TANZIA:Msanii Maunda Zorro afariki

NA DIRAMAKINI

MSANII wa Bongofleva, Maunda Zorro amefariki dunia kwa ajali ya gari usiku wa kuamkia leo, Kaka wa marehemu ambaye pia ni Msanii wa Bongofleva Banana Zorro amethibitisha taarifa hizo.
Banana amesema hadi jana jioni alikuwa pamoja na Maunda kwenye msiba wa rafiki yao lakini baadaye akapata taarifa kuwa Maunda amefariki.

"Nimezipata hizo taarifa ndio naelekea Hospitali ya Kigamboni, taarifa ni za kweli tulikuwepo kwenye msiba jioni ya leo wa rafiki yetu mwingine wa karibu, nilikuwa nae Maunda hadi jioni saa 11 hadi 12 nikarudi nyumbani kulala maana msiba ulikuwa Kigamboni na yeye anakaa Tuangoma, kwa taarifa zaidi (kuhusu msiba) ni hadi nikifika Hospitali.

"Chanzo cha kifo ni ajali ya gari, nimeachana na Maunda saa 12 jioni ajali amepata mida ya saa 4 usiku, ila sina uhakika sana (wa muda aliopata ajali) hadi nikifika Hospitali maana nilirudi nyumbani nikiwa nimechoka sana,"amesema.

Maunda ambaye ni dada yake na Banana Zorro na binti wa mwanamuziki mkongwe nchini, Zahir Ally Zorro alikuwa na kawaida ya kuachia nyimbo chache.

“Sina haraka ya kutoa nyimbo kila mwaka, sio kwamba ndio inaprove kwamba wewe ndio mwanamuziki, natoa time inaruhusu kwamba sasa hivi I can, natoa. Saa zingine nakuwa nimebanwa na vitu vingine,” alikaririwa wakati wa uhai wake.

Akiongelea siri ya kuandika nyimbo zenye maisha marefu, Maunda alisema ni kuandika nyimbo zenye hisia za ukweli.

“Kwangu mimi huwa naandika nyimbo ambayo ina ukweli sio fiction, sio kitu cha kufikirika. Naandika kitu ambacho kinagusa jamii hata kama sio cha kwangu, kimetokea sehemu fulani, kimemtokea mtu fulani. Kwa mfano kama nilivyoandika ‘Niwe Wako’, watu wanapendana kila siku. Ndio maana hata ukisiliza hata mwakani bado utahisi kama ni nyimbo mpya na bado inakugusa kwa njia moja ama nyingine,"alikaririwa Maunda Zorro wakati wa uhai wake.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news