Barrick yatekeleza kwa vitendo Sera ya Serikali inayotaka makampuni ya madini kushirikiana na Watanzania

NA DIRAMAKINI

KAMPUNI ya Madini ya Barrick imeanza kutekeleza kwa vitendo sera ya Serikali inayoyataka makampuni ya madini kushirikisha Watanzania katika mnyororo wa uchumi wa madini ambapo hadi kufikia sasa takribani asilimia 70 ya watoa huduma katika migodi yake inayoendesha nchini ni Watanzania.
Meneja wa Barrick nchini, Georgia Mutagahywa, akizungumza kwenye jukwaa la kwanza la utekelezaji wa ushirikishwaji wa Watanzania katika sekta ya Madini, lililofanyika jijini Mwanza.

Kampuni imeanza kutekeleza sera kwa vitendo katika maeneo ya ajira, utoaji wa zabuni, sambamba na kuendesha miradi ya kusaidia jamii katika maeneo yanazozunguka migodi yake nchini kupitia sera ya kampuni ya kuhudumia jamii (CSR).

Hayo yamebainishwa wakati wa jukwaa la kwanza la utekelezaji wa ushirikishwaji Watanzania katika sekta ya madini linalofanyika jijini Mwanza mwishoni mwa wiki.
Baadhi ya washiriki wakifuatilia matukio.

Barrick, tayari imeanzisha programu ya kuwaendeleza wafanyabiashara wa ndani,(Local Business Development Programme (LBD) inayosimamiwa na mgodi wa North Mara, ambayo ni mhimili wa kusimamia kanuni hii na kuhakikisha watanzania wananufaika nayo kwa asilimia kubwa kwa kuboresha maisha yao kupitia uwekezaji katika sekta ya madini, na fursa zilizopo kwenye sekta hii na tayari baadhi ya wafanyabiashara wamepatiwa mafunzo katika awamu ya kwanza.

Rais na Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Barrick, Mark Bristow, alisema wakati wa uzinduzi wake kuwa programu hii inadhihirisha jitihada endelevu za Barrick, katika kujenga uwezo wa watu wa ndani.
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Prof Idris Kikula, akizindua jukwaa la kwanza la utekelezaji wa ushirikishwaji wa Watanzania katika sekta ya Madini, lililofanyika jijini Mwanza.

“Tangu migodi ianze kufanya kazi, tumekuwa tukishirikiana na wakazi wa maeneo yanayozunguka migodi yetu kwa kutengeneza fursa za uchumi endelevu kupitia mkakati wa usambazaji wa bidhaa za ndani kwa ajili ya uchumi wa maeneo hayo na taifa kwa ujumla,”alisema.

Alisema, programu hiyo ya maendeleo ya biashara za ndani italeta mabadiliko makubwa kwenye mnyororo wa thamani kwenye sekta ya madini na kuimarisha makampuni ya ndani sambamba na kutumia fursa zilizopo kwenye mnyororo huo wa thamani.
Baadhi ya Wadhamini wa jukwaa hilo wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Prof.ldris Kikula.

Serikali ya Tanzania, iliunda sera ya Local content mwaka 2015 ikilenga sekta ya madini, mafuta na gesi ili kuhakikisha uchimbaji wa madini na mapato yake yanawanufaisha watanzania.

Sera hiyo na kanuni zake inalenga kupanua uwanda wa kibiashara kwenye uchumi wa Tanzania, kutengeneza nafasi za ajira kwa kuhamasisha maendeleo ya taaluma na uwezo wa watanzania kushiriki katika shughuli mbalimbali za kiuchumi nchini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news