Waziri Biteko apokea taarifa ya maendeleo ujenzi wa jengo Soko la Madini ya Tanzanite

NA TITO MSELLEM-WM

WAZIRI wa Madini,Dkt.Doto Biteko amepokea taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa jengo la soko la madini ya Tanzanite lililopo katika Mji wa Tanzanite Mirerani uliopo wilayani Simanjiro mkoa wa Manyara ambapo amemtaka mkandarasi wa zabuni hiyo kuongeza kasi ili mradi huo umalizike kwa wakati.
Dkt. Biteko ametoa kauli hiyo baada ya kutembelea ujenzi wa jengo hilo unaondelea katika Mji wa Tanzanite Mirerani wilayani Simanjiro ambao ulianza tarehe 22 Mei, 2022 na unatarajiwa kukamilika Mei, 2023 ambapo utaghalimu zaidi ya Tsh. bilioni 5.49.

“Haya ni maono aliyokuwa nayo Mhe. Rais wetu Samia Suluhu Hassan ya kutaka kuona mji huu unapata hadhi yake kama eneo ambalo Tanzanite inachimbwa, ukienda Geita utakuta mji huo umechangamshwa na dhahabu hivyo na Mirerani lazima inufaike na Tanzanite iliyopo katika eneo lake,” amesema Dkt. Biteko.
Awali, Dkt. Biteko alikutana na viongozi wa wachimbaji wadogo wa madini ya Tanzanite, Mabroka, wafanyabiashara wakubwa wa Tanzanite (Dealers) na viongozi wa Eneo Tengefu la Mirerani ambapo aliwataka washiriki kikamilifu katika kutoa maoni yao kuhusiana na maandalizi ya rasimu ya Kanuni za biashara ya Tanzanite.

Aidha, Dkt. Biteko amesema Mwaka wa Fedha 2021/22 Mchango wa Wachimbaji Wadogo wa Madini umeongezeka kufikia asilimia 44 kwenye Pato la Taifa ikilinganishwa na asilimia 30 ya Mwaka wa Fedha 2020/21.

Kwa upande wake, Mbunge wa Simanjiro Christopher Ole-Sendeka amempongeza Dkt. Biteko kwa kuiongoza vyema Wizara ya Madini ambapo amemshukuru kwa kuendelea kuwashirikisha wadau wa madini kutoa maoni yao ili kuandaa rasimu ya Kanuni mpya za biashara ya Tanzanite.
“Udhibiti wa madini haya unakwenda vizuri lakini ombi langu ni kwamba, kituo cha utalii wa madini kijengwe Mirerani sababu Serikali imewekeza fedha nyingi hapa na isitoshe madini ya Tanzanite yanapatikana Mirerani pekee na ukizingatia uwanja wa ndege wa kimataifa wa KIA upo karibu na Mirerani,” amesema Sendeka.

Naye, Mwenyekiti wa Chama cha Mabroka nchini (CHAMMATA) Jeremiah Simon ametoa maoni yake kwa Dkt. Biteko ambapo ameshauri kwamba, Serikali iruhusu biashara ya madini ya Tanzanite yaliyoongezewa thamani ifanyike katika masoko ya madini ya hapa nchini ambapo kwa sasa Sheria ya Madini inasema biashara ya Tanzanite ifanyike Mirerani pekee.

“Madini ya Tanzanite hayaruhusiwi kutoka Mirerani kwenda kwenye masoko ya nje ya hapa, naomba zuio hili litolewe ili tuweze kuyatangaza madini yetu na pia, madini yakiongezewa thamani yaende kwenye masoko mbalimbali isiwe Mirerani pekee,” amesema Simon.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news