UJUMBE WA ZIMBABWE NCHINI TANZANIA WARIDHISHWA NA USIMAMIZI MASOKO YA MADINI

NA STEVEN NYAMITI-WM

NAIBU Waziri wa Madini wa Jamhuri ya Zimbabwe, Mhandisi, Dkt. Polite Kambamura na ujumbe wake wamesema wamejifunza usimamizi wa masoko ya madini ambayo yamesaidia kurasimisha biashara ya madini kwa wachimbaji wadogo nchini Tanzania.
Naibu waziri wa madini Dkt. Kiruswa na naibu waziri wa madini wa Jamhuri ya Zimbabwe Mhandisi. Dkt. Kambamura na ujumbe wake wakiwa kwenye soko la madini ya Almasi.

Mara baada ya ziara katika Mkoa wa Mwanza, Geita na Shinyanga leo Mei 25, 2022, Dkt. Kambamura na ujumbe wake wamesema wamejifunza kuhusu mwenendo wa masoko ya madini unavyofanya kazi nchini, ambao kwa kiasi kikubwa umeondoa utoroshaji wa madini kwa wachimbaji kwa kupata masoko na bei ya uhakika.
Amempongeza, Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa usimamizi mzuri wa masoko ya madini ambayo yamesaidia kutokomeza utoroshaji wa madini na kuongezeka kwa mapato ya Serikali.

Amesema, lengo la ziara hiyo lilikuwa kujifunza namna wachimbaji wadogo wa madini Tanzania wanavyofanya shughuli zao ili waweze kujifunza na pia kupata uzoefu wa kuwaendeleza wachimbaji wadogo wa Zimbabwe kuongeza ufanisi.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini, Dkt.Steven Kiruswa amemshukuru Dkt. Kambamura na ujumbe wake kwa kutembelea maeneo ya wachimbaji wadogo wa Geita na Shinyanga, masoko ya madini na kiwanda cha kusafisha dhahabu cha Mwanza.

Amesema, ziara hiyo ililenga kujengeana uwezo kuhusu Sekta ya Madini inavyofanya kazi nchini ili kwa pamoja waweze kujifunza masuala mbalimbali ya usimamizi katika sekta hiyo.

Naye, Katibu wa Chama cha Wachimbaji Wadogo Mkoa wa Shinyanga (SHIREMA), Gregory Kibusi ameishukuru wizara kwa kutengeneza mazingira mazuri ya wafanyabiashara wa madini nchini.
Naibu waziri wa madini Dkt. Kiruswa na naibu waziri wa madini wa Jamhuri ya Zimbabwe Mhandisi. Dkt. Kambamura na ujumbe wake wakiwa kwenye soko la madini ya Almasi.

Amesema, ziara ya Naibu Waziri wa Madini wa Zimbabwe imetoa fursa kwa wachimbaji wadogo wa madini nchini kwenda kuchimba katika nchi yao baada ya kuhakikishiwa na Dkt. Kambamura.

Naibu Waziri wa Madini wa Zimbabwe na ujumbe wake wamemaliza ziara ya siku tano katika mkoa wa Mwanza, Geita na Shinyanga ambayo ililenga kujifunza masuala mbalimbali katika Sekta ya Madini nchini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news