maana sio kila homa ni malaria”.

Aidha Kiswaga amezihimiza Halmashauri za wilaya kutekeleza mikakati ambayo inawekwa na Mpango wa Taifa wa kudhibiti Malaria ili kupunguza madhara na vifo na hatimaye kutokomeza Malaria na kwamba elimu ya Afya itolewe kwa jamii kuhusu kuwahi matibabu mapema na kuondoa imani potofu kuhusu matumizi ya vyandarua vyenye viuatilifu vya muda mrefu.
Mkuu wa wilaya ya Kahama Mhe. Festo Kiswaga akizungumza kwenye Maadhimisho ya Siku ya Malaria Duniani ambayo katika Mkoa wa Shinyanga yamefanyika leo Jumatatu Aprili 25,2022 katika kijiji cha Didia kata ya Didia Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.

“Malaria ni kati ya magonjwa ambayo taifa hutumia rasilimali nyingi katika kupambana nao. Ili kutokomeza Malaria, wananchi tumieni vyandarua vyenye viuatilifu vya muda mrefu kwa kujikinga na mbu wakati wa kulala na sio vinginevyo, kuvulia samaki ,kufugia vifaranga vya kuku,kutumia kama kamba za mifugo,kutumia kama kamba za nguo,”amesema Kiswaga.

Katika hatua nyingine, Kiswaga ameeleza kuwa Takwimu zinaonesha kuwa katika mkoa wa Shinyanga halmashauri ya Wilaya ya Ushetu inaongoza kwa kuwa na maambukizi asilimia 45.2 ya Malaria ambapo mwaka jana 2021 maadhimisho ya siku ya malaria kimkoa yalifanyika katika halmashauri hiyo ikifuatiwa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga 43.1% ambapo Mwaka huu 2022 kilele cha maadhimisho kimkoa yamefanyikia.
Amesema kwa upande wa Halmashauri zingine , Halmashauri ya Wilaya ya Msalala inaongoza kwa maambukizi ya Malaria kwa 37% ,Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu 27.5%, Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga 20.5% na Halmashauri ya Mji Kahama 19.8%.

“Kutokana na takwimu hizo ndiyo maana mkoa umeamua kwa Mwaka huu 2022 kufanya madhimisho haya katika halmashauri ya Shinyanga ili wananchi muweze kujua ukubwa wa tatizo na kujua jinsi ya kulikabili”,amesema Kiswaga.
“Serikali inatumia rasilimali zake nyingi kudhibiti ugonjwa huu, hivyo basi tuzitumie ili kuboresha afya zetu kwa faida ya familia na taifa kwa ujumla kwa kuhakikisha tunapunguza kiwango cha maambukizi na vifo vitokanavyo na malaria”,ameongeza Kiswaga.

Kiswaga amesisitiza wananchi kusafisha mazingira wanayoishi kwa kufyeka nyasi, kufunika madimbwi ya maji, kutoa makopo au vifuu vinavyoweza kutuamisha maji, kuzibua mifereji ya maji ili kuondoa mazalia ya mbu pamoja na Halmashauri kunyunyizia viuadudu katika maeneo yote yenye mazalia ya mbu.
Aidha amewakumbusha wananchi kulala kwenye chandarua chenye dawa ya viuatilifu na Mama mjamzito apate dozi za SP kliniki kipindi cha ujauzito.
Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Yudas amesema Malaria ni ugonjwa unaoambukizwa baada ya kuumwa na mbu jike aina ya Anofelesi aliyebeba vimelea vya Malaria toka kwa mtu mwenye vimelea na kwenda kwa mtu asiye na vimelea mara pale anapomuuma mtu huyo na kwamba maambukizi hayo huleta madhara makubwa na vifo katika jamii.
Dkt. Ndungile pia amewataka wananchi kuwahi mapema kwenye vituo vya afya pindi waonapo dalili za malaria ili kupata matibabu sahihi na kumaliza matibabu yote.

Dkt. Ndungile amezitaja dalili za ugonjwa wa malaria kuwa ni homa, maumivu ya kichwa, kutapika, kuharisha, mwili kuchoka/kuregea na kukosa nguvu na kukosa hamu ya kula.
Maadhimisho ya Siku ya Malaria Duniani mkoa wa Shinyanga yakiongoza na kauli mbiu “Matokeo ya Sensa,Msingi wa Mapambano Dhidi Ya Malaria - Ziro Malaria Inaanza na Mimi” pia yamehudhuriwa na wadau wa afya Kanisa la KKKT Dayosisi ya Kusini Mashariki ya Ziwa Victoria kupitia Idara ya afya ya jamii Uinjilisti ambao wanatekeleza mradi wa kutokomeza malaria katika Halmashauri ya Shinyanga.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news